Tuesday 29 March 2016

WITO WA MAHAKAMA KWA WANAJESHI NA WALIO NJE YA NCHI.


Image result for SUMMONS
NA  BASHIR  YAKUB - 

Mtu  anaposhtakiwa/kulalamikiwa  hutakiwa  kufika  mahakamani.  Lakini  atafikaje  mahakamani  bila  kujua  kama  ameshitakiwa. Ni  lazima  kuna  utaratibu  wa  kumjuza  mtu  kuwa   kuna  shitaka   dhidi  yako. Na  utaratibu  ambao  hutumika  si  mwingine  bali  ni  kumtumia   mtu  wito  maalum ambao  hujulikana  kama  summons.  

1.UTARATIBU  WA  SUMMONS  KWA   MAKUNDI  MAALUM.

Wito  au  summons  ya  kuitwa  kuhudhuria  shauri  baada  ya  kushitakiwa  hutolewa  kwa  namna  tofauti  kutegemea  na  aina  na  mazingira  aliyomo  muitwaji.  Upo  utaratibu  wa  wa  summons  kwa  mtu  wa  kawaida,  utaratibu  kwa  mtu  aliye  nje  ya  nchi, utaratibu  kwa  mtu  aliye  nje  ya  wilaya  au  mkoa, utaratibu  kwa watumishi  wa  vyombo  vya  ulinzi, utaratibu  kwa  mtu  asiyejulikana  alipo, n.k. Baadhi ya tofauti  hizi  ndizo  zitakazotizamwa  katika  haya makala.

2.  SUMMONS  HUTOLEWA   WAKATI  GANI.

Summons/wito  haitolewi   tu wakati  mtu anapofunguliwa  shauri .  Bali  hutolewa  hata  kwa  mashahidi, hutolewa  kabla  ya  hukumu  kwa  yule  ambaye  hakuhudhuria  kesi ambayo  imesikilizwa  upande  mmoja, hutolewa  kama  ukumbusho kwa  mtu  ambaye  alikuwa  akihudhuria  mahakamani  lakini  baade  akaacha, n.k.

3.  WITO/SUMMONS  KWA  ALIYE  NJE  YA  TANZANIA.

Amri  ya  “v”   kanuni  ya 29 ya  sheria  ya  mwenendo  wa  mashauri  ya  madai  imetofautisha  watu  walio  nje  ya  nchi. Watu  walio  nchi  za  jirani  kama Uganda, Kenya, Malawi, Msumbiji,  na Zambia  imewawekea  utaratibu  tofauti  na  wale  ambao wako nje ya  nchi  lakini sio  katika hizo  zilizotajwa.

Hapa  tunaongelea  wale  ambao  hawako  katika  nchi  hizi za jirani.  Hawa   sheria  hii  imesema  kuwa  wanaweza  kuitwa  kufika  nchini  katika  mahakama  husika ili  kukabiliana  na mashtaka  yao.  Sheria  imeeleza  kuwa  hawa  wanaweza  kuitwa  kwa  njia tatu. Kwanza   kwa  njia ya  posta  ambapo  summons  itamfikia  moja  kwa  moja  mhusika  au  kupitia  mtu  anayetumia  naye  sanduku  la  barua.  Hii  ni  njia  nzuri  na  ya  uhakika  zaidi.

Pili  ni  kwa  njia  ya  wakala.  Hii  zaidi  ni  pale  ambapo  mshitakiwa  atakuwa  ni  kampuni au  taasisi.  Ikiwa  ana  wakala   hapa  nchini  basi  summons  hiyo  anaweza  kupewa wakala  na  ikahesabika  kuwa  ametaarifiwa na  hivyo  kuondoa  lawama  kwa kinachoweza  kutokea  mbeleni.

Tatu  ni  kwa kutumia  mahakama  iliyo  katika  nchi  ambamo  mshitakiwa  anaishi. Kwa  mfano  kama  yuko  Texas marekani  basi  mahakama  ya  Tanzania  inaweza  kuitumia  summons  mahakama  ya  Texas  ambayo itafanya utaratibu wa  kumpatia mshitakiwa. Hivi  ndivyo  mshitakiwa  aliye  nje  ya  nchi  anavyoweza  kupewa  wito/summons.

4.  WITO/SUMMONS  KWA  MWANAJESHI.

Amri  ya  “v”   kanuni  ya 26 ya  sheria  ya  mwenendo  wa  mashauri  ya  madai  inasema  kuwa  ikiwa  mlalamikiwa/mshitakiwa  ni  mwanajeshi  wa  Jamhuri  ya  Muungano  wa  Tanzania  basi  wito  wake  unatakiwa   kupelekwa  kwa  mkuu   wake  wa  kazi( commanding  officer).  Hautatakiwa  kumpa  yeye  moja  kwa  moja  isipokuwa   utapitia  kwa  mkuu  wake  na  kumfikia  yeye  mlengwa.

Mbali  na  wanajeshi  sheria  hiyo  inasema  pia  kuwa  mtu  aliye  katika  magereza  anaweza  pia  kupewa  wito  ikiwa  analo  shauri  jingine  la  kujibu  tofauti  na  lile  lililomuweka  ndani.  

Sheria  hiyo  inasema  kuwa  wito  wake  atapatiwa  mkuu  wa  magereza   wa  eneo  alipo  mshitakiwa.  Nakala  zitakuwa  mbili  ambapo  nakala  halisi  atapewa  mkuu  wa  magereza  husika  na nyingine  atapewa  mhusika  mwenyewe  lakini  kupitia  mkuu  huyo  wa  magereza.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com






0 comments:

Post a Comment