Monday 11 April 2016

UTAKAPOFANYA HAYA UTAHESABIKA KUTENDA UHAINI.


Image result for PINGU MKONONI
NA  BASHIR  YAKUB - 

Uhaini  ni  kosa  la  jinai .  Ni  kosa  kati  ya  makosa  makubwa  ya  jinai.  Katika  jinai  yapo  makosa  makubwa  na  yapo  makosa  madogo.  Yumkini  udogo  na  ukubwa    wa  kosa  waweza  kupimwa  kwa   kutizama  adhabu  ya  kosa.  Kosa  ambalo  huadhibiwa  kwa  adhabu  ndogo   huwa  ni  kosa  dogo  na  lile  ambalo  huadhibiwa  kwa  adhabu  kubwa  huwa   ni  kosa  kubwa.

1.NI  SHERIA  IPI  HUELEZA  MAKOSA  YA  JINAI.

Sheria  zinazofafanua  makosa  ya  jinai  zipo  nyingi.  Hakuna  sheria  moja  katika  makosa  ya  jinai.  Hata  hivyo  sheria  kuu  katika  makosa  ya  jinai ipo.  Ni  sheria  inayojulikana  kama  kanuni  za  adhabu( penal  code).  Hii  ni  sheria  kuu  katika  makosa  ya  jinai. 

Ni  sheria  inayoeleza  karibia  makosa  yote ya  jinai.  Mbali   na  sheria  hiyo  pia  zipo  sheria nyingine kama  za  kuzuia  na  kupambana  na  rushwa, sheria  ya  uhujumu  uchumi, sheria  ya  ugaidi na  nyinginezo.  Hizi  nazo hueleza  makosa  ya  jinai. 

Tofauti  kubwa  kati ya sheria  hizi  na  ile  ya  kanuni  za  adhabu  ni kuwa  hizi  sheria  nyinginezo  hueleza  makosa  rasmi  ya  jinai. Kwa  mfano  sheria  ya  ugaidi  itaeleza  mambo  ya  ugaidi  tu  na  si vinginevyo,  sheria  ya  uhujumu  uchumi  itaeleza  makosa  yanayotokana  na  uchumi  tu  na  si vinginevyo,  sheria  ya  utakatishaji  fedha  itaeleza  utakatishaji  fedha  tu  na  si  vinginevyo.

Wakati  sheria  ya  kanuni  za  adhabu  ndani  mwake  utakuta  makosa  tofauti  tofauti  ya  jinai.  Utakuta  makosa ambayo  hayafanani na yasiyokuwa na  uhusiano. 
Utakuta  kuhusu  kubaka,  kuiba, kupigana, kuua, kuharibu  mali, rushwa, kughushi ,  uhaini  na  mengine  mengi. Kwahiyo  kwa  mtu anayehitaji  kuyajua  makosa  ya  jinai  basi na  asome  sheria  ya  kanuni  za  adhabu.

2.  UKIFANYA  HAYA  UTAKUWA   UMETENDA  UHAINI.

( a ) Kifungu  cha  39 ( 1 )  cha  kanuni  za  adhabu  kinasema  kuwa  mtu  yeyote  ambaye   yumo  ndani  ya  Jamhuri  ya  muungano  au  popote  akajaribu  kumuua  rais   atakuwa  ametenda uhaini.

( b ) Pia  mtu  yeyote  aliye  ndani  ya  Jamhuri  ya  muungano  au  popote  na  akaanzisha  vita  dhidi  ya   Jamhuri  ya  muungano  atakuwa   naye  ametenda  kosa  la  uhaini.

( c ) Mtu  yeyote  ambaye  yuko  ndani  ya  Jamhuri  ya  muungano  au popote ambaye  atajenga,  kusababisha  au  kuwezesha,  kuchochea,  kushawishi,  kushauri, kuhusu  kifo, kumlemaza, kumzuia,  au  kufungwa  kwa  rais  atakuwa  ametenda  uhaini.

( d ) Mtu  yeyote  ambaye  yuko  ndani  ya  Jamhuri  ya  muungano au popote ambaye  atajenga,  kusababisha  au  kuwezesha,  kuchochea,  kushawishi,  kushauri  kumwondoa  rais  madarakani  visivyo  halali  atakuwa  ametenda  uhaini.

( e ) Mtu  yeyote  ambaye  yuko  ndani  ya  Jamhuri  ya  muungano au popote  ambaye  atajenga,  kusababisha  au  kuwezesha,  kuchochea,  kushawishi,  kushauri   kumwondolea  rais  heshima  na  jina  la  mkuu  wa  nchi,  amiri  jeshi  mkuu,  au  kiongozi  wa  serikali  atakuwa  ametenda  kosa  la  uhaini.

( f ) Mtu  yeyote  ambaye  yuko  ndani  ya  Jamhuri  ya  muungano  ambaye  atajenga,  kusababisha  au  kuwezesha,  kuchochea,  kushawishi,  kushauri  kupindua  serikiali  iliyo  madarakani, kutishia   serikali, bunge  au  mahakama  atakuwa  ametenda  kosa  la  uhaini.

3.  NI  IPI  ADHABU  YA  KOSA  LA  UHAINI.

Vifungu  vya  39  na  40  vya kanuni  za  adhabu  ambavyo  vimeeleza  ni  matendo gani  yanaweza  kuitwa  uhaini  vimeeleza  pia  adhabu  ya  matendo  hayo. Vimeeleza  kuwa  adhabu  ya  kukutwa    na  hatia  ya  uhaini   ni  kifo. Uhaini  ni kati  ya  makosa  machache  sana  ambayo  adhabu  yake  ni  kifo.

Kwahiyo  kwa  namna  yoyote  ukijihusisha  na tendo lolote kati ya matendo yaliyotajwa  hapo  juu  ndipo  utahesabika  umetenda  uhaini na  adhabu  yake  ni  kifo  ikiwa  itathibitika  mahakamani. Kila  kilichoelezwa  hapo  juu  katika A – F ni  tafsiri  halisi ya  uhaini.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com




0 comments:

Post a Comment