Tuesday 24 November 2015

HAYA YATAKUSAIDIA UWAPO MIKONONI MWA POLISI.

Image result for AKAMATWA NA POLISI

NA  BASHIR  YAKUB -

1.JE  KITU  GANI  KIFANYKE  ASKARI  ANAPOKUNYIMA  DHAMANA.

Kwanza  ieleweke  kuwa  dhamana  ni  haki  yako. Haki  ni  jambo  la  lazima.  Haki  ya  dhamana  inaruhusiwa  kunyimwa  katika  makosa  machache  sana kwa  mfano  uhaini, wizi  wa  silaha,  mauaji n.k.  Makosa  mengine  madogo madogo hasa  haya  ya kila  siku  ya  kutukana,  kudhalilisha, kupigana,  ajali ndogo, wizi  usio  wa  silaha, na  mengine   dhamana  ni  lazima.  Hata  hivyo  makosa ambayo  hayaruhusiuwi  kwa  dhamana   ni  lazima  askari  anapokunyima  dhamana  aandike  sababu  za  kukunyima  dhamana. 

Na  hapohapo  yatakiwa  ahakikishe  anakufikisha  mahakamani  haraka  sana  iwezekanavyo  hasa  ndani  ya  saa  24  ili  mahakama  ikatizame  shauri  lako   na  haki  unazostahili.  Ni makosa  makubwa  askari  kumnyima  raia  dhamana   pale  anapostahili  na  ni  makosa  makubwa  askari  kutomfikisha  mtuhumiwa  mahakamani  haraka  bila  sababu  za  msingi.  Unayo  haki  ya  kumtaka  askari   akufikishe  mbele  ya  hakimu/jaji   haraka  ili  ukaombe  dhamana  huko na  haki  zako  nyingine.  Katika  hili hautaomba  ila   utamtaka  askari kufanya  hivyo.

2. JE  DHAMANA  NI  LAZIMA  UWEKE(DEPOSIT) YA KIASI  CHA  FEDHA.

Hapana  dhamana   si  lazima  uache  pesa. Unaweza  ukapewa  dhamana  kwa  ahadi  ya  maandishi  tu.  Ahadi  ya  maandishi   ni  masharti  ambayo  utayasaini   na  kuahidi  kuyatekeleza  utapokuwa  umeachiwa  kwa  dhamana.  Moja  ya  masharti  hayo   ni  kuahidi  kufika  tena  kituo  cha  polisi  au  mahakamani  katika  muda  utakaopangwa.  Dhamana ya  kuweka  kiasi  cha  fedha  huwa inaamriwa   iwapo  kuna  makosa  makubwa  yaliyotendeka.  Hata  hivyo  fedha  hizo  hutakiwa  kurudishwa  ama  baada  ya  upelelezi  kukamilika  na  kuonekana  mtuhumiwa  hana  kosa au  baada  ya  kuwa  huru  kutokana  na  amri  ya  mahakama.

3 JE  INARUHUSIWA  KUMKAMATA  MWINGINE BAADA  YA  KUMKOSA  MTUHUMIWA  HALISI.

Ni  kosa  kubwa  askari  kumkamata  mtu  mwingine  baada  ya  kumkosa  mtuhumiwa.   Mara  kadhaa hutokea  askari  kuondoka  na  ndugu , mtoto  au  mke  wa  mtuhumiwa  baada  ya  kumkosa  mtuhumiwa  nyumbani.  Hii  hairuhusiwi  kabisa. Sheria  iko  wazi  kuwa  aliyetenda  kosa  ndiye anayewajibika  kwakosa.  Kama  hayupo  na  hawezi kupatikana  hilo  haliwahusu  ndugu, watoto,  mke  au  mme  wa  mtuhumiwa. Kosa  ni  kwa  aliyetenda kosa   basi  na  si  vinginevyo.

4. KUWEZESHWA  KUWATAARIFU  NDUGU  UNAPOKAMATWA.

Inapotokea  umekamatwa  bila ndugu  zako  kuwa  na  taarifa  na  ukawa  unashikiliwa  kituo  cha  polisi  basi  unayo  haki  ya  kuwezeshwa  na  askari  waliokukamata  kuwataarifu  ndugu,  jamaa  na  mwanasheria   iwapo  unaye  ili  waweze  kufika  kituoni  kwa  hatua . Kama  huna  mawasiliano  ya  simu  ni  wajibu  wa  askari  waliokushikilia  kukuwezesha  kupata  mawasiliano  hayo  ili  uwasiliane  na  ndugu  hao.

5. JE  INARUHUSIWA  KUKAMATWA  BILA  KUAMBIWA  SABABU.

Hapana hairuhusiwi. Unapokamatwa  ni  lazima  kuambiwa   sababu  za  kukamatwa  huko. Ikiwa  umekamatwa  katika  mazingira  ambayo  sio ya  vurugu   basi  inatakiwa  kabla  hujakamatwa  askari  ajitambulishe  na  akwambie  kuwa  anatakiwa  kukukamata  kwasababu  hii  na  hii. Ikiwa  katika  mazingira  ya vurugu  kwa  mfano  ulikuwa  unagombana, kwenye  maandamano  haramu ,  mapambano  ya  askari  na  wafanya  fujo  basi  sababu  ya  kukamatwa  utaambiwa  baada  ya  kuwa  umekamatwa  na  sio  kabla.

6. JE  UFANYE  NINI  IWAPO  UMETOA LALAMIKO  NA  ASKARI  WAMELIPUUZA.

Wapo  baadhi  ya watu  wametoa malalamiko  ya msingi   kuhusu  kuonewa  au  kutendewa  jinai  lakini  askari  polisi  wamekataa  kusajili  malalamiko  hayo  wala  kufungua  kesi. Hii  inaweza  kuwa  imesababishwa  na  uzembe  au  rushwa  aliyotoa  mtenda  kosa  ili  asifunguliwe  mashitaka. Ikiwa  litakutokea  hilo  basi  waweza  kutoa  taarifa   kwa  askari  wa  cheo  cha  juu  zaidi  ya  yule  uliyeripoti  kwake  na  hasa  mkuu  wa  kituo. Ikiwa  na  huko  hakuna  msaada  basi  waweza  kutoa  taarifa   kwa  hakimu  wa  mahakama  iliyo  karibu ambaye  atatoa  amri  ya  kusajiliwa  shitaka  hilo. 
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA  KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                  WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA HARAKA  BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



0 comments:

Post a Comment