Thursday 21 April 2016

MAMBO MANNE MUHIMU KUHUSU UMILIKI WA MALI KWA WANANDOA.

Image result for WANANDOA

NA  BASHIR  YAKUB - 

Baadhi  ya  wasomaji  wameuliza maswali  mengi  kuhusu  habari  ya  umiliki  wa  mali  kwa  wanandoa. Wanataka  kujua  ipi  mali  ya  ndoa  na  ipi  siyo, wanataka kujua   mali  unayokuwa  nayo  kabla  ya  ndoa  inahesabika  vipi  baada  ya  kuingia  nayo  katika ndoa, wanataka  kujua  uuzaji  wa  mali  za  ndoa,  wanataka  kujua  kigezo  kinachozingatiwa  katika  kugawana  mali ndoa  inapovunjika, wanataka  kujua  iwapo   inawezekana kuwa  na umiliki  wa  pekee  wa  mali   wakati  upo  katika  ndoa,  wanataka  kujua  haki  ya mali kwa  ndoa ya  mke  zaidi  ya  mmoja, wanataka  kujua  nani  kati  ya  mume  na  mke  ana  haki  zaidi  ya  mali  na  mengine  mengi.

Haya  yameulizwa  na  watu  tofauti  lakini  kwa  wingi. Hata hivyo mengi  yake  yalikwisha elezwa hapa.  Mengi  yameelezwa  katika  makala  tofauti zilizopita.  

Tunaamini  wapo  walioona  na  wengine  hawakuona. Kwasababu  hiyo  hakuna  ubaya  kujibu  tena  maswali  ya  aina  hii  ili   hata ambao  hawakubahatika  kusoma  waweze  kusoma  leo.

1.JE  NDOA  INAPOVUNJIKA NI  KIGEZO  KIPI  HUTUMIKA  KATIKA  KUGAWA  MALI  ZA  WANANDOA.

Iliwahi  kuelezwa  hapa  kuwa  wengi  wanajua kuwa  katika  kugawana  mali  za  ndoa  pale  ndoa  inapovunjika  kigezo  kinachotumika  ni  cha  asilimia. Wanajua  kwamba  sheria  imeeleza  wazi  kuwa  kuna  asilimia  fulani  anatakiwa  kupata  mwanamke  na  asilimia  fulani  mwanaume.

Hili  si  kweli  kwani  kigezo  kikubwa  kinachotumika  ni  kigezo  cha   nguvu au  juhudi  za  pamoja  katika  upatikanaji  mali( joint  effort) husika. Juhudi  za  pamoja  huangaliwa mchango  wa  kila  mmoja  katika  upatikanaji   au  uendelezaji  wa  mali  husika.  

Na  juhudi  za  pamoja  sio  tu pesa  au  mali  bali  pia  hata  kazi  za  nyumbani  nazo  ni  sehemu  ya  juhudi  za  pamoja  katika  kupatikana  kwa  mali.
Kwahihyo  juhudi  ya kila  mmoja  itapimwa  na  mali  zitagawanywa. Mahakama  ndio  chombo  chenye  mamlaka  na  kazi hiyo.

2. JE MALI UNAYOINGIA  NAYO  KATIKA NDOA  INABADILIKA  NA  KUWA  YA  WOTE.

Kifungu  cha 58  cha  sheria  ya  ndoa  kinasema  kuwa  ndoa  haitatumika  kubadilisha  umiliki  wa  mali  isipokuwa  kama  kuna  makubaliano maalum  au  vinginevyo.
 Hii  ina  maana  ndoa  tu  haibadilishi  umiliki  na  kuufanya  kuwa wa  pamoja.  Mali  inaweza  kuwa  ya  mtu  mmoja  awe  mke  au  mme  labda iwe vingenevyo  kuwa  kuna  makubaliano  maalum  kuwa  mali  hii  itakuwa  ya  wote.

Pia  kunaweza  kusiwe  na  makubaliano  hayo  lakini  mmoja  akawa  amechangia  katika  kuiendeleza  mali  ile. Hapo  napo  inaweza  kuwa  ya  wote.  Lakini  kinyume  na  hayo  mali  inaweza kuendelea  kuhesabika  ni  ya  mmoja  kati  ya  mke  au  mme  hata  kama  wako  kwenye ndoa.

3. JE  HAKI  YA  MALI  IKOJE  PENYE   MKE  ZAIDI  YA  MMOJA.

Kifungu  cha  57  cha  sheria  ya  ndoa  kinasema  kuwa   ili  kuondoa  shaka  inapotokea  mme  ana  mke  zaidi  ya  mmoja basi  wake  hawa  watahesabika  wana  haki  sawa , hadhi  sawa  na dhima  sawa. Isipokuwa  sasa  suala  la  mali ikiwa  ndoa  ya  mmoja  au wote itavunjika   basi  kila  mtu  atapata kutokana  na  mchango  wake  katika  kupatikana  hizo  mali.

4.  JE MWANANDOA ANAWEZA KUUZA  MALI   BILA  RIDHAA  YA  MWENZAKE.

Kifungu  cha  59   cha  sheria  ya  ndoa  kinasema  kuwa  mali  ardhi  inapokuwa  inamilikiwa  na mume  au  mke  wakati  ambapo  ndoa  ikiendelea   basi  mmoja   kati  ya  wanandoa  hao  hataruhusiwa  kuuza,  kutoa  zawadi, kuweka  rehani,  au  kupangisha .

Na  ikitokea  akafanya  hivyo  basi  yule  ambaye hakuhusika  naye atahesabika  kuwa  na  maslahi   yanayompa  haki  ya  kuzuia(caveat)  hicho  kilichofanyika.
Kwa  leo  ni  hayo  mengine  yataelezwa  katika makala  nyingine.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

 



      

0 comments:

Post a Comment