Thursday 14 April 2016

KOSA LA KUTOA USHAHIDI WA UONGO.

Image result for WITNESS  IN   COURT

NA  BASHIR  YAKUB  - 

Kutoa  ushahidi wa  uongo  ni  kosa.  Ni  kosa  lenye  adhabu kisheria. Ushahidi  wa  uongo  ni  pamoja  na  kupanga   au  kupangiwa  la  kusema  mahakamani  wakati  mkijua  kuwa  sio  la  kweli. Kosa  hili  ni  moja  ya  makosa  yanayotendwa  mno  tena  kiholela. Ni  kawaida  watu  kupanga  waseme  nini  mahakamani  huku  wakijua  wanachopanga sio  cha  kweli.  

Suala  la  ushahidi   wa  uongo halijalishi  kesi  ni  ya  aina  gani.  Iwe  jinai  au  madai  shahidi  anawajibika  kuwa  mkweli  daima. Kisichotakiwa  ni  kusema  uongo   ambao  hupotosha  usimamizi  bora wa  haki.

1.NAMNA  YA  KUWACHUKULIA  HATUA  SHAHIDI  WAONGO.

Ni  wajibu  wa  mtu  wa  upande  wa  pili  katika  kesi  kuchukua hatua  dhidi  ya  shahidi  msema  uongo. Ikiwa  uko  upande  wa  pili  wa  kesi  na  shahidi  wa  upande  mwingine  anatoa  ushahidi  wa  uongo  dhidi  yako  ni  wajibu  kwako  kuchukua  hatua  haraka  sana.

Hatua  inayofaa  ni  hii   ya  kutoa  taarifa  polisi au kwa hakimu/jaji  husika ili kumfungulia  mashtaka  shahidi  kwa kusema  uongo.

2.  KOSA  LA  KUTOA USHAHIDI  WA  UONGO  KATIKA  SHERIA.

Kifungu  cha  102  cha  Kanuni  za  adhabu  kinasema  kuwa   mtu  yeyote  wakati  wa  kufungua  shauri  au  wakati shauri  likiendelea,  kwa  kujua  akatoa  ushahidi  wa  uongo  kuhusu suala lolote  katika  kesi   atakuwa  ametenda  kosa.  

Hiki  ndicho  kifungu  cha  sheria  kinacholitangaza  tendo  la  kutoa  ushahidi wa  uongo  kuwa  kosa( perjury).

3.  HAIJALISHI   USHAHIDI  ULITOLEWA KWA KIAPO AU   BILA  KIAPO.

Kawaida  upo  ushahidi  unaotolewa  kwa  kiapo  na upo  usiotolewa  kwa  kiapo.  Ushahidi  kutolewa  kwa kiapo  ina  maana  shahidi  ataapa  kabla  ya  kusema  lolote   kama  shahidi. Na  bila  kiapo  shahidi hataapa. 

Kwahiyo  iwe  ushahidi  ulitolewa kwa kiapo  au  bila  kiapo  ikiwa  ni  wa uongo   hakuna  kinga  isipokuwa  litakuwa  kosa  tu.  Wapo  wanaodhani  ukitoa  ushahidi  bila  kiapo  basi  hata  uwe  wa  uongo  itakuwa  haina  shida.  Si  kweli  kosa  linabaki  palepale.

4.  USHAHIDI  UWE  WA  MDOMO  AU  MAANDISHI  BADO  NI  KOSA.

Ushahidi  waweza  kutolewa  kwa  namna  mbili. Unaweza  kutolewa  kwa  mdomo  au  kwa  maandishi.  Ushahidi  kwa  mdomo  ni  pale  mtu  anapohojiwa  na  akazungumza  mbele  ya  mahakama. 

Wakati  ule  wa  maandishi  ni  ule unaotolewa kwa kuandika.Shahidi anaweza  kuandika  mwenyewe au  wakili  wake nje  ya  mahakama.  Kisheria  huu  wote  ni  ushahidi  na  wajibu  wa  kusema  kweli  unabaki  palepale.

5. KUSAIDIA AU  KUSHAURI  KUTOA  USHAHIDI  WA  UONGO  NALO  NI  KOSA.

Kifungu  cha  102 ( 2 )  cha kanuni  za  adhabu   kinasema  kuwa  mtu  yeyote  ambaye  atasaidia , atashiriki, atashauri, atatuma  au  kushawishi  mtu  mwingine  kutoa  ushahidi  wa  uongo  atakuwa  ametenda  kosa  la  kushawishi kutoa  ushahidi  wa  uongo.

Huyu  hatashitakiwa  kwa  kutoa  ushahidi  wa  uongo  bali  kushawishi  kutoa  ushahidi  wa  uongo.

6.  ADHABU  YA  KUTOA  USHAHIDI  WA  UONGO.

Kifungu  cha  104  cha  kanuni  za  adhabu  ndicho  kinachotoa  adhabu  kwa  yote  mawili, yaani  kutoa  ushahidi  wa uongo  na  kushawishi  kutoa  ushahidi  wa  uongo.
Kinasema  kuwa  mtu  yeyote  ambaye  atatenda  kosa  la  kutoa  ushahidi  wa uongo au  kushawishi  kutoa  ushahidi  wa  uongo   atawajibika  kwa  adhabu  ya  kifungo  cha  miaka  saba.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com




0 comments:

Post a Comment