Tuesday 10 February 2015

JE HAURIDHISHWI NA MSIMAMIZI WENU WA MIRATHI, HII NI NJIA YA KUMUONDOA.


NA  BASHIR  YAKUB-

Wapo  watu ambao  baada  ya  kupata  cheo au  nafasi  ya  kuwa wasimamizi wa mirathi  hugeuka  waungu.  Huwa hawaambiwi  wala  hawasikii  la  mtu. Huwezi kuamini  kuwa  kuna baadhi ya wasimamizi wa  mirathi  wamekataa  kugawa  mali  za marehemu  sasa ni zaidi ya miaka   kumi. Na si kwamba wamefanya  hivyo  kwa maslahi mapana  ya familia, hapana. Wamefanya  hivyo kwa ukorofi  lakini kubwa zaidi  wanafanya  hivyo  ili waendelee  kunufaika na  mali za marehemu  peke  yao. Mambo hayo  yameleta  sana  faraka  kwenye familia.

Warithi  na  wote  wenye haki katika  mali  za marehemu wengi wao huchukizwa  na  matendo  haya  yumkini wapo  ambao  hujua  la kufanya  na wapo ambao  hubaki  njia  panda wasijue la  kufanya.  Mali zinaliwa  lakini   warithi  wafanye nini, hawaoni njia.  Katika makala haya  nini  mfanye iwapo hamridhishwi au hamumtaki kabisa msimamizi wenu  wa mirathi ni kati  ya mambo  yatakayoguswa.

1.             MSIMAMIZI  WA  MIRATHI  NI  NANI.

Msimamizi  wa  mirathi ni  mwakilishi halali wa kisheria wa mambo yote ya marehemu na mali  zote  za  marehemu   ambazo  huwa  chini yake. Neno mwakilishi katika  maana hii linamaanishi uwakilishi  kama uwakilishi  tunaoujua. Uwakilishi  sio umiliki. Hivyo  msimamizi  wa mirathi  ni  mwakilishi .  Msimamizi  wa  mirathi  hupatikana  kwa  njia  mbili kwanza  huteuliwa  na marehemu  mwenyewe kupitia  wosia na  pili  huweza kuteuliwa  na wana familia  ikiwa marehemu  hakuacha wosia  au aliacha wosia  lakini wosia  wenyewe hauoneshi  kwa  namna  yoyote ile nani  awe  msimamizi  wa  mirathi.

2.         AINA  ZA WASIMAMIZI  WA  MIRATHI.

Wafuatao  wanaweza  kuwa wasimamizi  wa mirathi:
Kwanza   ndugu wa marehemu na wale wenye maslahi na mirathi ya marehemu. Hawa wanaweza  kuwa ni watoto, wazazi, wajukuu, kaka  au dada  wa marehemu na  ndugu  au  wasio  ndugu  kutegemeana  na  nani alikuwa  hai wakati  wa kifo cha  marehemu au  wakati  mirathi  inachakatwa.

Pili, kabidhi wasii mkuu  anaweza  kuwa  msimamizi  wa  mirathi  ya  marehemu. Kabidhi  wasii ni ofisi ya serikali ambayo hujihusisha pamoja na mambo mengine,usimamizi wa mirathi,endapo itaombwa na mtu yeyote lakini  mwenye  maslahi katika  mali za marehemu  au  marehemu mwenyewe wakati wa uhai wake.

Tatu, mwakilishi wa kisheria wa mtu aliyetajwa kama msimamizi wa mirathi (mtu aliyepewa power of attorney).  Mtu aliyeteuliwa  kuwa msimamizi  wa mirathi  naye  anaweza kumpa mtu  mwingie  kitu kiitwacho  nguvu  za kisheria (power  of attorneys)  ambapo kupitia  kitu hicho  yule aliyepewa atakuwa  na mamlaka sawa na  yule msimamizi  wa mirathi. Lakini hii ni katika mazingira  malum  ya kisheria. Aidha huyu aliyepewa  naye ataitwa  msimamizi  wa  mirathi. Wapo wengine hao  ni baadhi tu.

3. JINSI YA KUMUONDOA  MSIMAMIZI  WA  MIRATHI            MKOROFI.

Zipo  njia  mbili  za  kulitekeleza hili.
( a ) Kumtaka ajiondoe  mwenyewe. Haki  hii anayo mtu yeyote mwenye maslahi na mirathi ya marehemu. Nimesema hapo juu kuwa   wenye  maslahi  wanaweza kuwa watoto, wazazi, ndugu, jamaa, wajukuu kutegemea na nani yupo hai. Hawa wote wana  haki ya kumtaka  msimamizi ajiondoe  katika usimamizi. Haijalishi  aliteuliwa na marehemu au wanafamilia.  Watu  wengi hujua  msimamizi  wa  mirathi ambaye ametajwa  katika wosia  na marehemu hawezi kuondolewa . Hili si kweli  hata kama  aliteuliwa  na marehemu  akifanya  mambo  nitakayotaja  hapa  baadae  kuondoka  kwake  si kwa hiyari.

( b ) Njia  ya  pili  ya  kumuondoa  msimamizi  wa mrathi  ni njia  ya mahakama. Hii  mara nyingi hutumika iwapo ile  ya  kwanza ya kujiondoa  kwa hiyari  inaposhindikana. Njia hii hufika  mahakamani  kwa njia  ya pingamizi.  Aidha mtu yeyote ambaye anaona  ana haki au ana maslahi na mirathi ya marehemu anaweza kuweka pingamizi mahakamani dhidi ya msimamizi  wa mirathi ikiwa  kama  njia  ya kumkataa   na  kama  mahakama  itaridhika  basi ataondolewa mara   moja.

4.HIZI  NI SABABU ZA KISHERIA ZA KUMUONDOA  MSIMAMIZI WA  MIRATHI .

( a ) Ikiwa  kuteuliwa kwake  kulikuwa kwa mashaka  labda  kikao cha  familia  kilichomteua  hakikuwa chenye  kueleweka pengine kilifanywa kwa siri   na wanafamilia  wengine au warithi walipigwa chenga  na hivyo hawakuhdhuria. Hii itakuwa ni  sababu ya kumuondoa. Pia kasoro yoyote katika mchakato wa  kupatikana kwa msimamizi  wa mirathi  ni sababu inayoweza kumuondoa.

( b ) Ikiwa  msimamizi  wa  mirathi atatumia  vibaya  mali  za marehemu  itakuwa  ni sababu  ya  kumuondoa. Hili linaeleweka.

( c ) Ikiwa  msimamizi  wa mirathi  anatumia  mali  za marehemu kujinufaisha kwa  mfano anazifanyia  biashara ambayo yeye  ndio  mpata faida  ni sababu  ya  kumuondoa.

( d ) Ikiwa anasababisha uharibifu wa aina yoyote  katika  mali za marehemu  ni sababu  ya  kumuondoa.

( e ) Ikiwa msimamizi wa mirathi kwa makusudi ameshindwa kuleta orodha ya mali za marehemu na taarifa  ya jinsi alivyozishughulikia. Wapo wasimamizi ambao hupenda kuwa wasiri  wakati  wa kushughulikia mali za marehemu. Hili si sawa lazima wenye maslahi wapate taarifa  za mara  kwa mara  za namna msimamizi anavyoshughulikia  mali za marehemu  laa sivyo wamwondoe kwasababu hiyo.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA JUMATANO.  PIA  NI KATI   YA  WANASHERIA  WAANZILISHI  WA  BLOG  HII.
0784482959,  0714047241              bashiryakub@ymail.com











0 comments:

Post a Comment