Monday 8 February 2016

FAIDA KUU NNE ZA KUWA NA HATI.


Tokeo la picha la HATI  YA  NYUMBA
NA  BASHIR  YAKUB - 

Masuala  yanayohusu  ardhi  ni  masuala  nyeti  sana.  Unyeti  wa  masuala  haya  unatokana  na  ukweli  kuwa  maisha yote  yamejengwa juu  ya  ardhi. Hakuna kilichowahi  kufanywa, kinachofanywa  na  kitakachofanywa nje  ya  ardhi. Iwe  kutembea,  kuendesha  kipando, kula, kulala, maendelezo  yoyote  ya  teknolojia, ujenzi,  maji  safi  na  salama, kupata  chakula, hata  unaporuka  hewani  iwe  kwa  ndege  au  kifaa  kinginecho  huwezi  kusema  sijatumia  ardhi kwakuwa hata  mruko  wenyewe(take off) huanza  na  ardhi.

Lakini pia hata  uruke  na  ukae  huko  miaka  200  bado  utatakiwa  kurejea ardhini.  Ardhi  ni  kila  kitu kwa  maana  ya  kila kitu.  Kupitia  msingi  huu  tunapata    umuhimu  mkubwa  wa  kueleza  kila  lililo  la  msingi  kuhusiana na masuala  ya ardhi  hususan umiliki wake.

Kupitia  makala  hizi   yalishaelezwa  mengi  kuhusu  namna  ya  kununua  ardhi,  namna  ya  kuepuka  migogoro  wakati  wa  ununuzi,  namna  ya  kubadilisha  hati  na  mengine . Fursa   ya  leo  itaeleza  umuhimu  na  faida  za  kuwa  na  hati.

1.NINI  MAANA  YA  HATIMILIKI .

Hati  miliki  ya  ardhi  hujulikana  pia  kama  “Title  Deed”.  Hatimiliki  ya  ardhi  ni  nyaraka  maalum  inayotolewa   na  wizara  ya  ardhi ikionesha  mwenye  haki  ya  umiliki wa  ardhi, eneo  na  kiasi  anachomiliki  huku  ikiainisha  wajibu  na  haki  alizonazo  mmiliki  huyo.

Wajibu  katika  hatimiliki  ni  yale  unayotakiwa  kutekeleza  kwa  mfano  malipo    ya  kila  mwaka,  matumizi  yaliyopangwa, na  kila  sharti  analotakiwa  kutekeleza  mmiliki.
Haki  katika  hatimiliki  ni  yale yote  anayostahili kupata  mmiliki  wa  ardhi  husika  ikiwemo  taarifa ( notice) rasmi  panapo  mabadiliko yoyote  katika  matumizi  na  umiliki, haki  ya  fidia,  na  haki  ya  kuwa   huru  katika  matumizi  halali.

2. TOFAUTI  YA  HATI, LESENI  ZA  MAKAZI,  NA  MIKATABA  YA  KUNUNULIA.

Wengi  wanajua  tofauti  ya  vitu  hivi  lakini  pia  wengi  hawajui  tofauti   ya  vitu  hivi. Wapo  wanaofikiri  mkataba  wa  kununulia ni  hati na hati ni leseni  ya  makazi  na  leseni  ya  makazi  ni  hati.

Tujue  kuwa hati  ni  waraka  ambao  hutolewa  na wizara  ya  ardhi  katika  maeneo  yaliyopimwa  wakati  leseni  ya  makazi  ni  nyaraka  ambayo  hutolewa  na  manispaa  hata  katika  maeneo  ambayo  hayajapinwa. Maeneo  ambayo  hayajapimwa  huitwa “ squarters”, na  kwa  kiswahili  kizuri  huitwa  maeneo/makazi  holela.  

Hapo hapo  mkataba  wa  kununulia  sio  hati  wala  sio  leseni  ya  makazi  isipokuwa   ni  hivyohivyo  tu  kama  jina  lilivyo  ni  mkataba  wa  kununulia(sale  agreement). Ni  muhimu  ijulikane  kuwa  hivi   ni  vitu  vitatu  tofauti.Mazingatio katika  vyote  hivi  ni kuwa hati  ni  nyaraka kubwa  kuliko hizi  nyingine  zote.

3.   FAIDA  KUU  NNE    ZA   KUWA  NA   HATI.

( a )  Faida  ya kwanza  kabisa  ni  usalama. Nenda  popote  iwe  wizara  ya  ardhi, mahakama  kuu ya  ardhi,  mabaraza  ya  ardhi  na  kila  mamlaka  inayohusiana  na  ardhi  utaambiwa   usalama  wa  ardhi  upo  kwa  mwenye  hati.

Zawadi  pekee  unayoweza  kuipatia  ardhi  yako  ni  ulinzi,  na  ulinzi  pekee ni kuitafutia  hati. Hii  ni  kusema  kuwa   ardhi  salama  ni  ardhi  yenye  hati. Hii  ni  faida  kuu  ya  kwanza  unayoweza  kupata  baada  ya  kuwa  unamiliki  hati.

( b ) Hati  hupandisha  thamani  ya  ardhi  haraka  mno.  Hii  ni  faida  nyingine  kubwa. Unaweza  kununua  ardhi  isiyo  na  hati  kwa  milioni  mbili  na  ukaiuza  milioni  hata  20  baada  ya  kuitafutia  hati. Wanaofanya  biashara  za  ardhi  hutumia  njia  hii  kujipatia  faida  kubwa. 

Hununua  maeneo  makubwa yasiyo  na  hati  kwa  bei  ndogo huyapimisha,huyakatakata  viwanja,  na  kuyatafutia  hati   halafu  huyauza  tena  kwa  bei  kubwa  zaidi. Ardhi  yenye  hati  ina  thamani  kubwa  mno.

( c ) Hati  ya ardhi  hutumika  kama  dhamana  mahakamani . Unapokuwa na  hati  si  tu  unamiliki  ardhi  bali  pia  unamiliki  mdhamini. Matatizo  yapo  mengi  ambayo   mtu  hujikuta  amefikishwa  mahakamani. Wakati  mwingine  kufikishwa  mahakamani  ni  jambo  ambalo  laweza  kukutokea  bila  hata  kutarajia wala  kufikiri  kama  kuna  siku  utafika huko. 

Hatimiliki ni  nyaraka  inayoweza  kukusaidia  usiingie  korokoroni .
Mara  nyingi  dhamana  huwa inahitaji   mali  isiyohamishimika  ambayo  ni  ardhi.  Na  kitu  pekee  kinachothibitisha   kumiliki  mali  isiyohamishika   ni  hati. Kupitia  hati  unaweza  kujidhamini  mwenyewe  au  kumdhamini ndugu, jamaa na rafiki.

(  d  )  Kupata  mkopo  ni  faida  nyingine  ambayo  sote  twaijua. Zipo  taasisi  za  fedha  zinazokubali  hata  nyaraka  nyingine  ambazo  sio  hati  lakini  kwa  mwenye  hati  ni  uhakika  zaidi. Hizi  zi  faida chache kati  ya  nyingi zilizopo.

Makala  yajayo  yataeleza  namna  ya kupata  hati.
                                       NYUMBA  KUBWA  INAUZWA.



1.Ina vyumba 4, kimoja master.
2. Ni  nyumba  kubwa  nzuri.
3. Iko  ndani  ya  fensi Sqm  1200
4. Bafu  2
5. Umeme umo na maji,jiko na public toilet.
6. Ipo mtoni  kijichi.
7. Bei milioni  97  inapungua kidogo.
0784482959.


2 comments:

  • Barkat says:
    12 June 2019 at 02:22

    ina hat

  • Unknown says:
    7 October 2019 at 10:56

    Mabaraza ya kata yanamalaka kutoa maamuzi/hukumu kwa maeneo yenye hati miliki?

Post a Comment