Monday 7 December 2015

TOFAUTI YA SHIRIKA ( FIRM ) NA KAMPUNI KIBIASHARA.


Image result for FIRM
NA  BASHIR  YAKUB -

Biashara  hufanywa  kwa  mitindo  ya  aina nyingi  kutegemea  na  mahitaji  ya  wahusika. Unaweza  kufanya biashara  kwa  mtindo  wa  kampuni,  unaweza  kufanya  biashara  kwa  mtindo  wa  mtu  binafsi, lakini  pia  unaweza  kufanya  biashara  kwa  mtindo  wa  shirika ( firm)/ubia.  Mitindo  hii  yote  inatofautiana kiutendaji,  kifaida na kiuwajibikaji (liability).  

Kuhusu  kampuni  tumeeleza  mara  nyingi  faida  zake, aina  zake,  masuala  ya  hisa, mpaka  namna  ya  kuunda  kampuni, ada  zinazostahili  na  kila  kitu.  Pia  yapo  makala  yaliyoeleza  biashara  binafsi  hasara  na  faida  zake.  Leo   katika  makala  haya  tutapata  kuona biashara  ya  shirika (firm)/ubia . Tukumbuke  kuwa  haya  yote  ni  mazao  ya  sheria na  hivyo  huwa  tunayatizama  kwa  mtazamo  wa  sheria.
Sheria  imeeleza  kwa  mapana  kabisa  aina  zote  hizi  za  biashara  ili  kuepusha  migongano  baina  ya  wahusika.  Sura  ya  345  ya  sheria  ya  mikataba  iliyofanyiwa  marekebisho  mwaka  2002  ndiyo  inayozungumzia  shirika/ubia kama  tutakavyoona.

1.SHIRIKA/UBIA  NI NINI.

Shirika/Ubia  ni  uhusiano  uliopo  baina  ya  watu  wanaofanya  biashara   ya  faida  kwa  pamoja . Kwa hiyo  ili  ubia  uwepo  ni  lazima  watu  wawili  au  zaidi  waungane  na  waamue  kufanya  biashara  kwa  pamoja. Hii  ni  kwa  mujibu  kifungu  cha  190  cha  sheria  ya  mikataba. Kuungana  huku  ili  kufanya  biashara  sio  kuunda  kampuni.  

Ni  kuungana  ambako  hakuhusishi  kampuni  lakini  kunakotambulika  kisheria. Muungano   wa  kufanya  biashara kwa  pamoja  ndio  ubia.
Watu  walioingia  ubia  kwa  umoja  wao  wanaitwa  shirika ( firm). Kwa hiyo shirika  na  ubia humaanisha  kitu  kimoja na  ndio  maana katika  makala  maneno  haya  yanatumika  pamoja.  Na  jina  wanalotumia  wabia linaitwa  jina  la  shirika ( firm  name).  

Mifano  ni  mingi  ila  mojawapo  ni  yale  mashirika  ya  wanasheria  yaitwayo  law firm, au  ya  wahasibu  yaitwayo  accountant  firm na  mengine  mengi.  Lakini  hata  katika  biashara  za  kawaida za  uuzaji  wa  bidhaa  na  mengineyo nako  ubia  hufanyika.

2. TOFAUTI  YA  SHIRIKA UBIA (PARTNERSHIP FIRM )  NA  KAMPUNI (COMPANY).

Tofauti  ni  nyingi   ila  hizi  ni  baadhi :
( a ) Katika  shirika (firm)  ikiwa  kuna  mkopo   umekopwa  na  shirika  kwa  ajili  ya  biashara  fulani  basi  wanashirika  wote wanawajibika  kwa  deni  hilo  kila  mtu  mmoja  mmoja  kwa  nafasi  yake.  Na  ikiwa   shirika litashindwa  kulipa  basi  mali  binafsi  za  kila  mmoja  ya  washirika  zinaweza  kukamatwa  kulipia  deni  hilo. Hii  haipo  kwenye  kampuni. KatIka  kampuni  haiwezi  kutumika  mali  ya  mtu  binafsi  mwanahisa  kufidia  deni  ambalo  kampuni  imeshindwa  kulipa hasa  kama  mali  hiyo  haikutumika  kama  rehani. Ni  mali  ya  kampuni  tu  itakayotumika.

( b ) Shirika  linaposababisha  hasara  kwa  mtu mwingine  ambaye  sio  mwanashirika  kwa  maana  ya  mtu  wa  tatu  basi  wanashirika(partners) wanawajibika  kufidia  hasara  hiyo   kwa  michango  yao.  Hii  ni  tofauti  na  kwenye  kampuni  ambapo  wenye  kampuni   hawawajibiki  kufidia  hasara  iliyosababishwa  na  kampuni  kwa  mtu  ambaye  si mhusika  katika  kampuni  hiyo. Kampuni  kama  kampuni  ndiyo  inayowajibika  kufidia  hasara  hiyo  na  si  wenye  kampuni. Mali  za  kampuni  ndizo  zitakazotumika   na  kama  hazipo  hilo  ni  jambo  jingine. Muhimu   ni  kuwa  mali  za  wenye  kampuni  hazitaguswa.

( c ) Katika ubia  hakuna  mtu  anaweza  kualikwa  kuwa  mbia  katika  shirika  bila  ridhaa  ya  wabia  wote.  Kila  mbia  ni  lazima  aridhie  ujio  wa  mbia  mpya. Katika  kampuni   hasa  makampuni  ya  umma (public  company)  haihitajiki  ridhaa  ya  wana hisa  wote  ili  mtu mpya akubaliwe  kuwa  mwanahisa.  

3.   KANUNI  KUU  ZINAZOONGOZA  SHIRIKA (FIRM).

Kanuni  kuu  inayoongoza  shirika  ni  makubaliano ya  kimkataba. Kile  mnachokubaliana  kimkataba ndicho  kinachotakiwa  kutekelezwa. Kama  hakuna  makubaliano  yoyote  basi  masharti  yaliyo  katika  kifungu  cha  194  cha  sheria  ya  mikataba ndiyo  yatakayotumika  kama  makubaliano  yenu. Masharti  hayo  ni  pamoja  na  kila  mbia  kuwa  sehemu  ya  uongozi  wa  shirika, maamuzi  kufanywa kwa  kura  za  walio  wengi, haki  ya  kukagua  vitabu  vya  shughuli za  shirika, kugawana  faida  kwa  usawa, n.k.

4.   SHIRIKA (FIRM) HUSAJILIWA  WAPI.

Mashirika (firm)  husajiliwa  kwa  msajili  wa  makampuni  na  biashara  BRELA. Vipo  vyeti  maalum  ambavyo  hutolewa  kwa  ajili  ya  usajili baada ya  ada  ya  usajili  hulipwa.  Katika  makala nyingine  tutaona  kipi  bora  kibiashara  kati  ya shirika (firm) na  kampuni ( company).

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.






5 comments:

  • Unknown says:
    21 January 2016 at 05:38

    Nimefarijika Kupata Elimu Katika Mada Zako Pamoja Na Uwasilishaji Wako Unazingatia Mambo Mengi Nikushukuru Na Kukupongeza "hongera Sana" Napenda Kujua Zaidi Ili Niweze Kuishi Kwa Utaratibu Na Jamii Inayo Nizunguka Pia Ningependa Kufaham Mengi Kuhusu Wadhifa Pamoja Na Taaluma Yako Inawezaje Kutukomboa Zaidi Tushiriki Wote Katika Kuleta Mabadiliko Na Tusikate Tamaa. Aksante ACDO GEITA-MBOGWE, ZAWAD MGHERO

  • Unknown says:
    16 February 2016 at 12:55

    Ahsante ndugu kwa elimu hii hakika umeongeza vitu vingi akilini mwetu wafuasi wa blog hii

  • Unknown says:
    29 April 2016 at 01:38

    Nashukuru nimeyafahamu mengi Sana kuhusu sheria ya Ardhi pamoja Na nyinginezo. Mungu akubarikie maisha marefu uendelee kutujuza tusiyoyajua.

  • Unknown says:
    22 May 2020 at 21:53

    Ahsante Sana kwa makala hii imenifundisha, lengo kuu nilitaka kujua kanuni za mikataba ya mashirika ili Mimi na wenzangu tuanzishe biashara ya kushirikiana

  • MRINDOCO says:
    22 August 2021 at 01:45

    mashallah !! special thanks to you !!
    🙏🙏🙏

Post a Comment