Sunday 22 March 2015

JE UNASUMBULIWA NA MGOGORO WA ARDHI, IJUE SEHEMU YA KUPATA HAKI.


Image result for BARAZA LA NYUMBA NA ARDHI

                      
NA  BASHIR  YAKUB-

Wako  watu  ambao  wamekuwa  wakipata  matatizo mbalimbali  ya  ardhi  lakini  wasijue  la  kufanya.  Kati  ya  hao  wapo  ambao  migogoro  imeanzia  mikononi  mwao   na  wengine   wamerithi  migogoro  hiyo kutoka  kwa  wazazi  au  ndugu  zao. Yote  kwa  yote    iwe  mgogoro  umeanzia  mikononi  mwako  au  umeurithi  bado mgogoro  ni  mgogoro  na  lazima  utafute jambo  la   kufanya  ili  kuumaliza. Nitakachoeleza  hapa ni  namna  gani  waweza  kumaliza  mgogoro  wa  ardhi  kwa kutumia  vyombo  tulivyonavyo  pamoja  na  sheria  zetu.

1.AINA  ZA  MIGOGORO  YA  ARDHI.

Migogoro  ya  ardhi  imegawanyika  katika   namna  tofauti. Pamoja na  kugawanyika  katika  namna  tofauti  lakini  bado  asilimia  kubwa  ya  migogoro  huhusisha  umiliki. Migogoro  ya  umiliki  baina  ya  watu  wawili au  zaidi  huku kila mmoja  akidai  kuwa  mmiliki  halali  aidha  kwa kununua  eneo  husika,  au  kudai  kurithishwa, au  kudai  kupewa  zawadi, au  kudai  kugawiwa  na  mamlaka  za  serikali n.k. ndiyo  inayoongoza . Migogoro  mingine  ni kama  kumiliki  eneo  maeneo  yasiyoruhusiwa  kisheria  kama  hifadhi  za  barabara, maeneo maalum  yaliyotengwa kwa  miradi  kama  shule, hospitali n.k . Migogoro  mingine ni  kuuziwa  eneo  ambalo  tayari  mwenye  nalo  ameliweka  dhamana  sehemu  fulani.  Kwa ufupi migogoro  ni  mingi  hiyo  ni  baadhi  tu.

2. NATAKA  KUMALIZA  MGOGORO  WA ARDHI  NIFANYEJE

Kama  unasumbuliwa  na  mgogoro  wa  ardhi  na  unahitaji  kuumaliza   tunashauri  mambo  yafuatayo  ya  kitaalam.

( A ) KUFANYA  SULUHU.

Hiii  ni  njia  ambayo  ipo  kisheria    na  inaweza  kutumika  muda wowote  kabla  ya kufungua  kesi  au  hata  baada  ya  kufungua  kesi. Ni njia ambayo   hutumiwa  na  wahusika  katika  mgogoro  ambapo suluhu  ya  mazungumzo  hufanyika   na  wahusika  hutumia  busara  zao kuelewana. Unapoamua  kutumia  njia  hii  jitahidi  sana  kupunguza msimamo mkali ulionao kuhusu  ardhi  inayogombewa. Baadhi  ya  mambo  kama  hayana  umuhimu  sana  amua  tu  kuachana  nayo  ili  kuweza  kumaliza mgogoro.  Wakati suluhu inaendelea   jitahidi  sana  kushuka  au  kujishusha  ili kuwezesha kufika  muafaka. Lengo  ni  kuepuka  gharama  kubwa  zaidi  mbeleni , kuepuka kupoteza  muda, pia  kuepuka kuharibu  mahusiano na wale  ulionao  kwenye  mgogoro. Ikiwa  makubaliano  yatafikiwa  kupitia  hili  basi  yatawekwa  katika  maandishi  maalum  ya  kisheria  na yatakuwa  na  nguvu  za  kisheria  na hayatakiukwa  tena. Na kama  mgogoro ulikuwa  umeshafika  mahakamani basi  yale  makubaliano   yatapelekwa mbele   ya  hakimu  au  jaji   yatasajiliwa   na  yatakuwa kama hukumu  ya   mahakama. Hii  itakuwa  njia  ya  kwanza  ya  kumaliza  mgogoro  wa  ardhi.

( B )  PELEKA  MALALAMIKO  YAKO   BARAZA LA  ARDHI  LA  KATA.

Migogoro   midogodogo  ya  ardhi  kama kugombea njia, jirani  kutanua  eneo  mpaka  kuingia  eneo  lako kwa  kiasi  kidogo, kutiririsha  maji  kwenye  eneo  la  jirani, kushindwa  kuacha  uchochoro  au  kugombea  uchochoro, na  mgogoro  mwingine  wowote  ambao  thamani  ya  eneo  linalogombewa haizidi  milioni  tatu  hupelekwa  baraza  la  ardhi  la  kata. Thamani  ya  eneo  linalogombewa kama  itazidi  milioni  tatu  basi  usipeleke  mgogoro  huo  baraza    la  kata  kwakuwa  sheria  inakataza  na  hivyo  utakuwa  umepoteza  muda. Kila  kata  uliyopo  baraza  la  kata  la  ardhi  lipo na  hivyo  mgogoro  wako  upeleke  hapo  utapatiwa  suluhu.

( C )  PELEKA  MALALAMIKO  YAKO  BARAZA  LA  ARDHI  NA  NYUMBA  LA  WILAYA.

Ikiwa  hukuridhika  na  maamuzi  ya  baraza  la  ardhi  la  kata  basi  waweza  kuendelea  mbele  kwa  kupeleka  mgogoro  baraza  la  ardhi  la  wilaya. Kila  wilaya  inalo  baraza  lake  ukiuliza   maeneo  ya  makao  makuu  ya  wilaya  yoyote   utaoneshwa. Baraza  hili  husikiliza   migogoro  mikubwa  kidogo  kuliko  ile  ya  baraza  la  kata. Muhimu  hakikisha   ardhi  unayolalamikia  thamani  yake haizidi  milioni  hamsini  kabla  ya  kupeleka  malalamiko. Sheria  imesema   wazi  kuwa  ardhi  inayolalamikiwa  inatakiwa  isizidi  thamani  ya  milioni  hamsini ili  baraza  la  ardhi  la  wilaya  liwe  na  uwezo  wa  kutatua  mgogoro  huo. 

Hivyo  usipate  usumbufu  kwenda  baraza  la  wilaya  iwapo  thamani  ya  ardhi unayolalamikia inazidi  milioni  hamsini. Kufungua  malalamiko  katika  baraza  hili  utafika  lilipo  baraza  utaomba  kupewa  fomu   namba  moja  utapewa  na utaijaza  kwa  msaada  wa   afisa  wa  mahakama  au   wewe  binafsi  kama  unaweza. Pia  waweza  kumtumia  mwanasheria  katika  kuandaaa  malalamiko  katika  hili  baraza.  Pia  inaruhusiwa  kumtumia  mwakilishi katika  kuandaa  malalamiko  na  kusimamiwa  mpaka  mgogoro  kuisha.

( D )  PELEKA  MALALAMIKO  MAHAKAMA  KUU  YA  ARDHI.

Ikiwa  hukuridhika   na  maamuzi ya   baraza  la  wilaya  sheria  inakuruhusu  kupeleka  malalamiko  mahakama  kuu  kitengo  cha  ardhi. Ikiwa  utaamua  kupeleka  malalamiko  yako  mahakama  kuu  ya  ardhi  hakikisha  thamani ya  ardhi  unayolalamikia  inazidi  thamani ya milioni  hamsini.  Ikiwa  chini  ya  milioni  hamsini   usipeleke  malalamiko  kwakuwa  utapoteza  muda  mwingi  na  baadae  kabisa  utawekewa  pingamizi  kuwa  mahakama  haina  mamlaka  ya  kusikiliza mgogoro  huo  na  malalamiko yako  yatatupiliwa  mbali.

Nimalizie  kwa  kusema  kuwa  ni  muhimu  sana  kujua  wapi  ukalalamike  hasa  ukichukulia  ukweli  kuwa  mgogoro  wa  ardhi   waweza  kukuta  muda  wowote. Ni  muhimu  kujua  wapi  ukapate  haki. Kujua  jambo  kama  hili kutakuepusha  kupoteza  muda kushughulikia  mgogoro  katika  njia  ambazo mwisho  haziwezi kusaidia  au  hata  zikisaidia  suluhu  yake  si  ya  kudumu  na  pia  haina  ulinzi  wa  sheria. Maeneo  ya  kulalamika niliyoeleza  hapa  ni  maeneo  ya  kisheria  na  suluhu  yake  ina  ulinzi  kisheria  na  hakuna  wa  kukiuka.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                

VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.

-WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA                    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.

-UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA   WANASHERIA     WETU.

-UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA                 BURE.

-IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA              MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.








0 comments:

Post a Comment