Thursday 14 January 2016

MAMBO YA KUZINGATIA KWA WANAONUNUA ARDHI YA VIJIJI KWA UWEKEZAJI.

Image result for ARDHI KIJIJI

NA  BASHIR  YAKUB - 

Masuala  ya  msingi  yanayohusu  ardhi  za  vijiji  yanasimamiwa  na  sheria  namba 5  ya  ardhi  za  vijiji. Sheria  hii  ilitungwa  mwaka  1999  na  kuanza  kutumika  rasmi   Mei  2001.  Upo  mwamko  mkubwa  wa wananchi  hasa wa  maeneo  ya  mijini na  wale  walio  nje  ya  nchi  wa  kununua  maeneo  ya  vijiji  kwa  ajili  ya  shughuli  mbalimbali  za   uwekezaji  na  uchumi  kwa  ujumla.

Hata  hivyo    wengi  wao  wamekumbwa  sana  na  migogoro  huko  wanakonunua.  Sababu  za  migogoro  hii  ni  nyingi. Lakini  mojawapo  ni  kutokuzingatia  mambo  ya  msingi  na  ya  kisheria  wakati   wa  kupata  ardhi hizo.  

Nani  asiyejua sasa  kuwa  migogoro  baina  ya  wawekezaji  na  wanavijiji  ni  janga,hakika  hakuna.

Ni aghalabu  kufungulia  runinga  au  redio usisikie  mgogoro  wa ardhi  baina  ya  wanakijiji  na  mwekezaji.  Ni  sababu  hii inayopelekea  makala  haya  na  makala  nyingine  zilizopita  kueleza  japo  baadhi  ya  mambo  ya msingi  na ya  kuzingatia unapoelekea  kumiliki  ardhi  ya kijiji.

1.NANI  ANA  HAKI  YA  KUTOA  UMILIKI  WA  ARDHI  YA  KIJIJI.

Kifungu  cha  25  cha  sheria  ya  ardhi  ya  vijiji  kinasema  kuwa  Halmashauri  ya  kijiji  ndicho chombo chenye  mamlaka  ya  kutoa  umiliki  wa  ardhi  ya  kijiji. Usikubali  kuuziwa  ardhi  ya  kijiji na  chombo  kingine  chochote   mbali  na  chombo  hiki. 

Wengi  wamenunua  ardhi   kwa  kuuziwa  na  mtendaji kata,  sijui  mwenyekiti,  sijui balozi  wa  nyumba  kumi  na hata wengine  wameuziwa  na  watu  binafsi.  Ardhi  ya  kjiji  hutolewa  na  halmashauri  ya  kijiji na  hii  ni  kwa  mujibu sheria.
Utakapokuwa  umeuziwa  na  chombo  tofauti , tafsiri  yake  ni  kuwa  hujanunua  umegawa  hela.  

Maana  yake ni  kuwa  muda  wowote  wanakijiji  na  serikali  yao  wataomba  kurudushiwa  ardhi  yao. Umakini  unahitajika  sana  eneo  hili  kwakuwa  wengi  wameuziwa  na  mamlaka/watu  ambao  hawana  uwezo  wa  kuuza  ardhi  ya  kijiji  kisheria.  Migogoro  mingi ina  sura ya   mtu  kumiliki  ardhi  katika  kijiji  huku kijiji  kikidai  kutomtabua. Sababu ni hii kuuziwa  na watu  wasio  na  mamlaka.

2.  NI  NYARAKA  IPI  UNAYOIPATA  UNAPONUNUA  ARDHI  YA  KIJIJI.

Kipo  kitu kinaitwa  cheti  cha hakimiliki  ya  kimila( customary  right  of  occupancy). Hiki  ndicho  kitu  kinachotakiwa   kutolewa  unapokuwa   umenunua  ardhi  ya  kijiji.  Cheti  hiki  ndicho  nilichosema  hapo  juu  kuwa  kinatolewa   na  halmashauri  ya  kijiji. 

Usikubali  kuambiwa  umenunua  ardhi  ya  kijiji  bila  kupatiwa  cheti  hiki. Hii  ni  kwakuwa  uhalali  wa  umiliki  wako  unategemea hiki  cheti.

3.  CHETI  CHA  HAKIMILIKI  KINAKUWAJE ?.

( a ) Kinakuwa  katika  mfumo  wa fomu  maalum.  Ni  fomu  ambayo  ina  kichwa  cha  serikali  ya  kijiji  husika.

( b ) Kitakuwa  na  sahihi   ya  mwenyekiti  wa  kijiji  na  katibu  wa  halmashauri  ya   kijiji. Ni  muhimu  ukayazingatia  haya  ili  unapopewa  cheti  hiki  uhakikishe  kiko  hivyo  ili  kuepuka  ulaghai.

( c ) Lazima  kiwe  na  sehemu  ya sahihi  au  dole  gumba  la mwombaji/anayemilikishwa/mnunuzi.

( d ) Lazima  kitiwe  sahihi  na  kusajiliwa  na  afisa  ardhi  wa  wilaya.  Wilaya  inayohusika  ni  ile  ambayo  kijiji  husika  kimo.

Kwahiyo  ni  muhimu  kwako  kuhakikisha  hakimiliki ya  kimila  unayopewa  baada  ya  kununua  ardhi  ya  kijiji  inakuwa  katika  muonekano  wenye  maudhui  haya .

4. MUDA WA  KUOMBA  KUMILIKI  ARDHI  YA  KIJIJI.

Maombi  ya  nia  ya  kumiliki  ardhi  ya  kijiji yatawasilishwa   mbele  ya  Halmashauri  ya  kijiji.  Usipeleke maombi  haya  kwa  mtu  binafsi,  au  kwa  mtendaji wa kijiji/kata pekee,  au  mwenyekiti  pekee,  au    balozi  pekee. Maombi  yanawasilishwa  kwa  Halmashauri  nzima.

Sheria  namba  5 ya  ardhi  ya  vijiji  inasema  kuwa  utatakiwa  kujibiwa  maombi  yako  ya  kumiliki  ardhi  ndani  ya  siku 90 tokea  siku  ulipowasilisha  maombi  hayo. Halmashauri  ya  kijiji  ndicho  chombo  chenye  wajibu  wa  kuhakikisha  kinatoa  majibu  ya  kukubaliwa  au  kukataliwa  ndani  ya  muda  huo  wa  siku 90.

5.  NASAHA.

Ni  ushauri  mujarabu  kuwa  ni  muhimu  sana  kupata  mwongozo  wa  wanasheria  kabla  ya  kuingia  katika  muamala  huu  wa  manunuzi. Hii  ni  kwakuwa zipo  taratibu  nyingi  hata  ambazo  hazijaelezwa  humu  zinazohitaji  ufanunuzi  wa  kisheria wakati  na  kabla  ya  kununua ardhi.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA     SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.      0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment