Tuesday 26 May 2015

NI KOSA ASKARI KUONDOKA NA MTU MWINGINE BAADA YA KUMKOSA MTUHUMIWA NYUMBANI.


Image result for CHINI YA ULINZI WA POLISI
               
NA  BASHIR  YAKUB-

Malalamiko  ya raia  dhidi  ya  jeshi  la  polisi  hayataishi  kama  polisi  wenyewe hawatajirekebisha.  Na ieleweke kuwa  si  kweli  kwamba wanaolalamika  ni  wajinga  au hawana sababu  za  msingi.  Mara  zote  ukiangalia  malalamiko  ya  raia huwa  ni  ya  msingi  na  mzizi  wake ni  mmoja  tu.  Ni  utamaduni  wa  askari  wetu  kutopenda  kutenda  hatua  kwa  hatua  kama sheria  inavyoagiza. Sheria  imetoa  maelezo  mazuri  tu  ya namna  ya  kuyaendea  mambo. Tatizo  watekelezaji  ndio  hakuna.
 Sheria  husema  kingine  na  watekelezaji  hufanya  kingine. 

Namna  hii  huwezi  kuepuka  chuki  na  migongano  kati  ya   hawa  watekelezaji  askari  na  raia. Na  migongano  na  kutokuelewana  kunapokuwa  kukubwa  na  usalama  nao  unayumba  kwakuwa   ili  askari  afanye  kazi  ya  usalama  vizuri   anategemea  msaada  wa  raia  karibia  kwa  asilimia  zaidi  ya  80.  Na  raia  huyu hatatoa  ushirikiano  wakati  jana  umempiga  bila  sababu,  umemtukana   na  kumtolea  maneno  ya  kebehi. Makala  iliyopita  nilizumgumzia  namna  sheria  inavyomruhusu  raia  kukataa  kukamatwa  na  polisi  iwapo  polisi  huyo  atakiuka  taratibu  katika  ukamataji.  Leo  nazungumzia   namna  sheria  inavyokataza kumchukua  mtu  mwingine  baada  ya  kumkosa  mtuhumiwa  halisi  wa  kosa.  Tutaona  hili  likoje.

1.ASKARI  KUONDOKA  NA  MTU  MWINGINE  BAADA  YA  KUMKOSA  MTUHUMIWA  HALISI.

Hii  ni  tabia  ambayo  imezoeleka  sana  na  ipo  kwa  muda  mrefu. Yumkini  kuzoeleka  kwake  na  kuwepo  kwake  kwa muda  mrefu hakuifanyi  hata  kwa  sekunde  moja  tabia  hii  kuwa  halali  kisheria.  Mara  nyingi  wanaokutwa sana  na tabia  hii  ni  watu  wa  vijijini  hasa  wa  hali  ya  chini.  Lakini  hata  mijini  pia  ipo  sana.  Nazungumzia   tabia  ya  kuondoka  na  mtu   mwingine  baada  ya  kumkosa mtuhumiwa  halisi.  Kwa  mfano  askari  wamekuja  nyumbani  kumtafuta  JOHN  kwa  kosa  analotuhumiwa  nalo.  Bahati  mbaya  au  nzuri  JOHN  hayupo  nyumbani. Kutokana  na hilo   askari  wanaamua  kuondoka  na  mke  wa  JOHN  au  mtoto  wake     ili  kumfanya  JOHN  aweze  kutokea. Hiki  ndicho  ninachozungumzia.  Na wanaokuwa  wakichukuliwa  mara  kwa  mara ni  mke  wa  mtuhumiwa  , mtoto  au  ndugu. Lengo   eti  ni kumfanya  mtuhumiwa  halisi  aweze  kujisalimisha.

2.  SHERIA  INAKATAZA  KABISA  KUMCHUKUA  MTU  MWINGINE  BADALA  YA  MTUHUMIWA  HALISI.

Ni  lazima  ieleweke  na  askari  wetu  wafahamu  kuwa sheria  iko  wazi  kuwa  aliyetenda  kosa  ndiye  anayewajibika  na  kosa. Haiwi  na  haitokuwa  kosa  la  fulani  akaliwajibikia  fulani. Askari  wajue  kuwa kamwe  kisheria  hakuna  anayesimama  kujibu  kosa  la  mwingine . Ni kutokana  na  msimamo  huu mahakama  kuu katika  kutafsiri  sheria  mbalimbali  zinazokataza  jambo  hili ikasema katika  kesi  ya  LULU TITU  vs  R ( 1968 ) HCD No. 330    kuwa  ni  kosa  kubwa  kwa  askari  kumkamata   au  kuondoka  na    na  mtu  mwingine  baada  ya  kumkosa  mtuhumiwa . Katika  kesi  hiyo  askari  walikuwa  wamemkamata  na  kumchukua  mke  wa  mtuhumiwa  baada  ya  kumkosa  mme  wake  ambaye  alikuwa  anatuhumiwa.  Mahakama  ilikemea  vikali  jambo  hilo  na  kutia  msisistizo  juu  uharamu  wake  kisheria. Maamuzi  ya  mahakama ( mahakama  kuu  na  ya  rufaa)  ni  sheria na  hivyo  msimamo huo  ni  sheria.

3.  NINI  UFANYE  HILO LIKIKUTOKEA  AU  KAMA  LIMEKUTOKEA  TAYARI.

Kwanza  kesi  hiyo  niliyotaja   hapo  juu  haikuishia  kukemea  jambo  hilo  bali  ilienda  mbele zaidi  kwa  kutoa  mwongozo  wa nini  mtu  afanye  iwapo  limemtokea  hilo . Mahakama  ilisema  kuwa  iwapo    mtu  amechukuliwa  bila  kuhusika  basi  anayo  haki  ya  kufungua  shauri  la  madai  na  kudai  kulipwa fidia.  Katika   shauri  la  madai  la namna  hii utamfungulia  askari  husika  lakini  pia  utaliunganisha  jeshi  la  polisi  ambalo  ni  mwajiri  wa  askari  huyo/hao.  Lengo  la  kuliunganisha  jeshi  la  polisi  ni  ili  hukumu  itakapotoka  ya  kulipwa  fidia  basi  jeshi  hilo  ndilo  lilipe fidia  kwa niaba  ya askari  wake.  Ndugu Mtanzania hakuna  shaka  fidia  utalipwa  tu  kama  hili  limekutokea  kweli.

Pili  kitu  kingine  ambacho  unaweza  kufanya  ni  kugomea  kukamatwa/kuchukuliwa.  Katika  kesi  ya JUMA  NZIGE vs R (1964) EA  107  mahakama  ilitoa  mwongozo  kuwa  raia  ana  haki  ya  kugomea  ukamataji wowote  ambao  si  halali.  Kwa  maana  hii  ikiwa  we  si  mtuhumiwa  basi  unaweza  kukataa  kukamatwa na  hakuna  lolote  litakutokea  kwakuwa  uko  sahihi  mbele  ya  macho  ya  sheria. KATAA  UNYANYASAJI, CHUKUA  HATUA.


MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                        WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA         BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.






0 comments:

Post a Comment