Wednesday 17 June 2015

MATOKEO YA KUFUTIWA HATI YA ARDHI.



Image result for hati ya nyumba
             
NA  BASHIR  YAKUB - 

Makala  zilizopita  nilieleza   mazingira ya  kisheria  ambapo  mtu  anaweza   kunyanganywa  ardhi  yake  na  kufutiwa  hati  miliki  na  hatimye  ardhi  kupewa  mtu  mwingine  au  kukabidhiwa  mikononi  mwa  serikali. Nilieleza  mambo  mengi  ikiwemo   sababu  ambazo  zinaweza  kupelekea mamlaka  za  ardhi  kufuta  hati  miliki  ya mtu.  Pia  nilionya  kuwa unapomiliki  ardhi  sio  kwamba  umemaliza,  hapana,  isipokuwa  kuna umuhimu  mkubwa wa  kuzingatia  na  kufuata masharti  yaliyo  katika  hati  miliki. Hii  ni  kwasababu  Sheria ya  Ardhi  imeweka  bayana  na  kutoa  mamlaka  kwa  ofisi  kuu  za ardhi  kufuta  umiliki  wa mtu  iwapo  unakiuka  masharti  ya  hati.

Pia  nikaeleza  kuwa  yawezekana  maafisa  ardhi  kutumia  mwanya huo   kuchukua  ardhi  yako  kwa  manufaa fulani  au  kwakuwa  yupo  mtu nyuma  ya  mchezo  huo  ambaye   anaitaka  ardhi  yako. Utatumika  mwanya  wa  kutotekeleza  masharti  kukunyanganya  ardhi ili  apewe  huyo  aliyesimamia  mchezo  huo. Na  mwisho  nikasema  kuwa  huwezi  kujua  kama  haya  yapo  mpaka  yakutokee  vinginevyo  unaweza  kudhani   tunaongea  vitu  ambavyo  havijawahi  kutokea. Waliofikwa  na  haya  wanajua  nazungumza  nini.

Ambao  hawakusoma  makala  hayo  hawajachelewa  andika  neno  SHERIA  YAKUB  BLOG  kwenye  mtandao  na  fungua blog  hiyo  utaona  makala  hayo  na  nyingine  nyingi  za  sheria. Makala   ya  leo  yatazungumzia  matokeo  ya  kufutiwa  umiliki,  kwa  mfano   ikiwa  ardhi  ulikuwa  umeikopea  nani atalipa  deni hilo,  pengine ardhi  ilikuwa  na  mgogoro  mahakamani  nani  ataendeleza  mgogoro  huo,  pengine kuna  mtu  alikuwa ameshalipia ardhi  hiyo  nusu  kwa  ajili ya kuinunua , haki  zake zinalipwa  na  nani,  na  vitu  vingine  kama hivyo.

1.MATOKEO  YA  KUFUTIWA  HATI     YA  ARDHI.
Kifungu  cha  49( 2 – 5) cha  Sheria  ya  Ardhi  ndicho  kinachozungumzia   matokeo  ya  kufutiwa  hati  ya  ardhi.  Hapa  chini  matokeo  yataelezwa.

( a ) Matokeo  ya  kwanza  kabisa  ni  kuwa haki  zote  za  kuwa  kama  mmiliki  ikiwemo  ile  haki  ya  kutumia  eneo  zinakwisha  palepale  na  mtu  anakuwa  anahesabika  sio  mmiliki  tena. Hii  ina  maana  hata  ukikutwa  ndani  ya  eneo  hilo   basi  utahesabika  kama mvamizi  na  ipo  haki  ya  kukufungulia  mashtaka  ya madai ya  uvamizi  kama  mvamizi  au  ya  jinai    pia  kama  mvamizi (criminal trespass). Hati  miliki  inapofutwa   si  tu  mtu  hatakiwa  kulitumia  lile  eneo  isipokuwa  hata  kuonekana  eneo  hilo   huwa ni  kosa.  Haki  zote  za  umiliki  alizokuwa  nazo  mtu  hurudi  mikononi  mwa  Rais  wa  Jamhuri  ya  Muungano  ambaye  ndiye  mdhamini  mkuu  wa ardhi yote  ya Tanzania.

( b ) Ikiwa  kuna  kesi  yoyote  iko  mahakamani  kuhusu  ardhi hiyo   basi   kama  mtu  aliyefutiwa  umiliki  ndiye  aliyekuwa  ameifungua   kudai  baadhi  ya  haki   kesi  hiyo  itachukuliwa  na  serikali  na  haki  hizo sasa  zitadaiwa na  serikali  na  kama  zitalipwa   malipo  yataingia  mikononi  mwa  serikali. Lakini  ikiwa   kesi  hiyo  aliyefutiwa  umiliki  ndiye  aliyekuwa  ameshitakiwa  na  anadaiwa  madai  fulani  kuhusu  hiyo  ardhi  basi  serikali  pia  itaichukua kesi hiyo na  kuwa  kama mshitakiwa  wa  kwanza  lakini  itamuunganisha   mtu  aliyefutiwa  umiliki  kama   mshitakiwa  wa pili  na  iwapo  hukumu itatoka  ikitaka  washitakiwa  walipe  malipo  yoyote  basi  mtu  aliyefutiwa  umiliki  ndiye  atakayetakiwa  kulipa  na  si  serikali.

( c ) Kama  kuna maendelezo  yoyote  ambayo  yalikuwa  yamefanywa  na mtu  aliyefutiwa umiliki   katika  ardhi  aliyonyanganywa  basi serikali  itatakiwa  kumlipa  fidia  sawa  na  gharama  alizotumia. Isipokuwa  malipo  hayo  yatatolewa  tu  iwapo  maendelezo  hayo  yalikuwa  ni  maendelezo yaliyoainishwa kwenye  hati  miliki. Kama  hayakuainishwa  kwenye  hati  miliki hakuna fidia.

( d  )  Ikiwa  kuna  kodi  za  ardhi au  tozo  zozote  ambazo  aliyefutiwa  hati  alikuwa  hajalipa  basi  atatakiwa  kuzilipa  kwa  kupewa  notisi  ya  siku  14  na  kisingizio  kuwa  amefutiwa  umiliki  hakiwezi  kutumika  kutolipa  malimbikizo  hayo.

( e ) Pia  serikali  haiwajibiki  kwa  namna  yoyote   kulipa Madeni  yoyote  ambayo  yalichukuliwa  na  mtu  aliyefutiwa  umiliki  kwa  kutumia  ardhi  hiyo  kama  dhamana   na  pia  haiwajibiki  kwa  wapangaji, wanafamilia au  kundi lolote  lenye  maslahi  ya kuishi  au biashara   katika  ardhi   iliyochukuliwa. Mizigo  hii  yote  ni  ya   mhusika  aliyefutiwa  umiliki.
Kwa  leo  ni  hayo  tu.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                        WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA         BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.





0 comments:

Post a Comment