Tuesday 15 September 2015

JITAMBUE KISHERIA UNAPOFUKUZWA KAZI KWA MAKOSA YA KINIDHAMU.


Image result for JENGO  LA  WIZARA  YA  KAZI

NA  BASHIR  YAKUB -

Kisheria  yapo  mambo  mengi  ambayo  huweza  kubatilisha  mkataba  wa  ajira  kati  ya  mwajiri  na  mwajiriwa. Mkataba  wa  ajira  sawa  na  mikataba  mingine  yote huzaliwa,  huishi  na  hufa. Huzaliwa  pale  tu  unaposainiwa ,  huishi  pale  unapoanza  kutekelezwa  na  hufa   pale  yanapojitokeza  baadhi  ya  mambo  ambayo  yameainishwa  na  sheria  kama  mambo  yanayoua mkataba  wa  ajira. Aidha zipo  taratibu  maalum  za  kumaliza/kuua  mkataba  wa  ajira  na  hii  ni  katika  mazingira  yote,  yaani mazingira  ya kumaliza  mkataba  kwa  hiari  na yale  ya kumaliza  kwa  kulazimika  kutokana  na  sababu  mbalimbali. Kumaliza  mkataba  wa  ajira  kwa  hiari  kumekuwa  hakuleti  shida  sana  kama  ilivyo  kumaliza  mkataba  wa  ajira  kwa kulazimika hasa  linapokuja suala la sababu   za  kinidhamu  kama  tutakavyoona.

1.KUACHISHWA  KAZI  KWASABABU  ZA  KINIDHAMU.

Ni  kweli  sababu  za  kinidhamu   ni  sababu  za  msingi  zinazoweza  kumpelekea  mwajiriwa  kupoteza  ajira  yake. Hata  hivyo   sababu  hizi  zimekuwa  zikitumiwa  vibaya  na  waajiri. Zimekuwa  zikitumika  kama  sehemu ya   kuoneshana  uwezo  kati  ya  mtu  na  bosi  wake,kukomoana, hila,  pia  zimekuwa  zikitumika  kama  sehemu  ya  kulipiziana  visasi   na  wakati  mwingine  hutumika  kumwondoa  mfanyakazi  mmoja  ili  mwingine  apate  kuajiriwa. Haya  ni  makosa  makubwa  kwa  mujibu  wa  sura  ya  366  Sheria  ya  ajira 2004. Ikumbukwe sheria  inaposema  ni  halali  kumfukuza  mwajiriwa  kwa  sababu za  kinidhamu  haimaanishi  kuwa   mwajiri  amtafutie  mwajiriwa   kisa.  Lazima  sababu  hizo  ziwe  zimejitokeza  kweli  na  ziweze  kuthibitishwa.  Isiwe  habari  ya  nilisikia au  nahisi  au  tuhuma  tu  zisizo  na  mashiko.

2.  HAIRUHUSIWI  KUMFUKUZA  MWAJIRIWA  MARAMOJA.

Kwa  lugha  ya  kitaalam  kufukuzwa  mara  moja  huitwa  “summary  dismissal”. Hii  ni  hatua  ambapo  mwajiriwa  anaweza  kufika  kazini  leo  na  kuambiwa  hamna  kazi  kwasababu  hizi  na  hizi  na  hivyo rudi  nyumbani na  kuanzia  leo  usije tena  hapa.  Kufukuzwa  kwa  mtindo  huu  humfanya  mwajiriwa  kupoteza  haki  zake  ikiwemo  kiinua  mgongo  ikiwa  ni  pamoja  na  kutopewa  taarifa( notice)  ya  kisheria.  Hata  hivyo ni muhimu  sana  kueleweka  kuwa ufukuzaji  wa  namna  hii  kwasasa hauruhusiwi  hasa  baada  ya  sheria  ya  ajira  kufanyiwa  marekebisho  mwaka  2004  na  2009. Hapo  nyuma  wapo wengi  wamefukuzwa  kwa  mtindo  huu  lakini  kwasasa  kwakuwa kitu  hiki   hakipatikani  tena   katika  sheria  hii  maana  yake   ni  kwamba  hakiruhusiwi.  Kwahiyo  twaweza  kusema  kuwa ni  makosa  kwa  mwajiri  kumfukuza  mwajiriwa  kwa  mtindo  wa  mara  moja “summary  dismissal”. Hii  ni  hata  kama mwajiriwa   alitenda  kosa  kubwa  la  kinidhamu bado utaratibu  huu  hautaruhusiwa.

3. KULIPWA  MSHAHARA  BAADA  YA  KUFUKUZWA  KAZI  KWASABABU  ZA  KINIDHAMU.

Katika  haki  alizonazo  mwajiriwa  aliyefukuzwa  kazi  kwasababu  za  kinidhamu  ni  pamoja  na  kulipwa  mshahara  wake  au  ujira  kisheria.  Hii  ni  kutokana  na  kifungu  cha 44 sheria  namba  6  ya  ajira  na  mahusiano  kazini.  Kwa  mujibu  wa  kifungu  hiki  mshahara  hulipwa  kwa  kuhesabu  kuanzia   tarehe  ya  mshahara  wa mwisho  mpaka  siku  aliyofukuzwa  kazi  mwajiriwa.  Hii  ina  maana  ikiwa  tarehe  ya mwisho  ya  kupokea  mshahara  ilikuwa tarehe 31  January 2015 halafu  ukafukuzwa  tarehe  21 february 2015  basi  utatakiwa  kulipwa kiwango  cha  pesa  kinacholingana  na  hizo  siku  ulizofanya  kazi  yaani  siku  21  kuanzia  tarehe  1  hadi  tarehe  21. Hii  ni  haki  ya  msingi.

4. LAZIMA  KUPEWA  NAFASI  YA  KUJITETEA  JAPO  KOSA  NI  LA  KINIDHAMU.

Haki  ya kusikilizwa  ni  haki  ya  asili. Ni  haki  ambayo  haiwezi  kuondolewa  na mtu. kampuni  au  taasisi  yoyote. Kwa maana  hii  hata  kosa  la  mwajiriwa  liwe  kubwa  kwa  kiwango  gani  ni  lazima  apewe  nafasi  asikilizwe  na  ajitetee  kwanini  asichukuliwe hatua.  Hii  ni  kwa  mujibu  wa  kanuni  ya  13 ( 3 ) ya  sheria  ya ajira  na  mahusiano  kazini.  Ni  makosa  kumfukuza  mwajiriwa  bila kumpa  nafasi  ya  kusikilizwa  na  kujitetea.  Kusikilizwa  ni  lazima  kuwe kule  kulikotekelezwa  na  mamlaka  husika  za ofisi ya mwajiriwa  kwa  mfano  bodi,  kamati  n.k.
Nataka  nisisitize  hapa  kuwa  ukubwa  wa  kosa  kwa  namna  yoyote  ile  hakuathiri  au  hakuingilii  haki  za  mwajiriwa. Haki  zote  zikiwemo  hizi  nilizotaja hapa  ni  lazima  apatiwe  mwajiriwa bila  kujali  ametenda  kosa  kubwa  kiasi  gani.  Sio  hiari  ya  mwajiri  kumpatia  mwajiriwa  haki  hizi.  Hii  ni kwasababu  haki  hizi  zipo  kisheria  na  kutekelezwa  kwake  ni  wajibu.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com

                                           TANGAZO   MUHIMU                                                
VIWANJA     NA     NYUMBA          ZINAUZWA.
·        
WANASHERIA   WETU   WATAKUANDALIA   MIKATABA  YOTE  BURE  NA    KUKUSIMAMIA  MPAKA   MANUNUZI    YAKAMILIKE   BURE.
·        
UHALALI   WA  NYARAKA   NA   UMILIKI   UMETHIBITISHWA  NA                        WANASHERIA  WETU.
·        
UTAPEWA  MTU  WA  KUKUSAIDIA  KUFANYA  TRANSFER   KWA  HARAKA         BURE.
·        
IKIWA   UTATOKEA   MGOGORO  NDANI   YA  MWAKA  TANGU  TAREHE  YA       MANUNUZI    UTAPEWA   WAKILI   WA   KUSIMAMIA  MGOGORO    BURE
                                                        0784482959.

 KUONA   BOFYA  HAPO  JUU    MWANZO  WA   BLOG.



0 comments:

Post a Comment