Wednesday 11 March 2015

NAMNA YA KUMSAIDIA NDUGU YAKO KUPATA DHAMANA POLISI.



Image result for akiwa mbaroni

NA  BASHIR  YAKUB-

1.DHAMANA  NININI.

Dhamana  ni  hatua ambapo   mtu  ambaye  tayari  ni  mtuhumiwa wa  kosa  fulani  huachiwa  huru  kwa  muda  ili  kusubiri  hatua  za  kufikishwa  mahakamani  au  kama  tayari  amefikishwa  mahakamani   husubiri  kuendelea  kwa  kesi  yake.  Kwahiyo ili  lije  suala  la  dhamana  ni  lazima  uwe  umetuhumiwa  polisi  au tayari umefikishwa  mahakamani. Ieleweke  kuwa  kuna  aina kuu mbili  za  dhamana. Kwanza  dhamana  ya  polisi  na  pili  dhamana  ya  mahakamani.Hapa  tunazungumzia  dhamana  ya  polisi.

2.UKIOMBWA  HELA  KWA  AJILI   YA  DHAMANA  KATAA.

Dhamana hutolewa bure. Ieleweke  wazi  kuwa  hakuna malipo yoyote yanayotakiwa kutolewa ili mtuhumiwa au mshtakiwa akubaliwe dhamana. Mchezo huu wa  kuomba  hela  ili  mtu  apate  dhamana  umetamalaki  zaidi vituo  vya  polisi. Wewe kama  raia unalotakiwa  kujua ni moja  tu  kuwa  hakuna  sheria  inayomtaka  raia  kutoa  hela  ili  apate  dhamana. Serikalini  hakuna  risiti  ya  malipo ya  dhamana. Kama  wewe  utaamua  kutoa  hela  hiyo ujue umetoa  kwasababu  zako  lakini  sheria  iko  hivyo.Ifikie  hatua  raia  wajisimamie  kwa  kukataa  kutoa  hela  kununua  dhamana.
Hakuna  kitu  ambacho  askari  anaweza  kukufanya ikiwa utakataa  kutoa  hela  kwa ajili ya  dhamana. 

Hakipo  kabisa  kinachohitajika  ni ujasiri  wako tu  kwa  kumwambia  askari  kwamba  sikupi  hela  kwakuwa  dhamana  hainunuliwi. Usikubali  kutoa  hela  kwa  ajili ya  dhamana ndugu ni  kosa  na  hela  hizo ni rushwa. Na  hiyo  ni  kwa  dhamana  zote  ya  polisi  pia  ya  mahakamani. Katika  taratibu za  kupata  dhamana  hamna  kulipa  hela.

3. POLISI  WANALAZIMIKA  KUKUPA    DHAMANA .

Hapo  juu  nimesema  kuwa  ili  upate  dhamana  hutakiwi  kutoa  hela  isipokuwa  kuna  mambo  yanazingatiwa ili upate dhamana. Baadhi  ya  mambo  hayo  ni haya.

( a ) Kisheria ikiwa makazi yako au  anuani  yako ya  makazi    inajulikana vyema au  haijulikani  lakini  umewafanya  polisi  kuijua na  wakajiridhisha  kwamba  kweli   fulani  haya  ndio  makazi yake  basi ni  sababu  ya  kupatiwa dhamana. Hii ni kwasababu lengo kuu  la dhamana ni ili utakapohitajika upatikane  kwa urahisi.

( b )Pili, ikiwa kosa  alilotenda mtu ni la kudhaminika  hakuna  haja  ya  kuendelea  kumshikilia. Sheria imeshaweka  wazi  makosa  yapi  dhamana ya  mtu  itolewe  na  makosa  yapi  isitolewe. Baadhi  ya  makosa  ambayo  mtu  hatakiwi kupata  dhamana  ni  kama  kuua(murder), uhaini,wizi  wa silaha n.k. Ajabu  ni  kuwa  kwenye  vituo  vyetu  vya  polisi unakuta  hata  mwenye  kosa  la  kutukana naye  kanyimwa dhamana. Hii  ni  kinyume  cha  sheria na  muda  umefika wa  raia wenyewe  kuyakataa  haya.

( c ) Pia  kama mtuhumiwa  hana  kumbukumbu (criminal records)  zozote za uhalifu nayo ni  sababu  au  kigezo  cha  kumfanya  apewe  dhamana  haraka. Hakuna sababu  ya  kuendelea  kumshikilia  mtu  ambaye kwa  kumbukumbu  hakuwahi  kutenda  kosa lolote la jinai hapo  kabla. Kisheria kutokuwa  na  kumbukumbu  za  uhalifu hapo  awali  ni dalili  za  uaminifu  na  ukweli. Hii  nayo  ni sababu  ya  kisheria na yafaa  izingatiwe  sana  huko vituo  vya  polisi.

( d ) Pia  ikiwa polisi itajiridhisha kwamba mtuhumiwa atatimiza masharti ya dhamana atakayopewa kama kufika siku na saa atakayoamriwa  basi hakuna  haja  ya  kumgangania  mtu. Hii  nayo  ni kati  ya sababu  ya  kisheria  ambayo huwa  haipewi nafasi kwenye  vituo  vya  polisi na  hivyo kuendelea  kulifanya  suala  la dhamana  kuwa  gumu.

4.  NAMNA  YA  KUJIANDAA  NA DHAMANA.

Ni  vema  sana  unapopata taarifa  za  ndugu  yako  kushikiliwa  kituo cha  polisi  kujiandaa  na  dhamana. Usitoke  nyumbani  kwenda  kituoni  bila  kujiandaa  na  dhamana. Na hii ni iwe  una  uhakika  amefanya  kosa fulani au  huna  uhakika. Zaidi  kama  unajua  kosa  lake  ni  la  kudhaminika  basi  umuhimu  wa  kujiandaa  na  dhamana  huongezeka. La kuzingatia sana hakikisha  unapotoka  nyumbani  una  barua  inayokutambulisha  kwa suala  la  dhamana  kutoka  serikali  za  mitaa, ukienda serikali  za  mitaa  wanazijua  hizi  barua. Pia  kama  ni  mwajiriwa  usisahau kwenda  na  kitambulisho  chako cha  kazi. Hii  husaidia kutopoteza  muda kwa kurudishwarudishwa huku ndugu yako akiendelea kusota. Kwa  kujiandaa  utamwokoa  ndugu yako  na  dhahama  ya  kulala au kukaa  selo. Usiende  polisi ukiwa  hujajiandaa  kwakuwa kufanya  hivyo  ni kupoteza  mda tu. .

5. OMBA  KUJIDHAMINI  MWENYEWE   INARUHUSIWA.

Kuna  watu  wamekuwa  wakikosa  dhamana  kwa  kukosa  wadhamini. Lakini  polisi  wamekuwa  hawawaelezi  watu  hawa  haki  hii  ya  kujidhamini  wenyewe. Mtu akikosa  mdhamini  na  polisi  nao  wanakaa  kimya mtu anaendelea  kusota. Hili  si  sawa  kwakuwa  moja ya majukumu  waliyonayo  polisi  ni  kuwaelimsha  watuhumiwa   haki  zao  za  msingi. Aidha kama  ulikuwa hujui  ndio  ujue  kuanzia  leo  kuwa  inaruhusiwa  kujidhamini  mwenyewe na  ukaondoka  kituo  cha  polisi  bila  kuhitaji  ndugu  yeyote  kukudhamini.  Unachotakiwa  kufanya  kama  uko  mikononi  mwa  polisi ni  kusema  tu  kwamba  nahitaji kujidhamini  ili  upewe  fomu  maalum uijaze  na  uondoke. Usisahau  kuliomba  hili  ni  haki  yako.  

6.  UMUHIMU  WA  DHAMANA.

Kwanza  ni kumfanya  mtu  kuwa  huru kama raia wengine wote  na  pili ni  kumfanya mtu kuwa nje ili aweze kujiandaa kukabiliana na tuhuma zinazomkabili kabla ya hajafikishwa mahakamani mfano kupata msaada wa kisheria.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,  0714047241   bashiryakub@ymail.com


                                                    TANGAZO   MUHIMU

VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.

-WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA                    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.

-UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA   WANASHERIA     WETU.

-UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA                 BURE.

-IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA              MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.





1 comments:

  • Komango Hill says:
    9 October 2022 at 12:14

    Very simple and clear , thanks

Post a Comment