Wednesday 12 September 2018

KULIPWA GHARAMA ZA KESI.


Image result for mahakamani


NA BASHIR  YAKUB -

Kuna tofauti kati ya gharama za kesi(costs), fidia (compesation), na faini(fine). Gharama za kesi ni nje ya haya lakini pia ni nje ya kile ulichoshinda. Kwasababu imeamriwa ulipwe fidia au imeamriwa ulipwe faini haimaanishi hata gharama zinahesabika humohumo. Laa, hasha, kama ni fidia utalipwa, kadhalika na gharama utatakiwa  kulipwa.

Ukweli ni kuwa watu wengi huwa hawadai gharama za kesi . Mtu akishaambiwa ameshinda basi. Kama imeamriwa alipwe pesa, au kama ni mali kama ardhi imeamriwa arudishiwe, au ushindi mwingine wowote basi  huondoka tu moja kwa moja bila kudai gharama zake. Sasa yafaa ujue kuwa nje ya ushindi unaopewa na mahakama pia unatakiwa kulipwa gharama zako za kuendeshea shauri/kesi.

1.GHARAMA ZA KESI NI NINI .

Gharama za kesi ni yale matumizi yote halali uliyoingia wakati ukishughulikia kesi/shauri husika. Hizi ni pamoja na nauli ulizokuwa ukitumia kutoka nyumbani kwenda mahakamani kwa kipindi chote cha kesi/shauri mpaka kuisha,pesa uliyomlipa wakili kama ulikuwa unawakilishwa na wakili, pesa uliyotumia kumlipa wakili kuandaa nyaraka , pesa ya kuchapa(print),pesa ya  kutoa kopi kwenye nyaraka mbalimbali ulizokuwa ukiwasilisha mahakamani, na gharama nyingine yoyote ambayo uliingia wakati ukifuatilia kesi/shauri.

Isipokuwa tu gharama hizo ziwe zile ambazo ni halali. Rushwa na gharama nyingine za ajabu ambazo umeingia haziwezi kulipwa na ni makosa iwapo ulifanya hivyo.

2. NANI HULIPA GHARAMA ZA KESI/SHAURI.

Aliyeshindwa hutakiwa kumlipa aliyeshinda. Mfumo wetu wa jumuia ya madola(common law) hakuna utaratibu wa kila mtu/upande kushinda(win win situation). Badala yake kuna mfumo wa shinda shindwa(win loose situation). Mmoja lazima atangazwe mshindi na mwingine mshindwa. 

 Kwahiyo yule aliyetangazwa kushindwa anawajibika kumlipa gharama  aliyeshinda. Na haijalishi iwapo huyo aliyeshinda alikuwa mlalamikaji/mshitaki, au alikuwa mlalamikiwa/mshitakiwa.Suala ni kwamba ameshinda basi alipwe gharama zake.

3.  NANI ANAAMRISHA GHARAMA KULIPWA.

Hakimu au jaji aliyekuwa anasikiliza shauri/kesi husika ndiye anayetoa amri ya kulipwa gharama. Isipokuwa wewe mlalamikaji au mlalamikiwa unatakiwa kuomba gharama hizo. Na wakati wa kuomba kulipwa gharama ni wakati ule kesi inapokuwa inaendelea. 

Gharama hazitolewi moja kwa moja ispokuwa unaomba. Na wakati wa kuomba ni huo wakati shauri/kesi inaendelea.

4. USHAHIDI KUWA UMETUMIA GHARAMA.

Ni muhimu sana wakati kesi ikiendelea kuwa unaomba kupewa,na kutunza risiti ya kila gharama unayoingia. Hata ukitoa kopi omba risiti ili ije kuwa ushahidi wako wa gharama. Gharama ambayo huna risiti yake inaweza kukataliwa. Hii husaidia pia kutotumia nafasi hiyo kumkomoa mtu ili alipe zaidi hata kwa kile ambacho hukutumia. 

Kwahiyo unashauriwa tangu siku ya kwanza uapopokea wito wa kuitwa mahakamani, au siku ya kwanza kufungua kesi/shauri, hakikisha kila hatua yako unakuwa na risiti ili uje kulipwa gharama zako.

5. WAKATI GANI GHARAMA HULIPWA.

Gharama hulipwa mwishoni kabisa baada ya kesi/shauri kuisha. Gharama haziwezi kulipwa kabla ya kesi/shauri kuisha kwasababu kabla ya hapo unakuwa hujajua umetumia kiasi gani. Kesi haijaisha maana yake bado unaendelea kutumia na hivyo huwezi kufanya majumuisho ya gharama.

 Kwahiyo gharama italipwa mwishoni kwakuwa hapo ndipo unapoweza kufanya majumuisho kuanzia mwanzo wa kesi/shauri lilipoanza hadi mwisho lilipoisha,na kujua umetumia kiasi gani.

Ni vema sasa ufahamu kuwa nje ya kushinda na kuambiwa ulipwe fidia, urudishiwe nyumba/kiwanja, au ushindi mwingine wowote, pia uwe unakumbuka kulipwa gharama ambazo umeingia katika kushitaki au kujitetea.
MWANDISHI   WA   MAKALA  HAYA   NI   MWANASHERIA  NA  MSHAURI   WA  SHERIA  KUPITIA  GAZETI   LA  JAMHURI   KILA   JUMANNE.  0784482959,  0714047241bashiryakub@ymail.com


0 comments:

Post a Comment