Thursday 10 March 2016

KUENDELEZA SHAURI ALILOACHA MAREHEMU ILI KUPATA ALICHOKUWA AKIDAI.


Image result for MAREHEMU

NA  BASHIR  YAKUB -

Makala  haya yanaeleza  wakati  ambapo  ndugu   anafariki  huku  akiacha  shauri  mahakamani   ambalo  alikuwa  akidai  kitu fulani kama  haki  yake.  Yaweza  kuwa  alifungua  kesi  kudai  ardhi,  nyumba,  mirathi,  mgogoro  wa  kimkataba, fidia,  na  madai  mengine  yote. Makala  yatatizama  uwezekano  wa  ndugu  kuendeleza  madai  haya   ili  kuona namna ya  kupata  kile  alichokuwa  akidai  marehemu.

1.ISEMAVYO  SHERIA.

Amri ya  22  kanuni  ya 1 –  12  Sheria  ya  mwenendo  wa  mashauri  ya  madai  ndiyo  inayozungumzia  jambo  hili.  Katika  kanuni  hizo  si  tu  imezungumzwa  haki  ya  marehemu  mlalamikaji  bali  pia  haki  ya  marehemu  mlalamikiwa/mdaiwa.  

Kanuni  ya  1 inasema  kuwa  kifo  cha  mlalamikaji/mdai  au  mlalamikiwa/mdaiwa   hakiui  shauri  ikiwa   haki  ya kulalamika  bado  haijafa.  

Maana  yake  ni  kuwa  kuna  wakati  mdai  anakufa  lakini  haki  yake  ya  kuendelea  kudai  alichokuwa  akidai  inaendelea  kuishi  na  kuna  wakati  akifa  anakufa  na  haki  yake  ya  kudai. Ni  wakati  gani  akifa  anakufa  na  haki  yake  ya kudai na  ni  wakati  gani  akifa  haki  yake  inaendelea  kuishi  tutaona  hapa  chini.

2. KUENDELEA   KUISHI  KWA  HAKI  YA  MADAI  NA  KUFA  KWA  HAKI  YA  MADAI.

Kuendelea  kuishi  kwa  haki  ya  madai  maana  yake  ni  kuwa  ndugu  wa  marehemu  hasa  msimamizi  wa  mirathi  anapata  haki  ya  kuendeleza  shauri  na  kudai  kilekile  alichokuwa  akidai  marehemu.  

Na  kufa  kwa  haki  hiyo  maana  yake  ni  kuwa  hakuna  ndugu  yoyote  kutoka  upande  wa  marehemu  akiwemo  msimamizi  wa mirathi  atayekuwa  na  haki  ya  kudai  au  kuendeleza  shauri  ili  kupata  kile  alichokuwa   akidai  marehemu. 

Hali  ni hiyohiyo   kwa  upande  wa  mlalamikiwa/mdaiwa  aliyefariki. Kwani  kuna  wakati  ndugu  watalazimika  kurithi   shauri  ambalo  alikuwa  ameshitakiwa  nalo  na  kuna  wakati   hawatalazimika.

3.WAKATI  NDUGU  WA  MAREHEMU MDAI/MLALAMIKAJI  WANAPORUHUSIWA  KUENDELEZA  MADAI.

Ili  kujua  kama  ndugu  waendeleze  shauri  au  lah  kinachoangaliwa  ni  aina  ya   shauri  alilokuwa amefungua marehemu. Ikiwa  alifungua  shauri  binafsi( personal)  au  lenye  viini  vya  ubinafsi(individuality)   basi  shauri  hilo  haliwezi  kuendelezwa  na  ndugu  wa  marehemu. 

Lakini  kama  shauri  sio  binafsi  basi  ndugu  wataliendeleza  na  hatimaye  kupata  alichokuwa  akidai  marehemu.  Mashauri  ambayo  sio  binafsi  ni  kama  kudai  ardhi, nyumba, mirathi,  madai  yatokanayo  na  mikataba,  na  madai  mengine  ya  kudai  mali.

Haya  ndugu  wa  marehemu   wanaruhusiwa  kuyaendeleza  ili  kupata  alichotakiwa  kupata  marehemu.

4.WAKATI  NDUGU  WA  MAREHEMU  MDAI/MLALAMIKAJI  WANAPOZUIWA KUENDELEZA  MADAI.

Hapo  juu  tumeona ndugu  wa  marehemu  wakiruhusiwa  kuendeleza  madai  na  sasa  hapa  tunaona  wanapozuiwa  kuendeleza  madai.  Tumesema  hapo  juu  kuwa  ikiwa  mlalamikaji/mdai  ambaye   sasa  ni  marehemu  alifungua  shauri  binafsi( personal) au  lenye  viini  vya  ubinafsi(individuality)  basi  ni  wakati  huo  ambapo  ndugu  wa  marehemu  wanakosa  haki  ya  kuendeleza  shauri  kama  hilo.  

Mashauri   binafsi au yenye  viini  vya  ubinafsi  ni  kama   mashauri  ya  fidia labda  kudai  fidia baada  ya  kupigwa,  kutukanwa,  Kudhalilishwa, kufunguliwa  mashtaka  ya  hila,  kusababisha  kufungwa  bila  sababu  za  msingi    na  mashauri   mengine  yanayofanana na  hayo.  

Mashauri  ya  namna hii hufa  baada  ya  mdai  kufa. Hayana  uhai  baada  ya  uhai  wa  mdai na hivyo  ndugu  hawawezi  kuyaendeleza.

Hata  hivyo  ikiwa  shauri  la  namna  hiyo  lilikuwa  limesikilizwa  tayari    na  inasubiliwa  hukumu  halafu  ndio  mdai  akafa  basi  hukumu  itatolewa  na  ndugu  wa  marehemu  watatakiwa  kulipwa  kile  alichostahili  kulipwa  marehemu  ikiwa  ameshinda.

Pia  ikiwa  marehemu  atakufa  baada  ya  hukumu  kutolewa  na  kabla  ya  utekelezaji(execution)  napo  ndugu watendeleza  kupata  kile  alichostahili  kupata  marehemu.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment