Monday 25 May 2015

JE WAJUA SHERIA INAKURUHUSU RAIA KUKATAA KUKAMATWA NA ASKARI TARATIBU ZINAPOKIUKWA ?.

Image result for POLISI WAKIMPIGA

NA  BASHIR  YAKUB-

Siku  zote  wananchi  wamekuwa    wakililalamikia jeshi  la polisi  kwa  namna  linavyoendesha  shughuli  zake hasa wakati  wa  ukamataji (arrest). Matumizi  ya  nguvu, ubabe    na  kutofuata  sheria    na  taratibu  maalum  limekuwa  ndio  tatizo  kubwa  kwa  wananchi  dhidi  ya  askari.  Sio  siri  askari wamekuwa  wakitumia  nguvu  na  ubabe  mno  katika  kuwakamata raia.  Hata  pale pasipo  na  haja  yoyote  ya  kutumia  nguvu    bado  wao  wamekuwa  wakilazimisha  nguvu  nyingi  hali  ambayo  hupelekea   vurugu , kuumizana  na  hata  mauaji. Mara  nyingi  unapochunguza  matukio   mbalimbali  ya  vurugu ambayo  huwahusisha raia  na polisi  utagundua  kwa haraka kuwa  ubabe    wa askari  ndio  uliopelekea  vurugu.  Basi  leo  nitaeleza nini  ufanye  askari  anapokiuka  taratibu   hasa  wakati  wa  kukamata/kuweka  chini ya ulinzi.

1.NINI  MAANA  YA  KUKAMATA ( ARREST ).

Sura  ya  20  Sheria  ya  Mwenendo  wa  Makosa  ya  Jinai  kama  ilivyofanyiwa  marekebisho  2002  ndiyo  sheria  inayotoa  mwongozo   wa  namna  na  jinsi  ya  kumkamata  mtu.  Pamoja  na  hayo sheria  hii  haikueleza   moja  kwa  moja  nini  maana  ya  kukamata. Hata  hivyo  kutokana  na  miongozo mbalimbali  ya  kimahakama  ambayo  hutumika  kutafsiri  sheria  hii  tunaweza  kupata  tafsiri  ya  neno  kukamatwa  kwa  kusema  kuwa  ni  tendo  la  kumzuia  kwa  muda   raia  ambaye  inatuhumiwa  kwa  kosa  fulani,   ambalo  hufanywa  na  mamlaka  husika. Kwa tafsiri  hiyo  tendo la kuzuia  lazima  liwe    la  muda,  raia  anayekamatwa  lazima awe  ametuhumiwa, na pia  ukamataji  lazima  ufanywe  na  mamlaka.  Huo  ndio  utakuwa  ukamataji ( arrest).

2.  NANI  NA  NANI  WANARUHUSIWA  KUMKAMATA  RAIA ( ARREST ).

Kwanza  kifungu  cha  14  cha  Sheria  ya Mwenendo  wa  Makosa  ya  Jinai kinampa  mamlaka    askari  polisi kumkamata  au  kumweka  chini  ya  ulinzi   raia mtuhumiwa  . Hii ni  kusema  kuwa  mamlaka ya  kukamata aliyonayo  askari  yeyote  ameyapata  kutoka  kifungu  hiki.

Pili  kifungu  cha  18 cha  sheria  hiyohiyo   kinampa  hakimu  yeyote  mamlaka  ya  kumkamata  raia mtuhumiwa.  Mahakimu  wamegawanyika,   wapo  mahakimu  mahakama  za  mwanzo,  mahakimu mahakama  za  wilaya  na  mahakimu mahakama  za  hakimu  mkazi. Hawa wote  ni  mahakimu    na wanayo  mamlaka  ya  kumkamata  mtuhumiwa  kwa  mujibu  wa  kifungu  hiki.

Tatu  kifungu  cha  16 cha sheria  hiyohiyo  kinatoa  mamlaka  kwa raia yeyote  kumkamata mtu anayetenda  kosa.  Hapa tofauti  ni  kuwa  mamlaka  ya  raia  kumkamata raia  mwenzake  ni  madogo  na huwezekana  pale tu ambapo  mtuhumiwa  ametenda  kosa  kubwa  na  pengine  kuna  wasiwasi  kuwa  anaweza  kutoroka  asipozuiliwa  haraka  na  kwa  muda  huo. Lakini  kama  mazingira  si  haya basi   raia    anatakiwa  kutoa  taarifa   polisi  ili  wao  wenyewe ndio  wafanye  kazi  hiyo.

3.  MATUMIZI   YA  NGUVU  HAYARUHUSIWI  WAKATI  WA  KUMKAMATA  RAIA.

Kifungu  cha 21 cha  sheria  hiyohiyo  kinakataza  kabisa  matumizi  ya nguvu  wakati  wa kumkamata  raia. Matumizi  ya  nguvu  ni  pamoja  na  kumpiga  raia, kumfunga  pingu, kumshika  suruali  kwa  kumningiza, kumtukana au  matumizi  yoyote  ya  lugha  chafu  na  kila  kitu  kinachofanana  na  hayo.

4. SHERIA  INAKURUHUSU  RAIA  KUKATAA KUKAMATWA   ASKARI  ANAPOKIUKA  TARATIBU.

Katika  kesi  ya  Nzige  Juma  vs R (1964) EA 107 uk 147  mahakama  ilisema  kuwa  ikiwa  mtu   atakamatwa   bila  kufuata  utaratibu  basi  mtu  huyo anaruhusiwa  kugomea  ukamataji  huo. Huu  ndio  uamuzi  wa  mahakama  na  kwa  mujibu  wa  sheria  uamuzi  wa  mahakama  ni sheria  na  hivyo  maamuzi  hayo  ni  sheria. Kwa sheria  hii  nitoe  mwito  kwa  raia  kutowaonea  aibu  askari  polisi  wanaokiuka  taratibu  ikiwa  ni  pamoja  na  matumizi  ya  nguvu  katika  ukamataji  kwa  kuwagomea. Ieleweke  kuwa  kugoma  katika  hili  si  kuvunja  sheria  bali ni  kutekeleza sheria. Ni  haki    yako  kama  zilivyo  haki  zako  nyingine. Na  kugoma  katika  hili  hakuwezi  kukuletea  shida  yoyote  na  hivyo  huna  haja  ya  kuwa  muoga.  Kumbuka  kama  wewe  mwenyewe  hautaweza  kulinda  haki  zako  hakuna  atakayelinda  haki  hizo  kwa  niaba  yako. Wewe   ndio  unatakiwa  kuwa  wa  kwanza  kulinda na  kusimamia  haki  zako  kwa  msimamo   usioyumba na  bila  woga  huku  ukiamini  kuwa  uko  salama  mbele ya  sheria. Chukua  hatua  sasa kwa  kukataa  na  kugomea  ukamataji  uliokiuka  taratibu.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                        WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA         BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.





0 comments:

Post a Comment