Tuesday 2 June 2015

ZIJUE ADA UNAZOTAKIWA KULIPA UNAPOTAFUTA/ KUBADILI HATI YA NYUMBA/KIWANJA.


Image result for wizara ya ardhi

NA  BASHIR  YAKUB -

Watu  wengi  wanaonunua  ardhi  wamekuwa  wakipata  usumbufu  mkubwa katika   kubadili  majina  yaani kutoka  mmiliki  wa  mwanzo  kwenda  kwa  mmilki mpya  aliyenunua. Upo  usumbufu ambao  husababishwa   kwa  makusudi na  maafisa  wanaohusika   lakini  pia  upo  usumbufu  ambao  husababishwa   na  watu  wenyewe  wanaotaka  kubadili  majina.  Wengi  huanza  muamala  huu  bila  kuwa  na  taarifa  kamili  za  nini kinahitajika kwa  maana  ya  nyaraka  ikiwemo  ada au  malipo  ya  kisheria jambo  ambalo  huwapotezea  muda  mwingi. Kwa wanaofanya kazi  hizi  kama  mimi  watajua  ni usumbufu  wa aina  gani  mtu  huupata anapoanza mchakato  huu bila  taarifa.  Unaposoma  makala  haya  ni  vema  basi  ukajua  inatakiwa  ujiandae  na  nini  na  hasa  ada ili  unapoanza  mchakato  huu  usijikute  unaishia  njiani.

1.UMUHIMU  WA KUBADILI  JINA  HARAKA  BAADA  YA MANUNUZI.

Nimewahi kuandika kuwa sheria iko wazi kuwa ambaye jina lake linaonekana kwenye hati ndiye mmiliki.
Kwa  kauli  hii   mnunuzi  anatakiwa  kufanya  jitihada  za  haraka  na za  makusudi  kubadili  jina  mara tu baada  ya  kununua  kiwanja  au  nyumba. Sikatai  kuwa  kunakuwa  na  mkataba wa  mauziano  lakini  lazima  ieleweke  kuwa  mbele  ya  macho  ya  sheria   jina  lililo  kwenye  hati  lina  uzito  kuliko  mkataba  wa  mauziano. Usiridhike  kukaa  na  mkataba  wa  mauziano  ikiwa  hujabadili  jina. Hii  ni  kwa  ajili  ya  ulinzi  wako  na  wa  ardhi  yako.  

Utakapotokea  mgogoro   wa  umiliki  ikiwa  hujabadili  jina waweza  kuwa  katika  hatari  kubwa  ya  kupoteza  hasa  kama  mgogoro  huo  umeanzishwa na aliyekuuzia. Huu  ndio  ukweli  na  lazima  tuonyane  ili    tuwe  salama na  mali  zetu. Lakini pia  hata  ukitokea  mgogoro  mwingine  wowote  wa  umiliki  kuna  mambo  ndan ya  sheria  yataufanya  kuwa   mgumu kutokana  na sababu  tu  kuwa ulikuwa  hujabadili   jina.  Hapo  sijaongelea  faida  nyingine  za kubadili  jina  kama  kukopa  n.k. Nishauri  tu  kwa  ufupi  kuwa  unapojiandaa  kununua  nyumba  au kiwanja  jiandae  pia na  kubadili  jina  moja  kwa  moja.  Hakikisha  haya  mawili  yanakwenda   pamoja.

2. ADA  ZA KUBADILI  HATI ZA NYUMBA/VIWANJA  HIZI  HAPA.

Nimesema  hapo  juu  kuwa  usipojiandaa  na  ada  vyema  mara   nyingi  utajikuta  unaishia  njiani  kwa  kushindwa  kukamilisha  mchakato  huu.  Lakini  utaandaaje  ada  bila  kujua  kinahitajika  kiasi  gani . Hili  ndilo  lengo  la  makala  haya. Malipo ya  ada  tunaweza kuyagawa  mara  mbili. 

Kwanza  kuna  ada inayolipwa  manispaa. Hii  hulipwa  katika  manispaa  ile  ambayo kiwanja  au  nyumba  ilipo. Kama  temeke  basi  ada  italipwa  manispaa  ya  temeke  halikadhalika  maeneo mengine  hivyohivyo. Na  hapa  ndipo  unapoanzia katika  ulipaji  wa  ada.  Ada  inayolipwa katika  manispaa  huwa ni  asilimia moja  ya  mkataba  wa  kununulia  au  ya  taarifa  ya  tathmini (valuation report). Unapokwenda  kulipa  ada  manispaa  ni  lazima  uambatane  na  mkataba  wako  ulionunulia  kiwanja/nyumba  pamoja  na  valuation  report  kwakuwa  hivi  ndivyo  wanavyotumia kama  vipimo  vya  ada. Ikiwa  mkataba  wa  kununulia  una  bei  kubwa  kuliko valuation  report  basi  wanachukua  asilimia  moja  ya  mkataba  huo na  ndio  itakuwa  ada. Lakini  ikiwa  pia  valuation  report  ina bei  kubwa kuliko  mkataba  basi  wanachukua  asilimia moja  ya  valuation  report. Kwa  ujumla  wao  huchukua  asilimia moja  ya  chenye  bei  kubwa  kati  ya  valuation  report  na  mkataba  wa  kununulia  na  huifanya  hiyo  ndio  ada.

Pili  baada  ya  kulipa  manispaa  faili  lako hupelekwa  mamlaka  ya  mapato  Tanzania ( TRA) kwa  ajili  ya  kodi. Hawa  wao  hutoza  asilimia  kumi  ya  taarifa  ya  tathmini( valuation  report). Kama  valuation  inasema  eneo  lako  lina  thamani  ya  milioni  kumi bila  shaka asilimia  kumi  yake  ni  milioni moja. Hiyo  ndio itakuwa  kodi. Angalizo  hapa  ni kuwa  hizi  valuation  report  hutakiwa zile mpya. Kwa  mfano  mtu anayo  valuation  yake   aliyofanyiwa  mwaka  2000  na  sasa anataka  kupata au  kubadili  hati  leo  2015. Hii  ya  mwaka  2000  haiwezi kutumika  kutathmini  kodi itahitajika  mpya  ya mwaka 2015.  Hii  ni  kwasababu  thamani  ya  ardhi  ya  mwaka  2000 si  sawa  na  ya  sasa  mwaka 2015. Hizi  ndizo  ada  unazotakiwa  kujiandaa  nazo.  


2.   PIA  ANDAA  NYARAKA  HIZI.

( a ) NYARAKA  ZA  UHAMISHO

Nayaraka  za  uhamisho  zinajumuisha  fomu  namba 29  ijulikanayo  kama  fomu  ya  kusudio  la  uhamisho( notification  of disposition) ambayo  hueleza  nia  na  lengo  la  muuzaji  kutaka  kubadili  jina  au  kuondoa  jina  lake  katika  hati.  Hii utaandaa  nakala  tatu . Pili  ni fomu  namba  30  ambayo  hujulikana  kama  fomu  ya  idhibati  ya  uhamisho ( application  for  approval  of  disposition).  Katika  fomu  hii  muuzaji  pia  atakuwa  anatoa  idhini  kwa  mamlaka  za  ardhi  kuidhinisha  hiari  yake   ya kuachia  umiliki  kutoka kwake   kwenda  kwa  mtu  mwingine ambaye  ndiye  mnunuzi.   

Mwisho  ni  fomu  namba  35  ijulikanayo kama fomu  rasmi  ya  kuhamisha  umiliki ( transfer of a  right  of  occupancy)  ambayo  ndiyo  rasmi  sasa  huhamisha  umiliki  kutoka  kwa  muuzaji  kwenda   kwa mnunuzi. Hii  ndiyo  humpa  mnunuzi  umiliki  rasmi . Pia  mkataba  wa  mauziano  ni  nyaraka  ambayo  itaambatanishwa  hapa.
Kwa  kiwanja  au  eneo  ambalo  halijaendelezwa ( halijajengwa)   huandaliwa  kitu  kiitwacho  commitment  bond  kikiwa  kama  ziada  ya  nilivyotaja  hapo.  Fomu  zote  hizo  pamoja  commitment  bond  hupatikana  katika  ofisi  za  wanasheria  na  huandaliwa  na  wanasheria.

( b ) URAIA

Sheria  iko  wazi  kuwa wanaotakiwa  kumiliki ardhi  ni  raia  wa  nchi  hii tu. Hivyo  unapotakiwa  kupata  hati  ya  umiliki  lazima  pia  uthibitishe  Utanzania  wako. Hapa   utatakiwa kuandaa  nakala(copy)   ya   cheti  cha  kuzaliwa ambayo  imethibitishwa( certified)  na  wakili  au  nakala  ya  pasipoti  ambayo  imethibitishwa  na  wakili  au  kama  huna  hivyo  vyote  basi  yakupasa  kuandaa  kiapo( affidavit).

Mwisho  niseme  kuwa  ikiwa  utajiandaa vyema  na  haya  utapata  hati  kwa  urahisi   au  kama unabadili  jina  utabadili  kwa  urahisi  pia. Jiandae epuka  usumbufu.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com
                                              
                                           TANGAZO   MUHIMU                                                

VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.

WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE NA                    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.

UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA   WANASHERIA     WETU.

UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA                 BURE.

IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA              MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.




0 comments:

Post a Comment