Monday 23 February 2015

NAMNA YA KUMDAI FIDIA ALIYEVUNJA MKATABA AU KUKIUKA MAKUBALIANO YENU.


 Image result for PESA


NA  BASHIR  YAKUB-

Kawaida unapokuwa umeingia katika mkataba au makubaliano katika jambo lolote lile kunakuwa na masharti ambayo unapaswa kuyatimiza au kutimiziwa. Na hapa nazungumzia mikataba yote uwe wa kuuza mbuzi au ule wa kujenga ghorofa mia, yote ni mikataba. Masharti hayo huwa ndio makubaliano yenyewe au twaweza kusema kuwa ndio mkataba wenyewe. Kila upande unawajibika  juu ya utekelezaji wa masharti hayo. Yeyote anayefikia hatua ya kukiuka masharti hayo  au hata kukiuka sharti moja tu, hana namna ila kukubaliana na  hatua na utaratibu wa kisheria kuhusu  uvunjwaji au ukiukwaji wa mikataba.

1.KUKIUKA  MKATABA   AU   MAKUBALIANO.

Uvunjaji wa mkataba unaweza kutokea katika njia nyingi. Moja ni ile ya kawaida ambapo mtu huamua kujitoa  kwa kusema,kutamka au kuandika kuwa sasa sitafanya hili na lile hata kama lipo katika makubaliano yetu.  Pili njia nyingine  ya kuvunja mkataba ni pale ambapo mtu hasemi kwa kutamka kwamba sasa sitafanya hili wala lile isipokuwa hatimiza wala hatekelezi kile mlichokubaliana. Ifahamike kuwa mtu anapoingia mkataba na mtu mwingine  au kampuni na kampuni  au kampuni na mtu sheria inalazimisha kutekeleza kwa usahihi yale yote yaliyokubaliwa  katika mkataba huo. Utekelezaji wa baadhi ya masharti na kuacha mengine au kutotekeleza yote kabisa ni uvunjaji au ni kujitoa katilka mkataba kwa mujibu wa sheria. Aidha nasisitiza kuwa ili mtu ajitoe katika mkataba sio lazima aseme kuwa nimejitoa katika mkataba. Kitendo cha kutofuata makubaliano  kama yalivyokubaliwa  ni kujitoa katika mkataba moja kwa moja.

2.KUMDAI  FIDIA    ALIYEKIUKA  MKATABA  AU  MAKUBALIANO. 

Si  vyema  mtu akafanya  makubaliano  na mtu mwingine  halafu  akapotea  bila  kutekeleza  kile  kilichokubaliwa. Ni  sababu  hii inayonifanya kuwaambia  watu  kuwadai  fidia  wale  wanaokiuka  masharti. Kudai kulipwa  fidia  baada ya  kuvunjwa  mkataba  ni takwa la  kisheria  na  hivyo  si  ukorofi  kama ambavyo  mtu anaweza kufikiri.

3.AINA  ZA FIDIA  UNAZOWEZA  KUDAI  UKIVUNJIWA  MKATABA.

( a ) Fidia zipo za aina nyingi.  Kwanza kuna fidia ambayo utatakiwa kulipa kutokana na makubaliano yenu ya awali wakati mnaingia mkataba. Hii ni aina ya fidia ambayo wahusilka katika mkataba hukubaliana  awali kabisa wakati wanaingia katika mkataba  ambapo hupanga kiasi cha fidia ambacho watalipana iwapo mmoja kati yao atakiuka au kujitoa katika mkataba. Kwa kuwa fidia hii huwa  imeandikwa na ipo ndani ya mkataba basi aliyekiuka au kujitoa katika mkataba hutakiwa kulipa fidia hiyo  kulingana na makubaliano yao mara moja.

( b ) Fidia  nyingine ni ile ambayo mtu hutakiwa kulipa iwapo wakati wanaingia mkataba hakuna fidia yoyote waliyokuwa wamekubaliana kulipa iwapo mmoja wao atakwenda kinyume.  Hii ni aina ya fidia inayotathminiwa na mahakama.  Mahakama hutathmini fidia hii kwa kuangalia mambo mawili yaani  kiwango cha ukiukwaji wa mkataba na hasara  zilizotokana na ukiukwaji huo. Kupitia hayo mahakama huweza  kutangaza kiwango cha fidia anachotakiwa kulipwa mtu ambaye amevunjiwa mkataba.

4. FIDIA  NYINGINEZO.

( a ) Aina  nyingine ya fidia inayoweza kuombwa mahakamani baada ya mkataba kuvunjwa ni  ile fidia ambayo itamweka mtu aliyevunjiwa mkataba katika nafasi fulani ambayo angekuwepo  iwapo mkataba ule ungefanyika. Mfano uliingia mkataba fulani na mtu au kampuni na iwapo mkataba ule ungetekelezwa kwa ukamilifu ulipaswa kupata faida ya shilingi milioni mia moja. Kutokana na hilo unaweza kuiomba mahakama ili ulipwe kiasi cha pesa hizo kama faida ambayo ulitakiwa kupata iwapo mkataba usingevunjwa.

( b ) Pia fidia  nyingine anayoweza kudai mtu ni  ile ya kutaka alipwe kutokana ma kiwango cha kazi iliyokuwa imefanyika tu na si vinginevyo. Mfano  umeingia mkataba wa kumpelekea mtu  gunia mia za mchele. Wakati umefikisha gunia khamsini mkataba unavunjwa na unaambiwa usilete nyingine. Kwa maana hii utakapokwenda mahakamani kuomba fidia unaweza kuomba  mahakama itathimini fidia kutokana na mkataba mzima yaani gunia mia au unaweza kuomba fidia itathminiwe kutokana na gunia khamsini  tu yaani  fidia kutokana na kazi ambayo ilikwisha fanyika tu.

5.KAMA UMEVUNJIWA MKATABA NA HUTAKI FIDIA WAWEZA PIA KUOMBA HAYA .

Yatupasa pia kujua kuwa sio lazima kila mkataba unapovunjwa uombe fidia. Yapo mambo mengine ambayo unaweza kufanya  kama tutakavyoona hapa.

( a ) Kwanza unaweza kwenda mahakamani kuomba  lifanyike lile lililokuwa linapaswa kufanyika  ndani ya mkataba, Mfano  uliingia mkataba  wa kuletewa vitabu miambili  ambapo vimeletwa  mia tu na vingine havikuletwa. Unaweza kwenda mahakamani ukiomba  mahakama kumlazimisha mhusika kumalizia vile vitabu mia ambavyo alikuwa hajamlizia na si vinginevyo.  Au ulimlipa hela katika tenda ya kukujengea nyumba ambapo alijenga kidogo  na hakumalizia. Unaweza kwenda mahakamani ukiiomba mahakama itoe agizo la kumtaka mhusika amalizie ile sehemu iliyobaki na si vinginevyo. Hii sio fidia na ni tofauti kabisa na fidia.

( b ) Kitu kingine ambacho unaweza kukiomba mahakamani baada ya mtu kuwa amekiuka au  amevunja mkataba ni kuiomba mahakama itoe agizo  la kurejeshwa katika hali yako ya kawaida kama ulivyokuwa kabla  ya mkataba, Mfano kama mkataba ulikuwa wa  kujenga na kumaliza nyumba  utaomba urejeshewe hela yako  na ikiwezekana  eneo lile lisafishwe kwa  kuvunja  yale yote aliyokwisha jenga ili eneo libaki kama lilivyokuwa awali kabla ya mkataba. Hii nayo sio fidia na ni tofauti kabisa na fidia.

( c ) Kitu kingine ambacho unaweza kuomba uwapo mahakamani baada ya kuvunjwa au kukiukwa kwa  mkataba ni kuzuia kuendelea kwa utekelezaji wa mkataba, Mfano uliingia mkataba  na mtu au kampuni ikujengee nyumba au barabara ndani ya muda fulani. Lakini kutokana na makubaliano yenu ujenzi ule unasuasua kiasi kwamba hauendi kama mlivyopanga. Kwa hali hii unaweza kuiomba mahakama  isitishe utekelezaji wa mkataba  kwasababu ya kutoridhika na utekelzaji wa masharti. Halikadhalika hii nayo sio fidia na ni tofauti  kabisa na fidia.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO. PIA NI KATI  YA WANASHERIA WAANZILISHI  WA BLOG HII.   0784482959, 0714047241
bashiryakub@ymail.com


TANGAZO   MUHIMU

VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.

-WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA                    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.

-UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA   WANASHERIA     WETU.

-UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA                 BURE.

-IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA              MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0783851726.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.





0 comments:

Post a Comment