Tuesday 17 March 2015

ILI KUBADILI HATI YA NYUMBA/KIWANJA KWA HARAKA ANDAA NYARAKA HIZI

Image result for KIWANJA


NA  BASHIR  YAKUB-

Watu  wengi  wanaonunua  ardhi  wamekuwa  wakipata  usumbufu  mkubwa katika   kubadili  majina  yaani kutoka  mmiliki  wa  mwanzo  kwenda  kwa  mmilki mpya  aliyenunua. Upo  usumbufu ambao  husababishwa   kwa  makusudi na  maafisa  wanaohusika   lakini  pia  upo  usumbufu  ambao  husababishwa   na  watu  wenyewe  wanaotaka  kubadili  majina.  Awali  ya  yote  lazima  nikiri   kuwa  baadhi  ya  maafisa  wa  mamlaka  za  ardhi  husababisha  uchelewaji  kwa  makusudi  kabisa  na lengo  likiwa kujenga  mazingira   ya  kupozwa kidogo. Hili  lipo  na  kila  mtu  ambaye  amekuwa  akishughulikia  masuala  ya  hati  na  kubadili  majina  miliki   kama  mimi  atakiri  kukutana  na  haya.  Hao  tuwaache  mimi  leo  nazungumzia  maandalizi  ambayo  ukiyafanya  mapema  utafanikiwa  kwa  urahisi na  haraka  kubadili   jina  la  kiwanja  au  nyumba  kutoka  kwa  mtu akiyekuuzia  kuingia jina  lako.

1.UMUHIMU  WA  KUBADILI  JINA  HARAKA  BAADA  YA  MANUNUZI.

Sheria  iko  wazi kuwa  ambaye  jina  lake  linaonekana  kwenye  hati  ndiye  mmiliki.
Kwa  kauli  hii   mnunuzi  anatakiwa  kufanya  jitihada  za  haraka  na za  makusudi  kubadili  jina  mara tu baada  ya  kununua  kiwanja  au  nyumba. Sikatai  kuwa  kunakuwa  na  mkataba wa  mauziano  lakini  lazima  ieleweke  kuwa  mbele  ya  macho  ya  sheria   jina  lililo  kwenye  hati  lina  uzito  kuliko  mkataba  wa  mauziano. Usiridhike  kukaa  na  mkataba  wa  mauziano  ikiwa  hujabadili  jina. Hii  ni  kwa  ajili  ya  ulinzi  wako  na  wa  ardhi  yako.  

Utakapotokea  mgogoro   wa  umiliki  ikiwa  hujabadili  jina waweza  kuwa  katika  hatari  kubwa  ya  kupoteza  hasa  kama  mgogoro  huo  umeanzishwa  na  aliyekuuzia. Huu  ndio  ukweli  na  lazima  tuonyane  ili    tuwe  salama na  mali  zetu. Lakini pia  hata  ukitokea  mgogoro  mwingine  wowote  wa  umiliki  kuna  mambo  ndani  ya  sheria  yataufanya  kuwa   mgumu kutokana  na sababu  tu  kuwa ulikuwa  hujabadili   jina.  Hapo  sijaongelea  faida  nyingine  za kubadili  jina  kama  kukopa  n.k. Nishauri  tu  kwa  ufupi  kuwa  unapojiandaa  kununua  nyumba  au kiwanja  jiandae  pia na  kubadili  jina  moja  kwa  moja.  Hakikisha  haya  mawili  yanakwenda   pamoja.

2. ILI  KUBADILI  HATI  KWA  URAHISI  NA  HARAKA   HEBU  ANDAA  NYARAKA  HIZI.

( a ) NYARAKA  ZA  UHAMISHO

Nayaraka  za  uhamisho  zinajumuisha  fomu  namba 29  ijulikanayo  kama  fomu  ya  kusudio  la  uhamisho( notification  of disposition) ambayo  hueleza  nia  na  lengo  la  muuzaji  kutaka  kubadili  jina  au  kuondoa  jina  lake  katika  hati.  Hii utaandaa  nakala  tatu . Pili  ni fomu  namba  30  ambayo  hujulikana  kama  fomu  ya  idhibati  ya  uhamisho ( application  for  approval  of  disposition).  Katika  fomu  hii  muuzaji  pia  atakuwa  anatoa  idhini  kwa  mamlaka  za  ardhi  kuidhinisha  hiari  yake   ya kuachia  umiliki  kutoka kwake   kwenda  kwa  mtu  mwingine ambaye  ndiye  mnunuzi.   

Mwisho  ni  fomu  namba  35  ijulikanayo kama fomu  rasmi  ya  kuhamisha  umiliki ( transfer of a  right  of  occupancy)  ambayo  ndiyo  rasmi  sasa  huhamisha  umiliki  kutoka  kwa  muuzaji  kwenda   kwa mnunuzi. Hii  ndiyo  humpa  mnunuzi  umiliki  rasmi . Pia  mkataba  wa  mauziano  ni  nyaraka  ambayo  itaambatanishwa  hapa.
Kwa  kiwanja  au  eneo  ambalo  halijaendelezwa ( halijajengwa)   huandaliwa  kitu  kiitwacho  commitment  bond  kikiwa  kama  ziada  ya  nilivyotaja  hapo.  Fomu  zote  hizo  pamoja  commitment  bond  hupatikana  katika  ofisi  za  wanasheria  na  huandaliwa  na  wanasheria.

( b )  TAARIFA  YA UTHAMINI.

Taarifa  ya  uthamini  ni taarifa  rasmi  ambayo  hutoa  tathmini  ya  thamani  ya  eneo/jengo.  Lazima  umtafute  mthamini( valuer) ili   athamini thamani  ya  eneo/jengo  lako  na  hiyo  taarifa  iwasilishwe mamlaka  za ardhi  ili iweze  kupitishwa  na mthamini  mkuu  wa  serikali  Wizara  ya  nyumba  na makazi. Ukienda  mamlaka  za  ardhi  uliza  utawakuta  wathamini  ili  wakufanyie  kazi  ya  uthamini  ninayoongelea  hapa.

( c  ) URAIA

Sheria  iko  wazi  kuwa wanaotakiwa  kumiliki ardhi  ni  raia  wa  nchi  hii tu. Hivyo  unapotakiwa  kupata  hati  ya  umiliki  lazima  pia  uthibitishe  Utanzania  wako. Hapa   utatakiwa kuandaa  nakala(copy)   ya   cheti  cha  kuzaliwa ambayo  imethibitishwa( certified)  na  wakili  au  nakala  ya  pasipoti  ambayo  imethibitishwa  na  wakili  au  kama  huna  hivyo  vyote  basi  yakupasa  kuandaa  kiapo( affidavit).

( d ) ADA

Ni muhimu  pia  unapofanya  taratibu  za kupata  hati  au  kubadili  jina  kujiandaa  na  malipo  ya  ada  za ardhi. Ada  ziko  aina  tatu  kwanza stamp  duty  fee, consent/approval  fee,  registration  fee. Sitaweka  viwango  vya  ada  hizi  kutokana  na  kubadilikabadilika  kwake .
Mwisho  niseme  kuwa  ikiwa  utajiandaa  vyema  na  haya  utapata  hati  kwa  urahisi   au  kama unabadili  jina  utabadili  kwa  urahisi  pia. Jiandae epuka  usumbufu.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com
                                              
                                           TANGAZO   MUHIMU                                                

VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.

-WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA                    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.

-UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA   WANASHERIA     WETU.

-UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA                 BURE.

-IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA              MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



1 comments:

  • Unknown says:
    20 July 2017 at 02:45

    Ntakuona wapi nna masuala mengi ya ardhi ntahitaji msaada toka kwako, naona uko vizuri na unajitolea kuelimisha watu juu ya masuala ya ardhi

    0754/0786-594534

Post a Comment