Tuesday 14 April 2015

NAMNA YA KUMSHITAKI DAKTARI ALIYESABABISHA MADHARA AU KIFO KWA MGONJWA.


Image result for madaktari tanzania

NA  BASHIR  YAKUB-

Wako  watu  wengi  wameathirika  kutokana  na  matendo  yanayotokana  na  uzembe,kutojali  au  makusudi ya madaktari. Wapo  waliopata  vilema    vya muda  kutokana  na  uzembe  huo,  wapo  waliopata  vilema  vya  maisha  na  wapo  waliouliwa  na  madaktari hawa hawa.  Ajabu  ni kuwa  ukifanya  tathmini  ya  haraka  utaona kuwa    watu  wote waliopata  madhila    kutoka  kwa  madaktari  huhusisha  madaktari  wa serikali  na  katika  hospitali  za  serikali.  Si   rahisi   kukuta  jambo  la ajabu  la  kitabibu  limehusisha  hospitali  binafsi.  Swali  langu   ni  kuwa,  ewe   

Mtanzania  daktari  amekusababishia   tatizo  iwe  ugonjwa  wa kudumu,  ulemavu  wa  muda  au  wa  kudumu,  au  hata  kifo  cha   ndugu  au  jamaa,  umechukua  hatua  gani   baada  ya  tukio hilo  ?.  Umekaa  kimya  ukiwa  umeridhika  au  umekaa  kimya  kwakuwa  hujui  la  kufanya ?.

1.INARUHUSIWA   KUMSHITAKI  DAKTARI  KWA  KUSABABISHA    MADHARA   KWA  MGONJWA  WAKATI  WA  TIBA.

Wapo  wanaodhani  kuwa  madaktari  hawashitakiwi kwa  kutomhudumia  vyema  mgonjwa.  Hili    si  kweli  daktari  ni  mtumishi  sawa  na  watumishi  wengine    na  kosa  lolote  la  uzembe,  kutojali  au  makusudi  analofanya  na  kusababisha  madhara  kwa  mgonjwa  sheria  inaruhusu  kumchukulia  hatua    daktari  huyo. Sawa  na  mtumishi  mwingine  akitenda  kosa kazini  anaadhibiwa  ndivyo  ilivyo  kwa  madaktari  pia. Kwa    mujibu  wa  sheria  daktari  amepewa  wajibu  wa  hali  ya  juu  kuhakikisha  anatumia  taaluma  yake,  weledi  na  uadilifu  katika  kutoa  huduma  ya  tiba    na  kuepuka  kabisa  hatua au  namna  yoyote  inayoweza  kuleta   madhara  kwa  mgonjwa.

Takwa  hili  kwa  daktari  ni  takwa  la  kisheria  na  wala  si  hiyari. Kwa  hiyo  watu  waelewe  kuwa  suala  la  daktari  kutoa  matibabu   kwa  umakini  ni  lazima.  Kitu   kikiwa  lazima (mandatory)  katika  sheria  maana  yake ni  kuwa  kutofanyika  kwake  hutoa  haki  ya  mtendewa  kushitaki.  Hivyo  ndivyo  ilivyo  kwa  madaktari.  Kwa  namna  yoyote  anapokosa  umakini  katika  kutoa  tiba  basi    ni  ruhusa  kwa  mtendewa  kushitaki.

2. MADHARA   YALIYOSABABISHWA  NA  MADAKTARI  TANZANIA.

Miaka  ya  nyuma   wapo  watu hospitali  ya  muhimbili   walifanyiwa  upasuaji   huku  kila  mmoja  wao  akifanyiwa   sehemu  ambayo  haihusiki. Ni  kisa  maarufu    kila  mtu anakumbuka   ambapo  mmoja  alifanyiwa  upasuaji  wa  goti   wakati  akiwa  na  tatizo  la  kichwa  na  mwingine  akafanyiwa  kichwa    akiwa  anaumwa  goti. 

 Mwaka  jana  msanii  mmoja  wa  sanaa  maigizo bongo  movie   alifariki   katika mazingira  ya kutatanisha  baada ya  kupigwa  picha  miale (xray)   na  kusomewa  kuwa  ana  matatizo  ya  utumbo   na  kuanza  kupatiwa  matibabu  ya  utumbo  pale Mwananyamala. 
Hali  ilizidi  kuwa  mbaya  akarufaniwa  muhimbili  ambapo  madaktari  bingwa  wakathibitisha  kuwa  aliyesoma  picha  miale (xray)  alikosea  tatizo  la  mgonjwa  halikuwa  utumbo  na  kuwa   amepoteza  muda  mwingi  katika  matibabu  yasiyohusika  na  hivyo  amechelewa  jambo  ambalo  lilipelekea  kifo  chake.  

Matukio  ya  mwananyamala   nayo  ni  mengi  huo  ni  mfano  tu.  Kisa kingine  cha  hivi  karibuni    ni kile  kilichotokea   mkoa  wa  Tabora    urambo  ambapo   daktari  alimfanyia  upasuaji  wa  tumbo  mwanamke  na  kusahau  kitambaa  ndani  ya  tumbo  la  mama  kitu  kilichopelekea  kuanza kuoza  utumbo  hadi  kufikia   kizazi nacho  kuoza  na  kuharibka  kabisa.  Mungu  mkubwa  mama  huyo alinusurika  kifo.  Visa  vya  namna  hii  vya  kusahau  visu, mikasi,  vitambaaa   kwa  akina  mama  wakai  wa  kujifungua  navyo  havina  idadi  nchini  mwetu.  Inasikitisha  sana.

3. NAMNA  YA  KUMSHITAKI  DAKTARI   ALIYESABABISHA  MADHARA.

Natoa   ushauri  na  hamasa  kuwa   imefikia  wakati  sasa  tuwashitaki  hawa  madaktari  na  serikali  yao  ili   kwa  kulipa    fidia  kubwa   wawe  makini  na  wapate  funzo  na  hii  itakuwa  ni salama  kwa  raia.  Nimesema  hapo  juu  kuwa  daktari  akisababisha  dhara  kwa  uzembe, kutojali  au  makusudi  kwa  mgonjwa  anashitakiwa. Namna   nzuri  ya  kushitaki  ni  kuomba  kulipwa  fidia  ya  hela  kutokana  na  madhara  uliyopata  au  aliyopata  ndugu  yako. 

 Kwakuwa  suala  ni  kutaka  kulipwa hela  basi  ikiwa  unataka  ulipwe  kuanzia  shilingi  moja  mpaka  milioni   100  basi  fungua  shauri  hilo   mahakama  ya  wilaya  au  ya  hakimu  mkazi  wengi  huiita  mahakama  ya  mkoa.  Na  ikiwa  unataka  ulipwe   zaidi  ya  milioni  mia  moja  mpaka  bilioni  au  tirioni  na  kuendelea  basi  shauri  hilo  lifunguliwe  mahakama  kuu. Hii  ni  kwa  mujibu  wa  sheria.   Hakikisha mahakama  utakayofungua  shauri  kama  ni  ya  wilaya iwe  ni  ile  ambapo  tukio  hilo  lilitokea. 

 Kama  ilitokea  wilaya  fulani  basi  mahakama  ya  wilaya  hiyo ndiyo  ina  mamlaka  ya  kusikiliza    shauri  hilo.  Na  kwa  upande  wa  mahakama  kuu   fungua  mahakama  kuu  iliyo  katika kanda   ambapo  lilitokea  tukio. Na  hiyo  ni  kwa  mujibu  wa  sheria pia.  Katika  kushitaki  mshitakiwa  namba  moja  atakuwa  daktari  aliyesababisha  madhara,  pili  utaunganisha  hospitali husika  ikiwa  kama  mshitakiwa  namba  mbili   na  tatu  utaunganisha  halmashauri  ya  wilaya  husika  ikiwa  kama  mshtakiwa  wa  tatu.  

Kisheria  shauri  la  namna  hii  huwezi  kumfungulia  daktari  peke  yake  bila  kuwaunganisha  hawa waajiri  wake. 
Hii  ni  kwasababu    yale  mamilioni  ya  hela  unayodai  inabidi yalipwe  na  hospitali  husika  au  halmashauri kwasababu  wao  ndio  wanaomjua  huyo  daktari.  Katika  kesi  iliyotolewa  hukumu wiki  hii  na  jaji  wa kanda ya Tabora  Jaji  Amir  Mruma   halmashauri  ya  wilaya  ya  Urambo  imeamrishwa   kumlipa Mwamini  Adam  kiasi  cha  milioni  25  kutokana  na  uzembe  wa  daktari  uliomsababishia  madhara.  Hii  ndio  sheria  na  ndivyo  ilivyo  tuchukue  hatua  sasa.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                

VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.

-WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA                    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.

-UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA   WANASHERIA     WETU.

-UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA                 BURE.

-IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA              MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.





0 comments:

Post a Comment