Monday 29 February 2016

JE UNAHITAJI KUPIMIWA ARDHI MJINI, FUATA UTARATIBU HUU.


Image result for UPIMAJI WA VIWANJA
NA  BASHIR  YAKUB - 

Tunapoongelea  upimaji   ifahamike  kuwa  upimaji  upo  wa  aina  nyingi.Kutokana na hilo upimaji  unaoongelewa  hapa  ni  upimaji  miliki. Lakini  pia  tunaongelea   upimaji miliki wa  ardhi  mijini na  sio vijijini. Upimaji wa  ardhi miliki ni  upimaji  ambao  lengo  lake  ni  kummilikisha  mtu  ardhi. Kummilikisha  mtu  ardhi  sio  kumuuzia  ardhi.  Kummilikisha  mtu  ardhi  ni  kutambua  ardhi  yake  kimipaka  na  kumpatia  nyaraka  mahsusi(specific)  inayohusiana  na  umiliki( hati).  

Kwa  maana  hii  wanaomiliki  ardhi  ambazo  hazijapimwa   hatuwezi  kusema  wamemilikishwa  ardhi . Haijalishi  ardhi  hizo  ni  za  kwao na  wamezinunua  kwa  pesa zao. Kwa  kusema  hivyo  haimaniishi  kuwa  ambao  hawana  hati  au  hawajapima  ardhi  zao  basi  sio  wamiliki,  hapana  isipokuwa  ni  kuwa  tu kwamba hawajamilikishwa  kisheria  na  mamlaka    za  serikali.

Kutokana  na  hilo   ardhi  iliyopimwa  na  ile  ambayo  haikupimwa  hutofautiana  hadhi na thamani kwa  kiasi  kikubwa.

1.NYARAKA  ZINAZOHITAJIKA   ILI  UPIMIWE  ARDHI.

( a )  Barua  kwenda  kwa  mkurugenzi.  Anayetaka  kupimiwa  ardhi   anatakiwa  kuandika  barua  kwenda  kwa mkurugenzi  wa  halmashauri  husika. Barua  ni  nyaraka  ya  kwanza  kabisa  ambayo unatakiwa  kuwa  nayo.  Ni katika  barua  hiyo  ambamo  utaeleza   nia  yako  ya  kutaka   kupimiwa  ardhi na  matumizi  ya  ardhi  yako kama  ni  makazi,kiwanda n.k.

( b ) Kuambatanisha  mkataba  wa  mauziano.  Katika  hatua  hii  mkataba  wa  mauziano utatambuliwa kama nyaraka  ya  umiliki. Mkataba  huu  ndio  utakaokutambulisha  kama  mmiliki  wa  ardhi  husika. Huu  unaambatanishwa  kwasababu  mmiliki  wa  ardhi  ndiye  mwenye  jukumu  la  kuomba  kupimiwa. 

Hivyo  kuambatanishwa  kwa  mkataba  kunathibitisha  kuwa  mmiliki  ndiye  anayeomba  kupimiwa  kwa  mujibu  wa  sheria. Ni  vema  mkataba  wa  umiliki  ukawa  ni  ule   mkataba  wa  kisheria   ulioandaliwa  na  kushuhudiwa  na  mwanasheria.

( c ) Barua  iliyotajwa  hapo  juu  katika  “A”  hakikisha  ina  muhuri  wa  mwen yekiti  wa  serikali  za  mtaa,  sahihi  pamoja  na mhuri  wa  mtendaji. Mwenyekiti  na  mtendaji  atakayetumika  sio  wa  pale  unapoishi    bali  pale  lilipo  eneo  unalotaka  kupima.  Kama  eneo  lipo  unapoishi  basi  utamtumia  huyohuyo  wa  eneo  unaloishi.

2.   HATUA  ZA  KUPIMIWA.
Hatua  hizi  ni  muhimu  kuzifahamu kwakuwa  unapokuwa katika mchakato   huu  unahitaji sana  kujua  kazi  yako  imekwama  wapi  na  kwa  nani ili  kama   kulalamika  ujue  pa  kuanzia.  Wanaofanya  kazi  za  ardhi  watajua  namaanisha  nini.

( a ) Barua  niliyotaja    hapo  juu  itawasilishwa  kwa  mkurugenzi  wa  manispaa .  Barua  hiyo  itakuwa  imeambatanishwa  na nyaraka  nilizotaja  hapo  juu. Manispaa  inayotumika  siyo  ile  unayoishi  bali  ni  ile  lilipo  eneo  husika.

( b ) Baada  ya  barua  hiyo  kufika  kwa  mkurugenzi  basi  huwasilishwa  kitengo  cha  ardhi.  Kila  manispaa  ina  kitengo  cha  ardhi.  Hapo  hushughulikiwa  na  afisa  ardhi  ambae  kazi  yake  kubwa  itakuwa  ni  kuthibitisha  uhalali  wa  umiliki  wa  mwombaji.

( c )     Ikitoka  hapo  kwa afisa  ardhi  inaenda  mipango  miji. Afisa  ardhi  huipeleka  kwa  afisa  mipango  miji  kwa  fomu  ijulikanayo  kama  SF 47.  Kazi  kubwa  ya  afisa  mipango  miji  ni  kutizama  iwapo  eneo  linaloombwa  kupimwa  lipo  katika  ramani  ya   mipango  miji.Kama  limo  katika  ramani  basi  ataangalia  matumizi  aliyoomba  mwombaji  kama  yanafanana  na  yaliyoainishwa  katika  ramani  walizonazo.

( d ) Afisa  mipango  miji  akishathibitisha  na  kuhakiki  basi  atatuma  fomu  maalum  SF  47  kwa  afisa  ardhi  mteule. Huyu  kazi  yake  ni  kujaza  fomu  maalum  SF 37  ambayo  ni  ya  maombi  ya  kupimiwa  ambayo  ataiwasilisha  kwa  afisa  upimaji. Atafanya  hivyo kwa  kuambatanisha  ramani  husika.

( e ) Mwisho  mpima  ardhi  atatoa  maelekezo  kwa  mpimaji  mahsusi  ambaye  ndiye  sasa  atafanya  kazi  ya kuja  kufanya  vipimo  na  utapimiwa  ardhi  kwa  ajili  ya  usalama  na  kuipandisha  thamani  ardhi  yako.
Haya  yote  yatafanyika  kwa  kufuata sheria  namba  4  ya  ardhi  na  kanuni  zake .
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com


2 comments:

  • Unknown says:
    1 March 2016 at 21:25

    Ahsante kwa kunielewesha

  • Zacharia J Malley says:
    16 August 2018 at 03:54

    Je? Kama ardhi husika haijapimwa na bado yalijatengwa kwa shughuli fulani ya manispaa

Post a Comment