Thursday 25 June 2015

MIRATHI ZA WATOTO WADOGO NA WASIO NA AKILI TIMAMU HUSIMAMIWA NA NANI KISHERIA ?

Image result for watoto

NA  BASHIR  YAKUB - 

Suala  la  mirathi  popote  linapotokea   hutokea  iwapo  kuna  mtu  amekufa  na   ameacha  mali  . Mtu  akishakufa  akaacha  mali  hata  kama  hakuna  ndugu wa kurithi  suala  la  mirathi  lazima  liibuke.  Huibuka kwakuwa  lazima  zile  mali  ziende  pahali  iwe  kwa  mtu  au  kwa  mamlaka. Hata  hivyo  suala  la  mirathi  huibua  hisia  zaidi  hasa  panapokwa  hamna  wosia.  Marehemu  asipoacha wosia  lakini  akaacha   mali  mambo  huwa  sio  mepesi  sana labda  iwe vinginevyo.  Ifahamike  kuwa mirathi  huhusisha   mambo  mengi. Lakini  pia huhusisha  sheria  nyingi.  Sheria  za kiislam huhusika, sheria  za  kimila  huhusika   na  pia  sheria  za  nchi  ambayo  ni  sura  ya  352.

1.USIMAMIZI  WA  MIRATHI  KAMA  KUNA  WOSIA.

Kama  marehemu  ameacha  wosia    basi  ni  vema  kuangalia  wosia  huo  umemtaja  nani awe  msimazi wa  mirathi. Hili  ni muhimu  watu  walijue  hata  wale  walioandika  wosia  tayari au  wanaotarajia  kuandika  wosia.  Wengi  wamekuwa  wakiandika  wosia  na  kugawa  mali  lakini  wakisahau  kuteua  na  kumtaja  msimamizi  wa  mirathi  wakiamini  kuwa  kila  mtu  atakapochukua  chake   mambo  yataishia  hapo. Laa  hasha  mambo  si  mepesi  kiasi  hicho.  Kwa  hiyo  yafaa  kuangalia  nani  ametajwa  kama  msimamizi  wa  mirathi  katika  wosia    na  huyu  ndiye  atakuwa  msimamizi  wa  mirathi. Ikiwa  wosia  upo  lakini  haukumtaja  msimamizi  wa  mirathi  basi  taratibu  za  kimahakama  nitakazoeleza  hapa  chini  zitafuata.

2.  KUMTHIBITISHA  MSIMAMIZI  WA  MIRATHI  MAHAKAMANI.

Ikiwa  wosia   umemtaja  msimamizi  wa mirathi  basi  hilo  tu  halitoshi. Sheria  inataka  msimamizi  wa  mirathi  athibitishwe  pia na  mahakama. Hii  ni  kwasababu   mahakama  hutoa  hati  maalum   kwa  aliyethibitishwa kuwa  msimamizi  wa  mirathi  ambayo  hutum ika  sehemu  zote  za  kisheria  kwa  mfano  kuchukua  hela  za  marehemu  benki, kuchukua  hisa za  marehemu, kuuza  na  kununua  mali  za  marehemu,kubadilisha  vitu  kama  hati na kila  kitu  ambacho  huhusisha  taratibu  maalum  za  kisheria. Kwakweli  isingewezekana  kutumia wosia  kwa kuuonesha  kila ofisi  unayoingia  katika kufanya  michakato  hii yote.  Na  hapa ndio  mahitaji  ya  kuthibitishwa  na  mahakama  na  kupata  hati maalum ambayo  ni  kama  utambulisho  yalipotokea.

Pili  kama  wosia  upo  lakini  haukumtaja msimamizi  wa  mirathi  napo   ndugu  watakaa kikao  watamteua  msimamizi  wa  mirathi  na  atakwenda  kuthibitishwa  na  mahakama  ili  kupata  hati  hiyo.  Utaratibu  ni  huu  huu  hata  panapokuwa  hakuna  wosia  wowote  ulioachwa   na  marehemu. Ndugu  watakaa  kikao  watamteua  msimamizi  wa  mirathi  na  atapelekwa  mahakamani  kuthibitishwa  na  kupata  hati  hiyo  maalum. Kwa  ujumla ninachotaka  kueleza  ni  kuwa  hatua  ya  kwenda  mahakamani   kumthibitisha  msimamizi  wa  mirathi  ni  katika  mazingira  yote,  yaani wosia  uwepo  na  umemtaja  msimamizi  mirathi, wosia  uwepo  lakini  haukumtaja  msimamizi  wa  mirathi   na  wosia  usiwepo  kabisa.

3.  NANI  HUSIMAMIA  MALI   ZA  MTOTO/WATOTO  WADOGO.

Marehemu  anapoacha  watoto/mtoto mdogo akiwa ndiye  mrithi  pekee  nani  ana  haki  ya  kusimamia  mali  zake ndicho  ninachomaanisha.  Na  hapa  ni  katika  mazingira  yote yaani  kuna  wosia  au  hakuna.  Kwanza  tumjue mtoto ni  nani.  Mtoto  mdogo kwa  maana hii  ni yule  ambaye  hajafikisha  umri  wa  miaka  18  na  hivyo  kutoruhusiwa  kuwa  msimamizi  wa  mirathi. Aidha  wengine  huacha  watoto  wa  mwaka  mmoja,  miezi  na  hata  siku.  Kifungu  cha  36( 1 )  cha  Sheria  ya  Mirathi  kinasema  kuwa  iwapo  kuna  mtoto/watoto  wanaostahili  kuwa  wasimamizi  wa  mirathi  lakini  hawawezi  kutokana  na  umri  wao  basi  mamlaka  ya  usimamizi  wa  mirathi  atapewa  mlezi  wao  au  mtu  mwingine  ambaye  mahakama  itamuona  anafaa.  Wakati  mwingine  mlezi  anaweza  kuonekana  si  mwadilifu  na  hivyo   kuziweka  mali  za  marehemu  katika hatari  ya  kupokwa. Ikiwa  wasiwasi  huo  utajitokeza  basi  mahakama   itamteua  mtu  mwingine  yeyote kusimamia  mirathi  mpaka  watoto/mtoto  huyo  akue ili  asimamie  mwenyewe.

4. NANI  HUSIMAMIA  MALI  ZA  ASIYE  NA  AKILI  TIMAMU.

Natumia  neno  asiye  na  akili  timamu  japo  ni  refu kwa  kuhofia  kutumia  neno  chizi au  kichaa  kutokana  na  ukali  wake. Hata  hivyo  namaanisha  hivyo.  Kifungu  cha 37  cha  Sheria  ya Mirathi  kinasema  kuwa  iwapo  mtu  asiye  na  akili  timamu  alitakiwa  kusimamia  mirathi  lakini  akashindwa    kutokana  na  hali  yake   hiyo basi  mtu  anayemtunza   au  mwingine  atakayeonekana  kufaa  zaidi atateuliwa  kusimamia  mirathi  hiyo  mpaka  akili  yake  itakaporejea.
Hawa  wote  mtoto  mdogo  na  asiye  na  akili  timamu   mali  zao  zinaweza  kusimamiwa hata  na wakili au  kabidhi  wasii  mahakama  ikiamua  hivyo. Na  haijalishi  wakili  au mtu  mwingine  atakayeteuliwa kama atakuwa  ndugu  au  vinginevyo  suala  la  msingi ni  uadilifu  wake  na  uwezo  wa  kutunza  mali  kwa  maslahi  mema  ya watu  hao.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                        WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA         BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



0 comments:

Post a Comment