Monday 16 February 2015

KISHERIA MAMA WA NYUMBANI ANASTAHILI MGAO WA MALI NDOA INAPOVUNJIKA.

Image result for WAGOMBEA MTOTO
NA  BASHIR  YAKUB-

Ndoa inapovunjika kuna kuna mambo makuu matatu ambayo hutokea yakiwa kama matokeo ya ndoa hiyo kuvunjika. Kwanza ni  kugawana mali walizochuma  wanandoa , pili hifadhi ya watoto  na tatu matunzo ya watoto. Haya  ni matokeo  ya kuvunjika  kwa ndoa, mengine zaidi kuhusu  kuvunjika kwa ndoa tutayaona hapa wakati nikieleza mgawanyo wa mali  za wanandoa.

1.MALI   ZIPI  HUTAKIWA  HUGAWANYWA NDOA  INAPOVUNJIKA.

Ndoa inapotangazwa kuvunjika mali ambazo hupaswa kugawanywa ni mali za wanandoa wenyewe. Swali mbele yetu ni kuwa ni zipi mali za wanandoa. Mali za wanandoa ni zile mali zote zilizochumwa na wanandoa hao kwa jitihada  au  juhudi  za  pamoja  wakati  wa  ndoa  yao. Mali hizo zaweza kuwa  zinahamishika au hazihamishiki. Mali zisozo hamishika ni kama nyumba, viwanja, mashamba n.k. Mali zinazohamishika ni kama magari,  baiskeli, pikipiki,vifaa vya ndani kama fenicha, fedha benki,  na mali nyingine ambazo hazionekani kwa macho au hazigusiki kama hisa  n.k. Zingatia  sana usije kudhulumiwa kwa  kuwa hata hisa pamoja na akiba ya fedha benki nayo ni mali inayostahili kugawanywa.

2. JE MALI ILIYOPATIKANA KABLA YA NDOA  HUGAWANYWA.

Mali zilizopatikana kabla ya ndoa haziwezi kugawanywa  ndoa inapovunjika  isipokuwa tu  kama zilibadilishwa  kuwa za wanandoa  wakati wa ndoa. Swali ni zinawezaje  kubadilishwa  kuwa za wanandoa. Zinabadilshwa kuwa za wanandoa  iwapo wanandoa walikubaliana kwa makubaliano maalum kuwa mali kadha wa kadha zitakuwa zetu wote. Na hii inaweza  kuwa kwa maandishi  au  kwa kubadili majina  ya nyaraka  za umiliki  na kuzifanya kuwa na  majina yote mawili  ya wanandoa kutoka  la mmoja  la awali. Lakini  pia zaweza kuwa  za kwao wote kimatendo, kwa mfano kabla ya ndoa mmoja wa wanandoa alikuwa na nyumba lakini haijamaliziwa.

Wakati wa ndoa  nyumba hiyo imemaliziwa kwa nguvu zao za pamoja  na sasa imekamiliki. Nyumba ile inageuka kuwa ya wote. Kwa ufupi  maendelezo yoyote yanayofanywa na wanandoa  katika  mali  ambayo hapo awali kabla ya ndoa ilimilikiwa na  mmoja peke yake  yanaibadilisha  mali ile kuwa  ya ndoa. Hata  kupaka rangi  ni tendo la kuifanya mali kumilikiwa kwa pamoja  na hivyo kustahili mgao  ndoa  inapovunjika.

3. MAMA  WA NYUMBANI  NI LAZIMA  KUPATA  MGAO  NDOA  INAPOVUNJIKA.

Hapo juu wakati naeleza maana ya neno mali za wanandoa  ambazo hustahili mgao ndoa inapovunjika nilieleza kuwa mali hizo inabidi ziwe zimepatikana kwa nguvu, juhudi au jitihada au mchango wa pamoja kipindi cha ndoa. Swali ni  nini maana nguvu, jitihada, au mchango  wa pamoja.

Watu wengi hujua kuwa juhudi au mchango wa pamoja unaopelekea mali kuwa za wote na hivyo kustashili mgao ndoa inapovunjika ni ile leta ni lete. Yaani kama ni nyumba inajengwa mume akitoa saruji mwanamke atoe nondo au mume akitoa hela na mwanamke atoe hela na kama ni gari mwanaume akitoa milioni kadhaa na mwanamke naye achangie za kwake kadhaa na hapo ndipo itakuwa mali yao wote  na eti  hapo ndipo mgao unapostahili. Hiyo ni maana  lakini finyu sana.

Maana ya kisheria  ya mchango au juhudi  za pamoja  hujumuisha kazi anazofanya mama nyumbani wakati baba akiwa nje ya nyumba kwa uzalishaji mali. Kuosha vyombo,kupika,usafi wa nyumbani,kutunza na kuandaa watoto,kufua, na kila kazi ya nyumbani  ni mchango  na juhudi  ya pamoja kwa maana niliyosema na lazima ilipwe  kwa kugawana mali ndoa inapovunjika. Kwa maana hii mama wa nyumbani hustahili mgao wa mali ndoa inapovunjika. Hii ni sheria  na kufanya hivyo ni lazima si hiari wala hisani ya mtu.

4. KWANINI  SHERIA  IMEAMURU  MGAO  WA  MALI  KWA  MAMA  WA  NYUMBANI.

Sheria  inamini kuwa wakati  wa ndoa  mwanamke huwa ametoa sadaka maisha yake  na utu wake katika kuwatunza watoto(kama wapo) na kuitumikia familia kwa ujumla  kwa kufanya  kazi  zote za nyumbani kitu ambacho humwekea ugumu wa kuzalisha pesa na baadhi ya mali zitokanazo na pesa. Sheria inaamini kuwa hilo  hutokana na nafasi yake hiyo ya kuwa mwangalizi wa nyumba wa muda wote. Hivyo basi haiwezi kuwa busara,hauwezi kuwa ubinadamu, hauwezi kuwa utu, hauwezi kuwa ustaarabu, haiwezi kuingia katika akili ya yoyote na haiwezi kamwe kuwa sawa kwa mwanamke kama huyo baada ya talaka asipate chochote na aondoke bila chochote baada ya kuwa amepoteza miaka mingi katika kuitumikia familia hiyo. Hii ndiyo sababu kuu ya  kumpa  mgao wa mali mama ambaye  hushinda  nyumbani.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.   PIA  NI   KATI   YA WANASHERIA  WAANZILISHI  WA  BLOG  HII . 0784482959,        0714047241              bashiryakub@ymail.com






0 comments:

Post a Comment