Monday 1 February 2016

MGAWANYO WA MALI ZA MAREHEMU.


Tokeo la picha la WAKIWA MSIBANI\
NA  BASHIR  YAKUB -

Mgawanyo  wa mali  za marehemu   hutegemea   mambo  makubwa  mawili. Kwanza  ni  ikiwa  marehemu  ameacha  wosia  na  pili  ni  ikiwa  hakuacha  wosia.  Ikiwa ameacha  wosia  basi  huwa ni rahisi  sana kwani mali  zake  zitagawanywa  kwa  kufuata  wosia.  Ikiwa  hakuacha  wosia  hapa  huwa  si  kwepesi  sana kwani  mali  zake  hulazimika  kugawanywa  kwa  mujibu  wa  sheria  zilizopo  wakati  sheria zenyewe  ziko  tatu  tofauti. Wakati  mwingine ni  kazi  kidogo  kuamua  sheria  ipi  itumike  katika  kugawa  mali  za  marehemu.

1.SHERIA  IPI  ITUMIKE  KATIKA  KUGAWA  MALI  ZA  MAREHEMU.

Ikiwa hakuna  wosia  swali  la  sheria  ipi  itumike  katika  kugawa  mali  za  marehemu  lazima  liibuke.  Kwa  ujumla  kuna  sheria  tatu  zinazotumika  katika  kugawa  mirathi.

( a )  Sheria  ya  kwanza  ni  sheria  ya  urithi  ya  India 1865 .  Hapa  kwetu  sheria  hii hujulikana  kwa  wengi  kama  sheria  ya  mirathi  ya  serikali.
Sheria  hii  hutumika  kwa marehemu  ambaye hakuishi maisha  ya  kiislam  na hakuishi  maisha  ya  kimila. 

 Zaidi  tunaweza  kusema  kuwa  sheria  hii  hutumika  kwa  wakristo na  madhehebu  mengine  ambayo  sio   ya  kiislam.Hata  hivyo  hata  muislam  ambaye  itathibitika  kuwa hakuishi  maisha  ya  kiislam  wala  ya  kimila  sheria  hii itatumika  kugawa  mali  zake.

( b ) Pili  ni  sheria  ya kiislam.  Sheria  hii  hutumiwa  na waumini  wa  dini  ya  kiislamu. Lakini  haitoshi  kusema inatumiki  kwa  waislam  isipokuwa  inatosha  kusema itatumika kwa waliokuwa wakiishi  maisha  ya  kiislam. Sheria  hii  hufuata  misingi  ya  Quran  tukufu  na  Sunnah.

( c ) Tatu  ni  sheria  za  kimila. Sheria  hizi  hutumika  iwapo  marehemu  aliishi  maisha  ya  kimila. Mfano  wake  ni  kama  tunavyoona  kwa wamasai, wahadzabe,  na  makabila  mengine  hasa  vijijini  ambao huishi  maisha  yao  yote pasi  na  kufuata  dini  yoyote  isipokuwa  mila  tu. Sheria  hii  imo  katika  kanuni   za urithi,  tangazo  la  serikali  namba  436  la  mwaka  1963.

Kwa ujumla  swali  la   sheria  ipi  itumike   kugawa mali  za  marehemu  pale  ambapo  hakuacha  wosia,  hujibiwa  kwa   kuangalia  aina  ya  maisha  aliyoishi  marehemu.

2.  KUGAWA  MALI  KWA  SHERIA  YA  SERIKALI.

Tumesema  sheria  hii inaitwa  Sheria  ya  urithi ya  India  ya  1865 ( India  Succesion  Act 1865) ila  wengi  huiita sheria  ya  serikali.
Kwa  kutumia  sheria  hii kama  marehemu  ameacha  mjane  na  watoto, mjane atapata  1/3  na  watoto/mtoto 2/3  ya  mali  yote.

Kama  marehemu  hakuacha  watoto  basi mjane  atapata  ½  na  ½  inayobaki  huenda  kwa wazazi,  dada,  kaka  wa  marehemu.

3.  KUGAWA  MALI  KWA  SHERIA  ZA KIISLAMU.
Warithi  wakuu  katika   sheria  za  kiislam  ni  mke/wake  wa  marehem, watoto  na  wazazi  wake  wawili.  Watoto  wa  kiume  hustahili  kupata  mara  mbili  zaidi  ya  wale  wa  kike .

Wajane  wa marehemu  wasiozidi  wanne  hutakiwa  kupata  1/8 ikiwa   marehemu  kaacha  watoto. Ikiwa  hakuacha watoto/mtoto  wajane  watatakiwa  kupata  ¼   ya  mali  yote iliyoachwa.
Baba  na  mama  hupata  1/6 ya  mali  ya  marehemu.

4.  KUGAWA  MALI  KWA  SHERIA  ZA  KIMILA.

Misingi  ya  sheria  za  kimila imo  katika  tangazo  la  serikali  namba  436  la  mwaka  1963.
Kwa  mujibu  wa  sheria  hii  ikiwa  marehemu  ameacha  watoto  basi  hao  ndio  watakuwa  warithi  pekee. Kama  marehemu  hakuacha  watoto   basi  wazazi , kaka,  dada, shangazi,  wajomba  wa  marehemu  huwa  ndio  warithi.

Aidha  mtoto  wa  kiume  mkubwa  kutoka  nyumba  ya  kwanza  hupata  fungu  kubwa akifuatiwa  na  watoto  wengine  wa  kiume   na  mwisho  ni  watoto  wa  kike  kutoka  nyumba  yoyote  ambao  hupata  kidogo.  Sheria  za  kimila  hazitoi  haki  kwa  mjane  kurithi.

Hata  hivyo  suala  la  mjane  kutokurithi  linapingana  na  katiba  pamoja  na  sheria  nyingine  ikiwemo  sheria  namba  4  na  5  za  ardhi..
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.     0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com





0 comments:

Post a Comment