Sunday 8 February 2015

JE UMECHUKUA MKOPO NA NYUMBA YAKO INATAKA KUUZWA, HAIRUHUSIWI KUUZWA MPAKA UTARATIBU HUU.




NA  BASHIR   YAKUB-

Wakopwaji/wadaiwa  wamekuwa  wakipata shida sana  kutoka  kwa wanaokopesha. Mkopesha awe ni mtu binafsi, taasisi ya fedha , kampuni  binafsi au mwingine  yeyote  wamekuwa  wakiwasumbua sana  wadeni  wao. Kubwa  zaidi hasa taasisi za fedha hutumia masharti ya mikataba ambayo  huwa yameandaliwa kitaalam kiasi cha  mtu ambaye  si mwanasheria  kutoelewa kwa undani maana  yake  kuwabana wadeni  ambao  hushtukia  masharti hayo baada  ya  kuwa wameshaanza  kudaiwa. Mbaya  zaidi  wamekuwa  wakifanya hivi bila kufuata taratibu za kisheria. Kwakuwa wamemsaidia  mtu kwa kumkopa   basi  wamekuwa  wakiichukulia  hali  hiyo kama  leseni ya  kufanya  lolote  ilimradi  tu  wanadeni  na wewe. Mali  za watu  huuzwa  hovyo  , wengine hufikishwa  mpaka   vituo  vya polisi  ilimradi  tu wakopeshaji   hupenda  kupindisha  utaratibu. Hapa  tutaeleza  baadhi  ya  mambo  kadhaa  ya msingi  ambayo  mkopeshaji  haruhusiwi kumfanyia  mdeni.

1.    WAKOPESHAJI  KUTOFUATA  TARATIBU  KATIKA UUZAJI  NYUMBA/KIWANJA   CHA  MDENI.

Sababu  kubwa  ambayo  imekuwa ikisababisha wakopeshaji  hasa  taasisi  za fedha kutofuata taratibu  wakati wa kuwadai  wadaiwa ambao wako  nje ya  mda kutokana  na  mikataba yao ya  mkopo  ni  kwasababu  wadaiwa wenyeywe  hawajui  haki  zao  za kisheria. Kama nilivosema hapo juu mikataba  ya kukopa  fedha iko kitaalam  sana  na  ni watu wachache wenye uwezo wa kugundua  utaalam ambao unapatikana katika  mikataba  ya  mikopo  wanayoichukua.  Mkopaji ana  haki  za msingi katika hatua tatu  muhimu  za mkopo wake. Kwanza  haki  wakati wa kuchukua  mkopo, haki wakati wa kurejesha mkopo, na  haki  wakati anaposhindwa  kurejesha  mkopo. Wakopaji wengi hawajui haki zao katika  hatua  hizi tatu muhimu. Hii ndio sababu hujikuta  wakilazimika kuzisujudia taasisi zilizowakopesha  zinapokuwa zikiwatisha.

2.      LAZIIMA  MKOPAJI  APEWE  TAARIFA YA MAANDISHI
     KABLA  YA  KUUZA  NYUMBA  YAKE.

Sheria  ya  Ardhi  ya 1999 kifungu cha 25( 1) kimeweka  bayana  kuwa  mkopeshaji hapaswi kuuza  nyumba ya  mdeni bila kumpa  taarifa  ya  mandishi(notice). Huwezi  kuamka asubuhi  unaanza kutangaza  mnada  wa  nyumba ya mtu. Haya  yamewakuta  wengi  mtu mali yake  inauzwa bila kupewa taarifa ya maandishi.  Wengine hupewa  taarifa ya  mdomo  kwa mfano mtu anapozuru  ofisi za taasisi iliyomkopesha maafisa wanamwambia  usipolipa  jumapili tunauza nyumba yako  halafu wanahesabu  eti hiyo  ni taarifa. Kwa  mujibu wa sheria hiyo sio taarifa  na huwezi  kuuza  nyumba  ya  mtu kwa taarifa  ya  namna  hiyo.

3.      KABLA  YA  KUPEWA NOTISI  YA  KUUZA  LAZIMA UWE   UMEPITA   MWEZI   MMOJA.

Hapo juu tumeona  kuwa  kabla nyumba  kuuzwa ni lazima  mdaiwa apewe notisi. Hata hivyo  ili  mdaiwa apewe  notisi  ni lazima uwe umepita mwezi mmoja  tangu aache kulipa kama  mkataba wake unavyosema. Hii ina maana  kuwa mdaiwa  hawezi  kuwa amepitisha mda wa malipo  kwa siku moja , wiki moja, wiki mbili au tatu halafu akaletewa notisi ya kutaka kuuzwa nyumba yake. Kwa mfano mdaiwa alitakiwa kurejesha tarehe 1 / 1 / 2015.  Tarehe 2, 3, 4 , 5  mpaka tarehe  30 hawezi kupewa notisi. Isipokuwa ni baada ya tarehe 30 ndipo anapoweza kupewa notisi.

4.       LAZIMA  IPITE  MIEZI  MIWILI  TANGU  SIKU  YA  NOTISI  MPAKA   KUUZA  NYUMBA   YA   MDENI.

Hapo juu tumeona kwamba  notisi inatolewa siku thelathini baada  ya kupitisha mda wa kurejesha. Lakini hapa kumbe tunaona kuwa  hata baada ya siku thelathini kupita na  mdeni ukapewa notisi  bado notisi  nayo ina mda wake ambao ni tofauti ni zile siku thelathini  za mwanzo. Hii ni kusema kuwa  huwezi kumpa  mdaiwa  notisi leo halafu  ukauza  nyumba yake kesho  au  ukampa  wiki hii halafu ukauza wiki ijayo.  Sheria  inasema  mkopeshaji anaweza kuuza nyumba ya  mdaiwa baada ya kupita  miezi miwili tangu siku ya  kupewa notisi ya kuuza.  Kwahiyo kama notisi ya kuuza imetolewa  mwezi wa kwanza  uuzaji utafanyika mwezi  wa tatu. Ina maana huu muda wote wa katikati  ni  nafasi  ya  mdaiwa kujipanga  kwa namna ya kulipa au kwenda mahakamani  kuzuia  nyumba isiuzwe. Ni  muda unaotoa  fursa  ya haki ya mdaiwa kujipanga  nini afanye. Sio kama ambavyo taasisi za fedha zimekuwa zikifanya, mtu anapewa  notisi  jumatatu  halafu anaambiwa nyumba  yake  inauzwa  jumapili.

5.        HUWEZI   KUUZA  NYUMBA YA MDAIWA  BILA KIBALI
      CHA  MAHAKAMA.

Taasisi  za mikopo zimekuwa  zikiuza nyumba za watu  mara tu muda wa notisi unapoisha. Hii hairuhusiwi  kisheria kwakuwa  muda  wa notisi ambao ni  miezi miwili unapoisha  mkopeshaji  lazima aende mahakamani afungue kesi  dhidi ya yule  anayemdai. Anayedaiwa naye ataitwa mahakamani ataambiwa shauri lake  atapewa nafasi ya kujitetea  na hukumu  ya kawaida kama  hukumu   katika  kesi  nyingine zilivyo  itatolewa. Katika hukumu hiyo  mkopeshaji  anaweza kushinda au kushindwa. Halikadhalika  mdaiwa anaweza kushinda au kushindwa. Mtoa mkopo  akishinda  basi ndipo atakapopewa  kibali  maalum cha kuuza kama  mahakama  itakuwa  imeona  hiyo ndio  suluhu. Kwa hiyo muhimu hapa ni kuwa nyumba yako haiwezi kuuzwa bila hicho  kibali cha mahakama. Suala  kwamba muda wa rejesho na notisi tayari umepita   halitoi  haki  ya moja kwa moja (automatic right)   ya kuuzwa kwa nyumba yako. 
6.       BAADA  YA MCHAKATO  HUU NDIPO NYUMBA  YA MDENI   YAWEZA   KUUZWA.

Kwanza  ni baada ya muda wa kulipa deni kumalizika na mdeni akapitisha siku thelathini.  Pili baada ya muda wa  notisi wa miezi miwili kuisha .  Na tatu baada ya  kesi kufunguliwa, kusikilizwa na kutolewa hukumu  ndipo  hatua  ya kuuza nyumba inapofikiwa. Hii  si  hatua nyepesi  na ya  haraka  kama ambavyo imekuwa  ikitekelezwa na tasisi za mikopo.  Ni mchakato  ambao una muda.

7. USHAURI  WA KITAALAM  KWA WAKOPAJI/WADAIWA.

Muda wa kufanya mambo kienyeji umekwisha. Kufanya mambo kienyeji ndiko kunakopelekea  haki zako kuminywa. Mkopaji/mdaiwa  hakikisha  unapata ushauri  wa  kisheria  katika hatua hizi, kwanza wakati ukitaka  kuchukua mkopo, pili wakati  wa kupitia mkataba wa mkopo ikiwezekana ule mkataba mwanasheria aupitie na akushauri kwasababu mikataba ya taasisi za mikopo ina mitego ambayo kwa mtu asiye na elimu ya sheria si rahisi kuigundua. Na tatu   pata ushauri wa kisheria mara  tu taasisi  ya  mkopo  inapoanza  kukusumbua  au  unapohisi  kuonewa. Kwa uzoefu wangu kwa kufuata ushauri huu nyumba nyingi zimeokolewa  mpaka sasa na haki  za   watu  zimepatikana.

8. UNAWEZA  KURUDISHA  NYUMBA  YAKO   IWAPO 
    ILIUZWA   BILA   KUFUATA   UTARATIBU  NILIOELEZA.

Utaratibu  wa kisheria unapofuatwa ndipo jambo fulani  huwa halali  na unapokiukwa  jambo hilo huwa batili kuanzia hapo( ab initio). Hii ni kusema kuanzia hapo( ab initio). Iwapo nyumba yako iliuzwa bila kufuatwa  kwa baadhi  ya taratibu nilizoorodhesha hapa  hata kama ilikiukwa moja tu bado waweza  kuirudisha nyumba yako kwakuwa  uuzwaji ule ulikuwa haramu na aliyenunua alinunua  kitu haramu. Hili wala si la ajabu isipokuwa ndivyo sheria ilivyo.  Na wala mtu asihisi kuwa amechelewa kwakuwa masuala yanayohusu  ardhi  sheria imetoa kipindi cha zaidi ya miaka kumi tangu kuonewa  hadi kufungua shauri. Na  hii  haijalishi nyumba yako iliuzwa kwa nani  na sasa amefanya maendelezo gani.
Yapo mengi kuhusu haki za  mkopaji  yaliyo  katika sheria Na. 4 & 5 ya 1999 lakini leo tuanze na haya.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.  PIA  NI  MMOJA  WA WANASHERIA  WAANZILISHI   WA  BLOGI  HII  0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com


1 comments:

  • Nsolo S. Stephen says:
    9 February 2015 at 14:26

    Maelekezo haya ni muhimu na yakufaa sana kwa wanaojali.

Post a Comment