Tuesday 17 February 2015

JE UMECHOSHWA NA UNAHITAJI TALAKA ? FUATA HATUA HIZI


Na Image result for AMPIGA MKEWE

NA  BASHIR  YAKUB-

Kuomba talaka si dhambi. Kama lingekuwa dhambi sheria isingeruhusu jambo hilo kwakuwa si kawaida ya sheria  kuhamasishi madhambi.  Ni kwasababu hii nasema kuwa atakayeona amebanwa basi aombe talaka. Si kosa hata kidogo kufanya hivyo isipokuwa ndivyo tunavyoelekezwa  na sheria zetu tunazozipenda na kuziheshimu sana.

1.   KUVUNJIKA  KWA  NDOA.

Kuvunjika kwa ndoa kwa mujibu wa sheria zetu za Tanzania kuna mazingira mengi. Baadhi ya mazingira hayo ni yale yaliyoorodheshwa kifungu cha 12 (a-e) cha Sheria ya ndoa ambayo ni pamoja na kifo cha mmoja wa wanandoa,  talaka ambayo tunaiongelea  lakini  pia yapo mazingira  mengine mengi.

        2.   AINA   ZA   TALAKA

Talaka twaweza kuzigawa katika makundi mawili nayo ni, talaka itolewayo nje ya mahakama ambayo hutokana na ndoa zilizo katika mfumo wa kimila na nyingine ni talaka itolewayo  mahakamani ambayo sisi hapa tutaiongelea.

        3.   UKITAKA    TALAKA    FUATA    HATUA   HIZI.

( a ) Hatua ya  kwanza kabisa kwa anayehitaji kupata talaka ni  kupeleka malalamiko yako kwenye kitengo maalum kijulikanacho kama Bodi ya usuluhishi wa ndoa ambayo imeanzishwa na Sheria ya ndoa kifungu cha 102(1).

Bodi itasikiliza malalamiko  na kujaribu kufanya usuluhishi. Lengo la bodi ni kusuluhisha ambapo ikishindwa kusuluhisha itaandaa maelezo yanayohusiana na kilichojiri wakati wa usuluhishi ikiwa ni pamoja na kueleza namna ilivyoshindwa kusuluhisha. Sharti hili limewekwa ili kulinda ustawi wa familia   kwa kuwa kupitia bodi wakati mwingine kunarejesha mahusiano ambayo yalikuwa tayari kuvunjika.

    4.    BODI   YA  USULUHISHI  NI   IPI   NA   IKO  WAPI.

Kwa waislamu  bodi ya usuluhishi ni Bakwata.Hautakiwi kufika mahakamani kudai talaka mahakamani mpaka una  maelezo ya Bakwata kuwa umepitia kwao  na suluhu  imeshindikana.Ofisi za Bakwata zipo maeneo mbalimbali lakini haswaa ukiuliza misikitini watakuonesha.

Kwa wakiristo bodi  ya usuluhishi iko ustawi wa jamii. Hautakiwi kufika mahakamani kudai talaka  mpaka una maelezo kutoka ustawi wa jamii kuwa wamesuluhisha na imeshindikana. Ofisi za ustawi wa jamii zipo  katika makao makuu ya kila wilaya ukifika hapo uliza utaoneshwa.


 ( b ) Hatua ya kwanza tumeona ni kupitia hizo bodi za suluhu sasa   ni hatua ya pili ambayo ni mahakamani ambapo mwombaji atatakiwa kufika akiwa na kibali chake kutoka bodi kinachoonesha mwenendo wa usuluhishi na kushindwa kwa bodi kurejesha mahusiano. Ni katika mahakama ambapo mwombaji atatoa maelezo ya kuomba talaka huku akionesha sababu za kuishawishi mahakama hiyo ili ipitishe hukumu ya kuvunja ndoa. Kubwa zaidi atakalolionesha  ni kuwa ndoa hiyo haiwezekani tena hata kwa namna gani.

Kwahiyo hatua ni mbili tu ile ya  bodi ya usuluhishi  na unamalizia  na mahakamani.

5.SABABU ZA KISHERIA ZINAZOWEZA KUKUFANYA UOMBE   TALAKA   NI  HIZI.

( a ) Kwanza ni zinaa. Inapotokea kuwa mmoja   wa wanandoa amejamiiana na mtu mwingine ambaye si mme/mke wake na hali yupo katika ndoa  ni sababu ya kubwa ya kuombea talaka.

 ( b ) Sababu nyingine ambayo mtu anaweza kuitoa  akiwa anadai talaka  ni kunyimwa unyumba kunakoendelea. Linatumika neno kunyimwa unyumba kunakoendelea  kumaanisha kuwa haiwezekani mwanandoa  akanyimwa unyumba maramoja au mara mbili halafu akaamkia mahakamani kudai talaka. Kunyimwa unyumba ili iwe sababu inabidi kiwe ni kitendo chenye kuendelea  na si kitendo ambacho kimejitokeza maramoja au mara mbili. 

( c ) Tatu , ukatili nao ni sababu anayotumiwa na mwombaji kuombea talaka. Tunaweza kusema kuwa ukatili ni matendo ambayo hayakubaliki yanayofanywa kwa makusudi  na ambayo kimsingi yanaweza kusababisha  hatari kwa afya ya mtu na maisha yake kwa ujumla kama kumpiga mtu mara kwa mara, kumtukana mtu mara kwa mara, kumuumiza kwa aina yoyote ile, kumwingilia  mwenza wako kinyume na maumbile, ulevi wa kupindukia na wenye kuendelea, na mengine yote ambayo ni kinyume na ubinadamu. 



( d ) Nne, talaka inaweza kutolewa iwapo mmoja wa wanandoa amethibitisha mahakamani kuwa mwenzake amemtelekeza . Kumtelekeza  mtu katika ndoa kuna maana ya kujitoa katika mazingira ya uana ndoa  bila sababu za msingi  na bila ridhaa ya  mwenzako hata kama mnaishi chini ya paa moja.  Kwa hiyo kutelekezwa si tu kuondoka nyumbani  mnakoishi na mwenza wako isipokuwa hata kuishi pamoja lakini bila kushirikiana katika mambo mbalimbali  nako  ni kutengwa.

( e  ) Tano mtu anaweza kuomba talaka iwapo mwenzake amehukumiwa kifungo cha maisha  au kwa kipindi kisichoshuka miaka mitano. Kama mtu amehukumiwa kifungo  kama nilivyosema  ni hiari ya mwanandoa kuamua kuivunja kwa talaka au kusubiri.

MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI  LA  SERIKALI   LA   HABARI   LEO  KILA  JUMANNE  , GAZETI  JAMHURI   KILA  JUMANNE  NA  GAZETI  NIPASHE  KILA  JUMATANO.    0784482959, 0714047241
bashiryakub@ymail.com



2 comments:

  • Unknown says:
    25 March 2019 at 09:53

    Ahsante kwa ushauri mzuri

  • Unknown says:
    21 December 2021 at 15:50

    Asante kwa ufafanuzi

Post a Comment