Friday 6 February 2015

NJIA YA KISHERIA YA KUKUEPUSHA KUNUNUA ARDHI YENYE MGOGORO.







NA   BASHIR   YAKUB--

Makala zilizopita  nilieleza   mambo au taarifa muhimu  zinazopaswa kuwa kwenye  mkataba wako  unapokuwa unanunua  nyumba/kiwanja. Nikasema  katika niliyosema  kuwa mkataba  lazima uoneshe  ukitokea mgogoro  utatatuliwa vipi,  ueleze kuwa  utapotokea mgogoro  muuzaji  lazima  awajibike kuhakikisha anakupa ushirikiano  mnunuzi  ili kumaliza  mgogoro huo na kuwa muuzaji  kama ana  mke  basi  mke wake ni lazima  aandaiiwe  nyaraka iitwayo  ridhaa ya mwanandoa ambayo  ni  tofauti  na mkataba  na  aisaini  pamoja na kuweka picha yake.  Nilieleza  mengi  lakini hayo ni baadhi tu. Leo  tena naeleza hatua  muhimu sana au ya lazima  na lazima haswaa  kwa mnunuzi wa kiwanja/nyumba  ambayo anatakiwa  apitie  kabla ya kufanya manunuzi.Hatua hii kwa  jina la  kitaalam huitwa OFFICIAL  SEARCH  kwa lugha rahisi tu waweza kuiita  utafiti,upekuzi,  upembuzi au upelelezi rasmi  ambayo hufanywa na wanasheria. Mi napenda niite upelelezi.


(1)AINA ZA VIWANJA/NYUMBA UNAPOTAKA   KUFANYA  UPELELEZI  KUJUA   KAMA   KUNA  MGOGORO.

Nyumba/viwanja   tunavyouziana  kila siku  vimegawanyika  katika hadhi mbalimbali. Kwanza  kuna nyumba/viwanja  vyenye hati, vyenye leseni za makazi, vyenye ofa na ambavyo havina hati, leseni ya makazi wala ofa.Kutokana  na makuzi ya miji yetu  viwanja/nyumba zenye hati  mara nyingi huwa ni chache sana.Zenye leseni za makazi ni nyingi kiasi  na haya  ni maeneo ambayo  hasa hujulikana kama uswahilini. Zenye ofa  huwa  ni chache nazo  kwakuwa ofa ni hatua  anayopitia mtu anapoelekea  kupata hati au leseni ya makazi. Pia maeneo  ambayo hayana hati wala leseni ya makazi  wala ofa nayo ni mengi sana pia.  Kwa Dar es salaam  haya ni maeneo ya pembeni  pembeni  mwa mji Tegete,bunju, pugu, chanika, mbagala, baadhi ya maeneo  ya kigamboni n.k. Hata hivyo  eneo liwe na hati leseni ya makazi au hapana bado kisheria linatambulika .  

(2)NAMNA YA KUJUA KAMA  NYUMBA/KIWANJA   KINA  MGOGORO

Kama kiwanja/nyumba  ina hati  kuna maombi  rasmi ya kisheria ambayo huwa yanafanywa kwenda  ardhi  wizarani, wizara  ya ardhi makao makuu   kwa Dar es salaam na  kwa mikoani maombi  hayo  mara nyingi huenda makao makuu ya  mkoa ambapo   katika  maombi hayo  mnunuzi  anaiomba  mamlaka ya ardhi  imjulishe mambo yafuatayo;

( a ) KUJUA  JINA  LA  MMILIKI  HALALI  WA NYUMBA/KIWANJA.

Kwanza kujua  jina la mmiliki. Jina hili linatakiwa kufanana sawasawa  bila tofauti yoyote  na yule mtu anayetaka  kukuuzia eneo. Hii husaidia kuthibitisha  kuwa  anayeuza ndiye kweli mmiliki wa eneo.Kama majina yatatofautiana basi haraka sana  achana na hilo eneo ili kuepuka mgogoro.

( b ) KUJUA  KAMA  NYUMBA/KIWANJA  UNACHONUNUA  KIMEWEKWA   KAMA          DHAMANA  YA  MKOPO.

Kitu  kingine unachouliza kwenye hayo  maombi rasmi  ni  kama hiyo nyumba/kiwanja kimewekwa  kama dhamana kwa ajili ya  vitu kama mkopo . Wakati  mwingine  yawezekana mtu kukuuzia eneo ambalo  limewekwa  dhamana  kwa mkopo wa hela nyingi tu. Na kisheria kama eneo limewekwa dhamana yule anayelimiliki  kwa dhamana  ndiye mwenye nalo kwa muda huo  na wewe uliyenunua  sheria iko wazi unakuwa umeliwa.  Ieleweke kuwa ni vigumu sana kujua kama  eneo unalouziwa limewekwa  dhamana au hapana  ikiwa hukufanya  upelelezi huu. Wakati mwingine  mtu huweka dhamana eneo lake  na  kubaki na hati . Kwa hati ile  wewe mnunuzi  ni rahisi kuhadaika  kuwa eneo ni lake  lakini kumbe ni eneo lenye  deni kubwa. Ukinunua eneo kama hilo utakuwa umenunua mgogoro  mkubwa ambao  wewe mnunuzi kushindwa na kunyanganywa ulichonunua  ni lazima tu.

( c ) KUJUA    KAMA   KUNA   MGOGORO   WA  KIFAMILIA.

Kitu kingine ambacho utaomba kujua  katika yale  maombi  ni kama  kuna mgogoro  wowote  wa  kifamilia  kama migogoro ya mirathi, migogoro  ya kindoa ambapo mwanandoa mmoja anaweza kuwa ameweka  zuio  kuhusu uuzwaji wowote wa nyumba/kiwanja hicho. Usipofanya upelelezi huu utanunua halafu siku ya kubadilisha jina ndio siku utajua kuwa eneo lile lilikuwa haliruhusiwi kuuzwa.Aidha ifahamike kuwa mamlaka za ardhi hupata taarifa hizi za viwanja vya watu kupitia utaratibu wa mazuio uitwao CAVEAT.

( 3 ) MNUNUZI   WA  ENEO  LENYE  LESENI   YA  MAKAZ I  AKAFANYE  UPELELEZI  WAPI.

Maeneo yenye  leseni  za makazi  maombi haya ya  upelelezi wa kiwanja/nyumba  yanapelekwa  manispaa.  Manispaa inayohusika  ni ile ambayo lilipo eneo husika . Kwa  mfano  ukitaka kununua eneo kinondoni manispaa ya kinondoni  ndiyo inayopelekewa maombi,  kama eneo unalotaka kununua lipo temeke  basi  manispaa ya temeke  ndio  ipelekewe  maombi. Aidha kuhusu  mpangilio  wa maombi  na  kile unachotaka kujua kuhusu eneo  ni kama  nilivyoeleza hapo juu  kwenye  hati .

( 4 ) MAENEO   AMBAYO  HAYANA   HATI,  LESENI  ZA  MAKAZI  UPELELEZI  HUFANYIKAJE.

Kwakuwa maeneo ya namna hii yanakuwa  hayana  nyaraka  yoyote maalum katika mamlaka  za serikali  basi wakati mwngine  huleta ugumu   kidogo katika  kujua ukweli  ili kuepuka mgogoro.  Lakini kitu ambacho huwa tunashauri katika maeneo ya  hivi  ni kuwa kwanza  muuzaji akueleze eneo alilipataje. Kama alilinunua kwa mtu  ni vema akaonesha ule mkataba alionunulia  na kama mauzo yatafanyika  basi ni lazima mnunuzi apate kopi ya ule mkataba. Pili  kama amelirithi  ni lazima aoneshe  fomu ya usimamizi wa  mirathi ambayo  ndiyo itakuwa inampa mamlaka ya  kuuza. Na kama alipewa zawadi  basi aonesha  waraka wa zawadi ( deed  of gift)  ambao umesajiliwa.

Jingine  la msingi sana  katika  maeneo yasiyo  na hati wala leseni  za makazi  huwa  ni kuuliza majirani. Eneo unalonunua kama wapo majirani  hebu waulize  tu kwa nia njema na mara nyingi ukiwapata wawili  watatu hivi ni rahisi kupata  ukweli au  kukuwezesha kujenga  shaka. Na  majirani usiwaulize kwa pamoja, mtafute mmoja mmoja kila mtu kwa muda wake ili kuepusha kuoneana haya katika kusema ukweli. Pia  hakikisha  wakati wa kuwahoji majirani   muuzaji  asiwepo,  we tafuta tu muda wako  nenda peke yako  na pata taarifa. Uwepo wa muuzaji unaweza kuingilia (influence)  ukweli. Usikurupuke utalia, ni  hayo kwa leo.


MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.  PIA  NI MKURUGENZI  NA MWANZILISHI  WA  BLOG  HII  0784482959, 0714047241
bashiryakub@ymail.com





0 comments:

Post a Comment