Monday 21 September 2015

KAMA UMEONEWA NA MWAJIRI WAKO HARAKA CHUKUA HATUA HIZI.

Image result for MTUMISHI  WA  UMMA


NA  BASHIR  YAKUB - 

Wapo  wafanyakazi wengi  ambao  wanasumbuliwa na  migogoro  ya kikazi  maofisini  kwao  lakini  hawajui  nini  wafanye. Wengine  hufanyiwa  mambo  ya  ajabu  huko  makazini  yumkini  wakashindwa kuchukua  hatua  yoyote kutokana  na  kutojua  waanzie wapi  na waende wapi.  Na hizo  ni  ajira  rasmi tusiongelee  hizo  zisizo  rasmi. Tusiongelee  vibarua  huko  viwandani  na  kwenye  maeneo  mbalimbali  ya  ujenzi hasa  yale  yenye  miradi  mikubwa  kama  ya  barabara,  madaraja  n.k.  Tusiongelee  wafanyakazi  wa  ndani  na  kazi  nyingine  zinazofanana  na  hizo.  Hawa hupata  shida  sana  na  mbaya zaidi  hukosa  msaada hata  wa  kujua  ni  hatua  gani  wachukue. Kimsingi  unaposumbuliwa  na  mgogoro  wowote  wa  kazi  zipo  hatua  za  kuchukua  ambazo  zimeainishwa   na sheria. Ni  hatua  nyepesi  tu  labda  mtu  usipende  kuzichukua.

1.KUJIUNGA  NA  VYAMA  VYA   WAFANYAKAZI.

Huwa  kuna  umuhimu  mkubwa  wa  kujiunga  na  vyama  vya  wafanyakazi.  Hii  ni  kwasababu  unapokuwa  mwanachama  pindi  unapotokea  mgogoro  kitu  cha  kwanza  unatakiwa  kutoa  taarifa  kwenye chama  chako  ambapo  uongozi  wa  chama chako   utawasiliana  na waajiri  wako  kwa  ajili  ya  kukutetea. Pia  ikiwa  mazungumzo  kati ya chama  chako  na  waajiri  yatashindikana  basi  chama  hubeba  jukumu  la  kwenda  mahakamani  moja  kwa  moja  kukutafutia  haki  yako. Huu  ndio  umuhimu  mkubwa wa  kujiunga  na  vyama  hivi.  Unapokuwa  unafanya  kazi  hebu  jaribu  kuuliza  kuhusu  vyama  hivyo  utaelezwa,  utajiunga  na  kuwa  mwanachama  kwa  ajili  ya  maslahi  yako kesho.

2.  PELEKA  MGOGORO  WAKO TUME  YA  USULUHISHI.

Tume  ya  usuluhishi  wa  migogoro  ya  kazi  huitwa  MEDIATION. Kisheria  tume  hii  inaainishwa  na sehemu  ya  II ya  sheria  namba  7  ya  taasisi  za  masuala  ya  kazi  ya  2004. Unapokuwa  na  mgogoro kwa  mara  ya  kwanza  ni  vema  ukatafuta  tume  hii  ilipo  na kupeleka  mgogoro  wako . Ukifika  hapo  utapewa  fomu  maalum  ya  kujaza  na  baada  ya  hapo  mwajiri  wako  ataitwa   kwa  ajili  ya  usuluhishi. Kwa  walio  Dar  es  salaam  tume  hii  ipo  jengo  la  msalaba  mwekundu  eneo  la  akiba  makutano  ya  bibi titi  na  morogoro.  

Mgogoro  wowote  unakubalika  unaweza  kuwa  mgogoro  wa  kimaslahi kwa  mfano  kutaka  kuongezewa  mshahara,  kutoridhishwa  na  mazingira  ya  kazi,  kufanya  kazi  kinyume  na  mkataba n.k. Pia unaweza  kuwa  mgogoro  wa  malalamiko  kwa  mfano  kufukuzwa  kazi  bila  kufuata  taratibu,  kupunjwa  mafao , kuvunjiwa mkataba kinyume  na  sheria n.k.
Hakikisha unapeleka  mgogoro  wako  ndani  ya  siku  30  tangu  kutokea  kwa  mgogoro  huo. Hata  hivyo  kama  zimepita  siku  30  na  unazo sababu  za  msingi za kwanini  hukupeleka  mgogoro  ndani  ya  muda huo  basi  utajaza fomu  ya  kuomba   kuongezewa muda  huku  ukitoa  sababu  za  kwanini  ulichelewa.

3.  MGOGORO  KWENDA  TUME  YA  UAMUZI.

Hapo  juu  tumeona  kuwa  mwajiri wako  ataitwa kwa  ajili usuluhishi ili  kupata  muafaka  wa  mgogoro. Hata  hivyo usuluhishi  unaweza  kushindikana   kwa  kutoelewana  katika  nukta  fulani fulani. Ikiwa  usuluhishi  utashindikana  basi  mgogoro  utaenda  tume  ya  uamuzi. Katika  tume  hii  kila  upande  utatoa  maelezo  yake  na  ushahidi. Upande  wa  mwajiri  utatoa  maelezo  na  upande  wa  muajiriwa  nao  utatoa  maelezo.  Tume  hii  itasikiliza  na  kutoa  maamuzi.  Maamuzi  ya  tume  hii  yana  nguvu  za  kisheria  kama  maamuzi  ya mahakama   na  hivyo   yakitolewa   ni  lazima  yafuatwe.

Zingatia  kuwa  katika  hatua  zote  hizo  juu  yaani  wakati  wa usuluhishi  na  wakati  wa  uamuzi  unaweza  kumtafuta  mtu  wa  kukuwakilisha  ikiwa  ni  mwanasheria, chama  cha  wafanyakazi  au mtu  unayeamini  anaweza  kukusaidia   katika  masuala  ya  kazi. Hili  linaruhusiwa.

4.  MGOGORO  KWENDA MAHAKAMA  KUU  YA  KAZI .

Ikiwa  hukuridhishwa  na  maamuzi  ya  tume  ya  uamuzi hapo  juu basi unaruhusiwa   ndani  ya  siku  30 tangu siku  ya  kutolewa  maamuzi  hayo   kupeleka  shauri  hilo  katika  mahakama kuu  ya  Tanzania.  Utaiomba  mahakama  kuu  irejee(revise)  vipengele  kadhaa  unavyolalamikia  unavyohisi  tume  ya  uamuzi  haikutenda  haki.  Ikiwa  pia  haukuridhika  na  maamuzi  ya  mahakama  kuu  basi  utapeleka  rufaa  yako  mahakama  ya  rufaa   ikiwa  suala  lako  lina  hadhi  ya  kwenda  huko.

Kubwa  na  muhimu  kuliko  yote kwenye  makala haya  ni  kujua  kuwa mgogoro  unapotokea, haraka  ndani  ya  siku  30  upelekwe  baraza la  usuluhishi. Kwa  walio  mikoani  au  wilayani kujua ilipo  tume  hii nenda  makao  makuu  ya  wilaya  au  mkoa  ulizia  hapo watakuonesha ilipo  tume. Hapo  utapata  muongozo  wa  kila  kitu  nilichosema  humu  na  ni  bure.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                   WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA         BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.




0 comments:

Post a Comment